Waamuzi 1:1-36

  • Ushindi wa kabila la Yuda na la Simeoni (1-20)

  • Wayebusi waendelea kuishi Yerusalemu (21)

  • Yosefu achukua Betheli (22-26)

  • Wakanaani hawakufukuzwa wote (27-36)

1  Baada ya kifo cha Yoshua,+ Waisraeli* walimuuliza Yehova,+ “Ni nani kati yetu atakayeenda kwanza kupigana na Wakanaani?”  Yehova akawajibu, “Kabila la Yuda litaenda kwanza kupigana nao.+ Tazama! Ninaitia nchi hiyo mikononi mwao.”*  Ndipo watu wa kabila la Yuda wakawaambia ndugu zao wa kabila la Simeoni, “Twendeni pamoja katika eneo tulilopewa*+ tukapigane na Wakanaani. Nasi tutaenda nanyi katika eneo mlilopewa.” Basi watu wa kabila la Simeoni wakaenda pamoja nao.  Watu wa kabila la Yuda walipoenda, Yehova akawatia Wakanaani na Waperizi mikononi mwao,+ wakawashinda watu 10,000 huko Bezeki.  Wakamkuta Adoni-bezeki huko Bezeki, wakapigana naye na kuwashinda Wakanaani+ na Waperizi.+  Adoni-bezeki akakimbia, wakamkimbiza na kumshika, wakamkata vidole gumba vya mikono na vya miguu.  Kisha Adoni-bezeki akasema, “Kuna wafalme 70 waliokatwa vidole gumba vya mikono na vya miguu wanaookota chakula chini ya meza yangu. Mungu amenilipa kulingana na matendo yangu.” Baadaye wakampeleka Yerusalemu,+ akafia huko.  Kisha watu wa Yuda wakashambulia jiji la Yerusalemu+ na kuliteka; wakawaua wakaaji wake kwa upanga na kuliteketeza jiji.  Baadaye watu wa Yuda wakaenda kupigana na Wakanaani waliokaa katika eneo lenye milima na waliokaa Negebu na Shefela.+ 10  Basi watu wa kabila la Yuda wakawashambulia Wakanaani waliokaa Hebroni (zamani Hebroni liliitwa Kiriath-arba), nao wakamuua Sheshai, Ahimani, na Talmai.+ 11  Kisha wakawashambulia wakaaji wa Debiri.+ (Hapo awali Debiri liliitwa Kiriath-seferi.)+ 12  Ndipo Kalebu+ akasema, “Yeyote atakayeshambulia na kuteka jiji la Kiriath-seferi, nitampa binti yangu Aksa awe mke wake.”+ 13  Othnieli+ mwana wa Kenasi,+ ndugu mdogo wa Kalebu, akaliteka. Kwa hiyo akampa Aksa binti yake awe mke wake. 14  Mwanamke huyo alipokuwa akienda nyumbani kwake, akamsihi mume wake amwombe baba* yake shamba. Kisha mwanamke huyo akashuka kutoka juu ya punda wake.* Kalebu akamuuliza: “Unataka nini?” 15  Akamwambia, “Tafadhali nibariki, kwa maana umenipa shamba upande wa kusini;* nipe pia Guloth-maimu.”* Basi Kalebu akampa Gulothi ya Juu na Gulothi ya Chini. 16  Na wazao wa Mkeni,+ baba mkwe wa Musa,+ walitoka katika lile jiji la mitende+ pamoja na watu wa Yuda na kwenda katika nyika ya Yuda, upande wa kusini wa Aradi.+ Wakakaa huko pamoja na wenyeji.+ 17  Lakini watu wa kabila la Yuda wakasonga mbele pamoja na ndugu zao wa kabila la Simeoni, wakawashambulia Wakanaani waliokaa Sefathi na kuliangamiza jiji hilo.+ Kwa hiyo wakaliita Horma.