Ufunuo kwa Yohana 9:1-21

  • Tarumbeta ya tano (1-11)

  • Ole wa kwanza umepita, mbili zaidi zinakuja (12)

  • Tarumbeta ya sita (13-21)

9  Malaika wa tano akaipiga tarumbeta yake.+ Nami nikaona nyota iliyokuwa imeanguka kutoka mbinguni mpaka duniani, naye akapewa ufunguo wa shimo refu lisilo na mwisho.*+  Akalifungua shimo refu lisilo na mwisho,* na moshi ukapanda kutoka katika lile shimo kama moshi wa tanuru kubwa, na jua likatiwa giza,+ pia hewa, kwa moshi wa lile shimo.  Na nzige wakatoka katika moshi huo wakaja duniani,+ nao wakapewa mamlaka, mamlaka kama ile ya nge wa dunia.  Wakaambiwa wasidhuru majani ya dunia au mmea wowote au mti wowote, isipokuwa watu wasio na muhuri wa Mungu kwenye mapaji ya nyuso zao.+  Na nzige hao walipewa ruhusa, si ya kuwaua, bali ya kuwatesa kwa miezi mitano, na mateso yao yalikuwa kama mateso ya mtu anapoumwa na nge.+  Katika siku hizo watu watatafuta kifo lakini hawatakipata kamwe, nao watatamani kufa, lakini kifo kitawakimbia.  Wale nzige walionekana kama farasi waliotayarishwa kwa ajili ya vita;+ na juu ya vichwa vyao kulikuwa na kitu kilichoonekana kama mataji ya dhahabu, na nyuso zao zilikuwa kama nyuso za wanadamu,  lakini walikuwa na nywele kama nywele za wanawake. Na meno yao yalikuwa kama ya simba,+  nao walikuwa na mabamba ya kifuani kama mabamba ya kifuani ya chuma. Na sauti ya mabawa yao ilikuwa kama sauti ya magari ya farasi yakikimbia kwenda vitani.+ 10  Pia, wana mikia yenye miiba kama nge, na katika mikia yao wana mamlaka ya kuumiza watu kwa miezi mitano.+ 11  Wana mfalme juu yao, yule malaika wa shimo refu lisilo na mwisho.*+ Katika Kiebrania jina lake ni Abadoni,* lakini katika Kigiriki jina lake ni Apolioni.* 12  Ole mmoja umepita. Tazama! Ole mbili zaidi+ zinakuja baada ya mambo haya. 13  Malaika wa sita+ akaipiga tarumbeta yake.+ Nami nikasikia sauti moja kutoka katika zile pembe za madhabahu ya dhahabu+ iliyo mbele za Mungu 14  ikimwambia malaika wa sita aliyekuwa na tarumbeta: “Wafungue malaika wanne waliofungwa kwenye mto mkubwa Efrati.”+ 15  Na wale malaika wanne, ambao wametayarishwa kwa ajili ya ile saa na siku na mwezi na mwaka wakafunguliwa ili waue theluthi moja ya watu. 16  Idadi ya majeshi ya wapanda farasi ilikuwa makumi mawili ya maelfu ya makumi ya maelfu;* niliisikia idadi yao. 17  Na hivi ndivyo nilivyowaona wale farasi katika maono na wale walioketi juu yao: Walikuwa na mabamba ya kifuani ya rangi nyekundu ya moto na ya bluu ya hayasinthi na ya manjano ya kiberiti, na vichwa vya wale farasi vilikuwa kama vichwa vya simba,+ na moto na moshi na kiberiti vilitoka katika vinywa vyao. 18  Theluthi moja ya watu iliuawa kwa hayo mapigo matatu, kwa ule moto na moshi na kiberiti vilivyotoka katika vinywa vyao. 19  Kwa maana mamlaka ya wale farasi imo katika vinywa vyao na katika mikia yao, kwa maana mikia yao ni kama nyoka na ina vichwa, nao wanaitumia kudhuru. 20  Lakini watu waliobaki ambao hawakuuawa kwa yale mapigo hawakutubu matendo ya mikono yao; hawakuacha kuabudu roho waovu na sanamu za dhahabu na fedha na shaba na mawe na miti, ambazo haziwezi kuona wala kusikia wala kutembea.+ 21  Nao hawakutubu mauaji yao wala mazoea yao ya kuwasiliana na roho wala uasherati* wao wala wizi wao.

Maelezo ya Chini

Au “abiso.” Angalia Kamusi.
Au “abiso.” Angalia Kamusi.
Maana yake “Mwangamizaji.”
Maana yake “Uharibifu.”
Au “abiso.” Angalia Kamusi.
Au “20,000 mara 10,000,” yaani, 200,000,000.
Neno la Kigiriki, por·neiʹa. Angalia Kamusi.