Ufunuo kwa Yohana 10:1-11

  • Malaika mwenye nguvu akiwa na kitabu kidogo cha kukunjwa (1-7)

    • “Hakuna kukawia tena” (6)

    • Siri takatifu itakamilika (7)

  • Yohana ala kile kitabu kidogo cha kukunjwa (8-11)

10  Nami nikamwona malaika mwingine mwenye nguvu akishuka kutoka mbinguni, akiwa amepambwa* wingu, na upinde wa mvua ulikuwa juu ya kichwa chake, na uso wake ulikuwa kama jua,+ na miguu yake ilikuwa kama nguzo za moto,  na mkononi mwake alikuwa na kitabu kidogo cha kukunjwa kilichofunguliwa. Naye akaweka mguu wake wa kuume juu ya bahari, na mguu wa kushoto juu ya dunia,  naye akapaza sauti kubwa kama simba anaponguruma.+ Na alipopaza sauti, sauti za zile ngurumo saba+ zikazungumza.  Basi zile ngurumo saba zilipozungumza, nilikuwa karibu kuandika; lakini nikasikia sauti kutoka mbinguni+ ikisema: “Yatie muhuri mambo ambayo zile ngurumo saba zilisema, nawe usiyaandike.”  Malaika niliyemwona amesimama juu ya bahari na juu ya dunia akainua mkono wake wa kuume kuelekea mbinguni,  naye akaapa kwa Yule anayeishi milele na milele,+ aliyeiumba mbingu na vitu vilivyo ndani yake na dunia na vitu vilivyo ndani yake na bahari na vitu vilivyo ndani yake:+ “Hakuna kukawia tena.  Lakini katika siku ambazo yule malaika wa saba+ atakuwa karibu kuipiga tarumbeta yake,+ ile siri takatifu+ ambayo Mungu aliwatangazia ikiwa habari njema watumwa wake manabii+ itamalizika.”  Nami nikasikia sauti kutoka mbinguni+ ikisema nami tena na kuniambia: “Nenda, ukichukue kile kitabu cha kukunjwa kilichofunguliwa, kilicho mkononi mwa malaika ambaye amesimama juu ya bahari na juu ya dunia.”+  Nikaenda kwa yule malaika na kumwambia anipe kile kitabu kidogo cha kukunjwa. Akaniambia: “Kichukue ukile,+ nacho kitafanya tumbo lako liwe na uchungu, lakini kinywani mwako kitakuwa kitamu kama asali.” 10  Nikakichukua kile kitabu kidogo cha kukunjwa kutoka mkononi mwa yule malaika nikakila,+ na kinywani mwangu kilikuwa kitamu kama asali,+ lakini baada ya kukila, tumbo langu likawa na uchungu. 11  Nao wakaniambia: “Lazima utoe unabii tena kuhusu jamii na mataifa na lugha na wafalme wengi.”

Maelezo ya Chini

Au “amefunikwa.”