*+ 18  Kisha watu wa kabila la Yuda wakateka Gaza+ na eneo lake, Ashkeloni+ na eneo lake, na Ekroni+ na eneo lake. 19  Yehova alikuwa pamoja na watu wa kabila la Yuda, nao wakamiliki eneo lenye milima, lakini hawakuweza kuwafukuza wakaaji wa bondeni,* kwa sababu walikuwa na magari ya vita yenye miundu ya chuma.*+ 20  Wakampa Kalebu jiji la Hebroni, kama Musa alivyoahidi,+ naye akawafukuza kutoka humo wale wana watatu wa Anaki.+ 21  Lakini Wabenjamini hawakuwafukuza Wayebusi waliokaa Yerusalemu, kwa hiyo Wayebusi wanakaa na Wabenjamini jijini Yerusalemu mpaka leo.+ 22  Wakati huo, watu wa nyumba ya Yosefu+ wakashambulia Betheli, na Yehova alikuwa pamoja nao.+ 23  Na nyumba ya Yosefu ikatuma watu wakapeleleze jiji la Betheli (zamani liliitwa Luzi),+ 24  na wapelelezi hao wakamwona mtu akitoka jijini. Wakamwambia, “Tafadhali tuonyeshe njia ya kuingia jijini, nasi tutakutendea kwa fadhili.”* 25  Basi akawaonyesha njia ya kuingia jijini, kisha wakawaua watu wote kwa upanga, lakini wakamwacha huru mtu huyo na familia yake.+ 26  Naye akaenda katika nchi ya Wahiti, akajenga jiji na kuliita Luzi. Hilo ndilo jina la jiji hilo mpaka leo. 27  Watu wa kabila la Manase hawakumiliki Beth-sheani na miji yake,* Taanaki+ na miji yake, Dori na miji yake, Ibleamu na miji yake, na Megido na miji yake.+ Wakanaani hawakukubali kutoka katika nchi hiyo. 28  Waisraeli walipopata nguvu, waliwatumikisha Wakanaani,+ lakini hawakuwafukuza wote.+ 29  Wala Waefraimu hawakuwafukuza Wakanaani waliokaa Gezeri. Wakanaani waliendelea kukaa kati yao huko Gezeri.+ 30  Watu wa kabila la Zabuloni hawakuwafukuza wakaaji wa Kitroni na wakaaji wa Nahaloli.+ Wakanaani waliendelea kukaa kati yao na kufanya kazi za kulazimishwa.+ 31  Waasheri hawakuwafukuza wakaaji wa Ako, Sidoni,+ Alabu, Akzibu,+ Helba, Afiki,+ na Rehobu.+ 32  Basi Waasheri wakaendelea kukaa kati ya Wakanaani waliokaa katika nchi hiyo, kwa sababu hawakuwafukuza. 33  Watu wa kabila la Naftali hawakuwafukuza wakaaji wa Beth-shemeshi na Beth-anathi,+ lakini waliendelea kukaa kati ya Wakanaani.+ Wakawatumikisha wakaaji wa Beth-shemeshi na wa Beth-anathi. 34  Waamori waliwazuia watu wa kabila la Dani wasishuke bondeni,* hivyo wakabaki milimani.+ 35  Kwa hiyo Waamori hawakukubali kutoka kwenye Mlima Heresi, na Aiyaloni,+ na Shaalbimu.+ Lakini watu wa nyumba ya Yosefu walipopata nguvu zaidi, waliwatumikisha. 36  Eneo la Waamori lilianzia kwenye mwinuko wa Akrabimu,+ kuanzia Sela kwenda milimani.

Maelezo ya Chini

Tnn., “wana wa Israeli.”
Au “Nimewapa nchi hiyo.”
Tnn., “kura yangu.”
Yaani, baba ya Aksa.
Au labda, “akapiga makofi akiwa juu ya punda ili kumwita baba yake.”
Au “eneo la Negebu.”
Yaani, “Chemchemi za (Mabakuli ya) Maji.”
Maana yake “Maangamizi.”
Au “nchi tambarare ya chini.”
Tnn., “magari ya chuma.”
Tnn., “tutakuonyesha upendo mshikamanifu.”
Au “miji jirani.”
Au “nchi tambarare ya chini.”