Nehemia 9:1-38

  • Watu waungama dhambi zao (1-38)

    • Yehova, Mungu anayesamehe (17)

9  Siku ya 24 ya mwezi huo, Waisraeli wakakusanyika; walikuwa wamefunga wakiwa wamevaa nguo za magunia na kujirushia mavumbi.+  Kisha wazao wa Waisraeli wakajitenga na wageni wote,+ wakasimama na kuungama dhambi zao wenyewe na makosa ya baba zao.+  Kisha wakasimama mahali walipokuwa na kusoma kwa sauti kitabu cha Sheria+ ya Yehova Mungu wao kwa robo siku;* na kwa robo nyingine ya siku walikuwa wakiungama na kumwinamia Yehova Mungu wao.  Yeshua, Bani, Kadmieli, Shebania, Buni, Sherebia,+ Bani, na Kenani wakasimama kwenye jukwaa+ la Walawi na kumlilia Yehova Mungu wao kwa sauti kubwa.  Nao Walawi, yaani, Yeshua, Kadmieli, Bani, Hashabneya, Sherebia, Hodia, Shebania, na Pethahia wakasema: “Simameni, msifuni Yehova Mungu wenu kwa umilele wote.*+ Na walisifu jina lako tukufu, ambalo limekwezwa juu kuliko baraka zote na sifa zote.  “Wewe peke yako ndiye Yehova;+ uliumba mbingu, naam, mbingu za mbingu na jeshi lake lote, dunia na vyote vilivyo juu yake, bahari na vyote vilivyomo. Nawe unavihifadhi vyote hai, na jeshi la mbinguni linakuinamia wewe.  Wewe ndiye Yehova Mungu wa kweli, uliyemchagua Abramu,+ ukamtoa katika jiji la Uru+ la Wakaldayo na ukampa jina Abrahamu.+  Nawe ukaona moyo wake ukiwa mwaminifu mbele zako;+ basi ukafanya agano naye ili umpe nchi ya Wakanaani, Wahiti, Waamori, Waperizi, Wayebusi, na Wagirgashi, ili kuupa uzao wake* nchi hiyo;+ nawe ukatimiza ahadi zako, kwa maana wewe ni mwadilifu.  “Basi ukaona mateso ya mababu zetu huko Misri,+ nawe ukasikia kilio chao kwenye Bahari Nyekundu. 10  Kisha ukafanya ishara na miujiza dhidi ya Farao na watumishi wake wote na watu wote wa nchi yake,+ kwa maana ulijua waliwatendea kwa kimbelembele.+ Ukajijengea jina ambalo limedumu hadi leo hii.+ 11  Nawe ukaitenganisha bahari mbele yao, wakavuka bahari juu ya nchi kavu,+ na wale waliowafuatia ukawatupa ndani ya maji mengi kama vile jiwe linavyotupwa ndani ya bahari iliyochafuka.+ 12  Uliwaongoza mchana kwa nguzo ya wingu, na usiku kwa nguzo ya moto, ili kuwaangazia njia waliyopaswa kupitia.+ 13  Nawe ukashuka kwenye Mlima Sinai+ ukazungumza nao kutoka mbinguni+ na kuwapa hukumu za uadilifu, sheria za kweli,* masharti bora na amri bora.+ 14  Ukawajulisha Sabato yako takatifu+ na kuwapa amri, masharti, na sheria kupitia Musa mtumishi wako. 15  Walipokuwa na njaa uliwapa mkate kutoka mbinguni,+ walipokuwa na kiu ukawapa maji kutoka kwenye mwamba,+ na ukawaambia waingie na kuimiliki nchi ambayo ulikuwa umeapa* kwamba utawapatia. 16  “Lakini mababu zetu, wakatenda kwa kimbelembele+ na kuwa wakaidi,*+ nao hawakusikiliza amri zako. 17  Walikataa kusikiliza+ wala hawakukumbuka matendo yako ya ajabu uliyofanya miongoni mwao, lakini wakawa wakaidi,* nao wakachagua kiongozi ili warudi Misri ambako walikuwa watumwa.+ Lakini wewe ni Mungu uliye tayari kusamehe,* mwenye huruma* na rehema, usiye mwepesi wa hasira, una upendo mwingi mshikamanifu,*+ nawe hukuwaacha.+ 18  Hata walipojitengenezea sanamu ya ndama wa chuma* na kusema, ‘Huyu ndiye Mungu wenu aliyewaongoza kutoka Misri,’+ nao wakatenda matendo makubwa ya ukosefu wa heshima, 19  hata wakati huo, kwa rehema zako nyingi, hukuwaacha nyikani.+ Nguzo ya wingu iliyowaongoza njiani mchana haikuondoka juu yao, wala nguzo ya moto iliyowaangazia njia usiku.+ 20  Nawe ukawapa roho yako njema ili iwape ufahamu,+ hukuwanyima mana vinywani mwao,+ na walipohisi kiu ukawapa maji.+ 21  Kwa miaka 40 uliwapa chakula nyikani.+ Hawakukosa chochote. Mavazi yao hayakuchakaa,+ wala miguu yao haikuvimba. 22  “Uliwapa falme na mataifa, ukawagawia kipande kwa kipande,+ nao wakamiliki nchi ya Sihoni,+ yaani, nchi ya mfalme wa Heshboni,+ na pia nchi ya Ogu+ mfalme wa Bashani. 