Ruthu 2:1-23

  • Ruthu aokota masuke ya nafaka katika shamba la Boazi (1-3)

  • Ruthu na Boazi wakutana (4-16)

  • Ruthu amweleza Naomi kuhusu fadhili za Boazi (17-23)

2  Basi Naomi alikuwa na mtu wa ukoo wa Elimeleki, mume wake; mtu huyo aliitwa Boazi+ na alikuwa tajiri sana.  Ruthu Mmoabu akamwambia Naomi: “Tafadhali, niruhusu niende mashambani nikaokote masalio+ ya masuke ya nafaka nyuma ya yeyote yule atakayeniruhusu.” Basi Naomi akamwambia: “Nenda, binti yangu.”  Basi akaenda na kuanza kuokota masalio mashambani nyuma ya wavunaji. Bila kutarajia akajikuta katika shamba la Boazi,+ aliyekuwa wa ukoo wa Elimeleki.+  Ndipo Boazi akaja kutoka Bethlehemu na kuwaambia wavunaji: “Yehova na awe pamoja nanyi.” Nao wakajibu: “Yehova na akubariki.”  Kisha Boazi akamuuliza kijana aliyekuwa msimamizi wa wavunaji: “Msichana huyu ni wa nani?”  Kijana aliyekuwa msimamizi wa wavunaji akamjibu: “Msichana huyu ni Mmoabu,+ aliyerudi na Naomi kutoka katika mashamba ya Moabu.+  Aliniuliza, ‘Tafadhali, ninaweza kuokota+ na kukusanya masuke* ya nafaka yaliyoachwa na wavunaji?’ Amekuwa akifanya kazi tangu alipokuja asubuhi, ni sasa tu ameketi kibandani ili kupumzika kidogo.”  Kisha Boazi akamwambia Ruthu: “Sikiliza, binti yangu. Usiende kuokota masalio katika shamba lingine, wala usiende mahali pengine popote; uwe karibu na wafanyakazi wangu wasichana.+  Angalia shamba wanalovuna, nawe uwafuate. Nimewaamuru wale vijana wa kiume wasikuguse.* Ukihisi kiu, nenda kwenye mitungi ya maji ukanywe maji yaliyotekwa na hao vijana.” 10  Ndipo Ruthu akapiga magoti na kuinama mpaka chini na kumwambia: “Nimepataje kibali machoni pako, na kwa nini umenijali ilhali mimi ni mgeni?”+ 11  Boazi akamjibu: “Nimeambiwa mambo yote uliyomfanyia mama mkwe wako baada ya mume wako kufa na jinsi ulivyomwacha baba yako na mama yako na nchi ya watu wako wa ukoo ukaja kwa watu ambao hukuwajua.+ 12  Yehova na akuthawabishe kwa yale uliyofanya,+ na upate malipo* kamili kutoka kwa Yehova Mungu wa Israeli, ambaye umekuja kutafuta kimbilio chini ya mabawa yake.”+ 13  Basi Ruthu akasema: “Acha nipate kibali machoni pako, bwana wangu, kwa sababu umenifariji na kunitia moyo,* ingawa mimi hata si mmoja wa watumishi wako.” 14  Wakati wa chakula, Boazi akamwambia: “Njoo hapa, ule mkate na kuuchovya katika siki.” Basi Ruthu akaketi kando ya wavunaji. Boazi akampa nafaka zilizokaangwa, akala, akashiba, na kubakiza. 15  Aliposimama ili aokote masuke ya nafaka,+ Boazi akawaamuru hivi watumishi wake: “Mwacheni aokote masuke* ya nafaka yaliyokatwa pia, msimtese.+ 16  Pia, hakikisheni kwamba mnachomoa masuke machache kutoka katika matita na kumwachia nyuma ili ayaokote, msimkataze.” 17  Basi akaendelea kuokota masuke shambani mpaka jioni.+ Alipoyapura, alipata karibu efa* moja ya shayiri. 18  Halafu akachukua nafaka hiyo na kwenda jijini, na mama mkwe wake akaona nafaka aliyokuwa ameokota. Halafu Ruthu akachukua chakula alichokuwa amebakiza+ baada ya kula na kushiba, akampa. 19  Basi mama mkwe wake akamuuliza: “Leo uliokota masuke wapi? Ulifanya kazi wapi? Na abarikiwe yule aliyekutendea kwa fadhili.”+ Ndipo akamwambia mama mkwe wake kuhusu mtu aliyefanya kazi katika shamba lake: “Nilifanya kazi katika shamba la mwanamume anayeitwa Boazi.” 20  Basi Naomi akamwambia binti mkwe wake: “Na abarikiwe na Yehova, ambaye hajawahi kamwe kukosa kuwatendea kwa upendo mshikamanifu walio hai na waliokufa.”+ Naomi akaendelea kusema: “Mwanamume huyo ni mtu wetu wa ukoo.+ Yeye ni kati ya watu wanaoweza kutukomboa.”*+ 21  Ndipo Ruthu Mmoabu akasema: “Pia aliniambia, ‘Uwe karibu na watumishi wangu mpaka watakapomaliza kuvuna mavuno yangu yote.’”+ 22  Naomi akamwambia Ruthu binti mkwe wake: “Binti yangu, ni afadhali ufuatane na wafanyakazi wake wasichana, usije ukasumbuliwa katika shamba lingine.” 23  Kwa hiyo akafuatana na wasichana wa Boazi na kuokota masuke mpaka mwisho wa mavuno ya shayiri+ na mavuno ya ngano. Naye akaendelea kuishi na mama mkwe wake.+

Maelezo ya Chini

Au labda, “matita.”
Au “wasikusumbue.”
Au “thawabu.”
Tnn., “umezungumza na moyo wangu.”
Au labda, “matita.”
Karibu kilogramu 13. Angalia Nyongeza B14.
Au “mmojawapo wa watu wetu wa ukoo walio na haki ya kutukomboa.”