Ruthu 1:1-22

  • Elimeleki na familia yake wahamia Moabu (1, 2)

  • Naomi, Orpa, na Ruthu wafiwa na waume zao (3-6)

  • Ruthu aonyesha ushikamanifu kwa Naomi na kwa Mungu wa Naomi (7-17)

  • Naomi arudi Bethlehemu pamoja na Ruthu (18-22)

1  Basi katika siku ambazo waamuzi+ walikuwa wakitekeleza hukumu,* kulikuwa na njaa kali nchini; na mwanamume fulani akatoka Bethlehemu+ huko Yuda akahamia katika mashamba ya* Moabu akiwa mgeni,+ yeye, pamoja na mke wake, na watoto wake wawili wa kiume.  Mwanamume huyo aliitwa Elimeleki,* na mke wake aliitwa Naomi,* na watoto wake wawili waliitwa Maloni* na Kilioni.* Walikuwa Waefrathi kutoka Bethlehemu nchini Yuda. Wakafika katika mashamba ya Moabu na kuishi huko.  Baada ya muda, Elimeleki mume wa Naomi akafa, naye akabaki na wanawe wawili.  Baadaye wana hao wakaoa wanawake Wamoabu; mmoja aliitwa Orpa, na mwingine aliitwa Ruthu.+ Waliishi huko kwa miaka kumi hivi.  Kisha wana hao wawili, Maloni na Kilioni wakafa pia, Naomi akabaki bila watoto wake wawili na bila mume wake.  Akaanza safari kutoka katika mashamba ya Moabu pamoja na binti wakwe zake, kwa maana akiwa Moabu alisikia kwamba Yehova alikuwa amewaelekezea uangalifu watu Wake kwa kuwapa chakula.*  Akaondoka mahali alipokuwa akiishi pamoja na binti wakwe zake wawili. Walipokuwa wakitembea njiani kurudi katika nchi ya Yuda,  Naomi akawaambia: “Nendeni, rudini kila mmoja wenu nyumbani kwa mama yake. Yehova na awatendee kwa upendo mshikamanifu,+ kama tu mlivyowatendea waume zenu ambao wamekufa na kama mlivyonitendea mimi.  Yehova na awabariki* ili kila mmoja wenu apate usalama* katika nyumba ya mume wake.”+ Kisha akawabusu, nao wakalia kwa sauti kubwa. 10  Wakamwambia tena na tena: “Hapana, tutaenda nawe kwa watu wako.” 11  Lakini Naomi akawaambia: “Rudini binti zangu. Kwa nini mnifuate? Je, ninaweza tena kuzaa watoto ambao watakuwa waume zenu?+ 12  Rudini, binti zangu. Nendeni, kwa maana nimezeeka sana siwezi kuolewa tena. Hata kama ningetumaini kupata mume usiku wa leo na kuzaa watoto pia, 13  je, mngeendelea kuwangojea ili wakue? Je, mngekataa kuolewa tena mkiwasubiri? Hapana, binti zangu, nina uchungu mwingi kwa ajili yenu, kwa sababu mkono wa Yehova umegeuka dhidi yangu.”+ 14  Wakalia tena kwa sauti kubwa, kisha Orpa akambusu mama mkwe wake na kwenda zake. Lakini Ruthu akashikamana naye. 15  Kwa hiyo Naomi akamwambia: “Tazama! Dada mkwe mwenzako mjane amerudi kwa watu wake na kwa miungu yake. Rudi pamoja na dada mkwe mwenzako.” 16  Lakini Ruthu akasema: “Usinisihi nikuache, nirudi na kuacha kukufuata; kwa maana mahali utakapoenda nitaenda, na mahali utakapolala usiku hapo ndipo nitakapolala pia. Watu wako watakuwa watu wangu, na Mungu wako atakuwa Mungu wangu.+ 17  Mahali utakapokufa nitafia hapo, na hapo ndipo nitakapozikwa. Yehova na aniadhibu, tena vikali, ikiwa kitu chochote kitanitenganisha nawe isipokuwa kifo.” 18  Naomi alipoona kwamba Ruthu anasisitiza kwenda naye, hakuendelea kumsihi asimfuate. 19  Wote wawili wakaendelea na safari mpaka walipofika Bethlehemu.+ Mara tu walipofika Bethlehemu, jiji lote likasisimka kwa sababu yao, na wanawake wakaulizana: “Je, huyu ni Naomi?” 20  Naye aliwaambia: “Msiniite Naomi.* Niiteni Mara,* kwa maana Mweza-Yote amefanya maisha yawe machungu sana kwangu.+ 21  Mikono yangu ilikuwa imejaa nilipoenda, lakini Yehova amenifanya nirudi mikono mitupu. Kwa nini mniite Naomi, wakati Yehova ndiye aliyenipinga na Mweza-Yote ndiye aliyeniletea msiba?”+ 22  Hivyo ndivyo Naomi alivyorudi kutoka katika mashamba ya Moabu+ pamoja na Ruthu, binti mkwe wake Mmoabu. Walifika Bethlehemu mwanzoni mwa mavuno ya shayiri.+

Maelezo ya Chini

Tnn., “wakihukumu.”
Au “eneo la.”
Maana yake “Mungu Wangu Ni Mfalme.”
Maana yake “Uzuri Wangu.”
Labda linatokana na neno la Kiebrania linalomaanisha “kuwa dhaifu; kuwa mgonjwa.”
Maana yake “Anayeshindwa; Anayefikia Mwisho.”
Tnn., “mkate.”
Tnn., “apate mahali pa kupumzika.”
Tnn., “awape zawadi.”
Maana yake “Uzuri Wangu.”
Maana yake “Uchungu.”