Nehemia 6:1-19

  • Kazi ya kujenga upya yaendelea kupingwa (1-14)

  • Ukuta wakamilika baada ya siku 52 (15-19)

6  Sasa mara tu Sanbalati, Tobia,+ Geshemu Mwarabu,+ na maadui wetu wengine wote walipoambiwa kwamba nimejenga upya+ ukuta na hakuna mwanya wowote ukutani (ingawa kufikia wakati huo sikuwa nimeweka milango kwenye malango),+  mara moja Sanbalati na Geshemu wakanitumia ujumbe wakisema: “Njoo, tupange wakati ili tukutane kwenye vijiji vya Bonde Tambarare la Ono.”+ Lakini walikuwa wakipanga njama ya kunidhuru.  Basi nikawatuma wajumbe kwao nikisema: “Ninafanya kazi kubwa sana, siwezi kushuka chini. Kwa nini kazi isimame ili nije kwenu?”  Wakanitumia ujumbe uleule mara nne, nami nikawapa jibu lilelile kila mara.  Kisha Sanbalati akamtuma mtumishi wake kwangu akiwa na ujumbe uleule mara ya tano, akaja na barua iliyokuwa wazi mkononi mwake.  Ilikuwa imeandikwa hivi: “Kuna habari zinazoenezwa katika mataifa, na Geshemu+ anasema pia kwamba wewe na Wayahudi mnapanga kuasi.+ Hii ndiyo sababu unajenga ukuta; na kulingana na habari hizo unataka kuwa mfalme wao.  Pia, umeweka manabii ili watangaze kukuhusu kotekote Yerusalemu, ‘Kuna mfalme katika Yuda!’ Na sasa mfalme atajulishwa mambo haya. Basi njoo, tuzungumzie jambo hili pamoja.”  Hata hivyo, nikamtumia jibu hili: “Hakuna jambo lolote unalosema ambalo limetendeka; umeyabuni wewe mwenyewe.”*  Kwa maana wote walikuwa wakijaribu kutuogopesha, wakisema: “Mikono yao italegea kazini, na kazi hiyo haitafanywa.”+ Sasa, ninasali, itie nguvu mikono yangu.+ 10  Kisha nikaenda nyumbani kwa Shemaya mwana wa Delaya mwana wa Mehetabeli, alipokuwa amejifungia ndani. Akasema: “Tupange wakati ili tukutane katika nyumba ya Mungu wa kweli, ndani ya hekalu, nasi tufunge milango ya hekalu, kwa maana wanakuja kukuua. Wanakuja kukuua usiku.” 11  Lakini nikasema: “Je, mtu kama mimi anapaswa kukimbia? Je, mtu kama mimi anaweza kuingia hekaluni na aendelee kuishi?+ Sitaingia!” 12  Ndipo nikatambua kwamba Mungu hakuwa amemtuma, bali Tobia na Sanbalati+ walikuwa wamemkodi ili atabiri maneno hayo kunihusu. 13  Alikuwa amekodiwa ili aniogopeshe na kunifanya nitende dhambi, kisha wawe na sababu ya kuniharibia sifa ili wanishutumu. 14  Ee Mungu wangu, mkumbuke Tobia+ na Sanbalati na matendo haya yote, na pia Noadia yule nabii wa kike na manabii wengine ambao daima walijaribu kuniogopesha. 15  Mwishowe ukuta ulikamilishwa katika siku ya 25 ya mwezi wa Eluli,* kwa muda wa siku 52. 16  Mara tu maadui wetu wote waliposikia habari hiyo na mataifa yote jirani yalipoona jambo hilo, wakaaibika sana,+ nao wakatambua kwamba kazi hii ilikuwa imefanywa kwa msaada wa Mungu wetu. 17  Siku hizo wakuu+ wa Yuda walikuwa wakimtumia Tobia barua nyingi, naye alikuwa akiwajibu. 18  Watu wengi huko Yuda walikuwa wameapa kumuunga mkono, kwa sababu alikuwa amemwoa binti ya Shekania mwana wa Ara,+ na Yehohanani mwanawe alikuwa amemwoa binti ya Meshulamu+ mwana wa Berekia. 19  Pia, kila mara walikuwa wakiniambia mambo mema kumhusu na kumjulisha mambo niliyosema. Naye Tobia alikuwa akinitumia barua za kuniogopesha.+

Maelezo ya Chini

Tnn., “yanatoka moyoni mwako.”