23  Nawe ukawafanya wana wao kuwa wengi kama nyota za mbinguni.+ Kisha ukawaleta katika nchi ambayo ulikuwa umewaahidi mababu zao kwamba wanapaswa kuingia na kuimiliki.+ 24  Basi wana wao wakaingia na kuimiliki nchi hiyo,+ nawe ukawatiisha Wakanaani walioishi katika nchi hiyo,+ ukawatia mikononi mwao, wao pamoja na wafalme wao na wakaaji wa nchi, ili wawatendee wapendavyo. 25  Wakateka majiji yenye ngome+ na ardhi yenye rutuba,*+ wakamiliki nyumba zilizojaa vitu vyema vya kila aina, visima ambavyo tayari vilikuwa vimechimbwa, mashamba ya mizabibu, mizeituni,+ na miti ya matunda kwa wingi. Hivyo wakala na kushiba na kunenepa, nao wakaufurahia wema wako mwingi. 26  “Hata hivyo, hawakutii, bali walikuasi+ na kuigeuzia mgongo Sheria yako.* Wakawaua manabii wako waliowaonya wakurudie, nao wakatenda matendo makubwa ya ukosefu wa heshima.+ 27  Kwa sababu hiyo uliwatia mikononi mwa maadui wao,+ walioendelea kuwatesa.+ Lakini walipokuwa wakiteseka walikulilia, nawe uliwasikia ukiwa mbinguni; na kwa sababu ya rehema zako nyingi, uliwapa waokozi waliowaokoa kutoka mikononi mwa maadui wao.+ 28  “Lakini mara tu walipopata utulivu, walitenda tena yaliyo maovu mbele zako,+ nawe ulikuwa ukiwaacha mikononi mwa maadui wao, ambao waliwakandamiza.*+ Kisha walirudi na kukuomba msaada,+ nawe uliwasikiliza ukiwa mbinguni na kuwaokoa tena na tena kwa sababu ya rehema zako nyingi.+ 29  Ingawa uliwaonya ili wairudie Sheria yako, walitenda kwa kimbelembele na kukataa kusikiliza amri zako;+ nao wakatenda dhambi kwa kutofuata masharti yako, ambayo mtu akiyafuata ataishi.+ Lakini walikugeuzia mgongo na kufanya shingo zao ziwe ngumu, nao wakakataa kukusikiliza. 30  Uliwaonyesha subira+ kwa miaka mingi na ukaendelea kuwaonya kwa roho yako kupitia manabii wako, lakini walikataa kusikiliza. Mwishowe ukawatia mikononi mwa mataifa ya nchi hizo.+ 31  Na kwa sababu ya rehema zako nyingi, hukuwaangamiza+ wala kuwaacha, kwa maana wewe ni Mungu mwenye huruma* na rehema.+ 32  “Na sasa, Ee Mungu wetu, Mungu mkuu, mwenye nguvu, mwenye kuogopesha, unayeshika agano lako na kutenda kwa upendo mshikamanifu,+ usiyaone kuwa madogo mateso yote yaliyotupata sisi, wafalme wetu, wakuu wetu,+ makuhani wetu,+ manabii wetu,+ mababu zetu, na watu wako wote tangu siku za wafalme wa Ashuru+ mpaka leo hii. 33  Umekuwa mwadilifu katika mambo yote yaliyotupata, kwa maana umetenda kwa uaminifu; lakini ni sisi tuliotenda uovu.+ 34  Wafalme wetu, wakuu wetu, makuhani wetu, na mababu zetu hawajashika Sheria yako wala kusikiliza amri zako wala vikumbusho ulivyowapa* ili kuwaonya. 35  Hata walipokuwa kwenye ufalme wao wakifurahia wema mwingi uliowapa na katika nchi kubwa na yenye rutuba* uliyowapa, hawakukutumikia+ wala kuacha mazoea yao maovu. 36  Basi leo hii sisi ni watumwa+—naam, watumwa katika nchi ambayo uliwapa mababu zetu ili wale matunda yake na vitu vyake vyema. 37  Mazao yake mengi ni ya wafalme uliowafanya watutawale kwa sababu ya dhambi zetu.+ Wanatutawala wapendavyo na kuitendea mifugo yetu wapendavyo, tunateseka sana. 38  “Basi kwa sababu ya hayo yote, tunafanya mapatano thabiti+ kwa maandishi, nayo yamethibitishwa kwa muhuri wa wakuu wetu, Walawi wetu, na makuhani wetu.”+

Maelezo ya Chini

Au “kwa saa tatu.”
Au “milele hata milele.”
Tnn., “mbegu yake.”
Au “sheria zinazotegemeka.”
Tnn., “uliinua mkono wako.”
Tnn., “na kufanya shingo yao kuwa ngumu.”
Au “fadhili nyingi zenye upendo.”
Au “neema.”
Au “Mungu mwenye matendo ya kusamehe.”
Tnn., “wakafanya shingo yao kuwa ngumu.”
Au “sanamu ya kuyeyushwa.”
Au “iliyonona.”
Tnn., “kuitupa Sheria yako nyuma yao.”
Au “waliwaponda.”
Au “neema.”
Au “maonyo uliyowapa.”
Au “iliyonona.”