Waamuzi 10:1-18

  • Waamuzi Tola na Yairi (1-5)

  • Waisraeli waasi na kutubu (6-16)

  • Waamoni wataka kuwashambulia Waisraeli (17, 18)

10  Baada ya Abimeleki, alitokea Tola mwana wa Pua, mwana wa Dodo, wa kabila la Isakari, ili awaokoe Waisraeli.+ Aliishi Shamiri katika eneo lenye milima la Efraimu.  Alikuwa mwamuzi wa Waisraeli kwa miaka 23. Kisha akafa na kuzikwa huko Shamiri.  Baada yake akatokea Yairi Mgileadi, naye akawa mwamuzi wa Waisraeli kwa miaka 22.  Alikuwa na wana 30 waliopanda juu ya punda 30, nao walikuwa na majiji 30 katika nchi ya Gileadi, ambayo mpaka leo yanaitwa Hawoth-yairi.+  Kisha Yairi akafa na kuzikwa huko Kamoni.  Waisraeli wakaanza tena kutenda maovu machoni pa Yehova,+ nao wakaanza kuabudu Mabaali,+ sanamu za Ashtorethi, miungu ya Aramu,* miungu ya Sidoni, miungu ya Moabu,+ miungu ya Waamoni,+ na miungu ya Wafilisti.+ Wakamwacha Yehova wala hawakuendelea kumtumikia.  Basi hasira ya Yehova ikawaka dhidi ya Waisraeli, naye akawatia mikononi mwa Wafilisti na Waamoni.+  Kwa hiyo wakawatesa na kuwakandamiza sana Waisraeli mwaka huo—kwa miaka 18 waliwakandamiza Waisraeli wote waliokuwa ng’ambo ya Yordani katika nchi iliyokuwa ya Waamori kule Gileadi.  Waamoni pia walikuwa wakivuka Yordani ili kupigana na watu wa kabila la Yuda, Benjamini, na Efraimu; Waisraeli wakataabika sana. 10  Ndipo Waisraeli wakamlilia Yehova awasaidie,+ wakisema, “Tumekutendea dhambi Mungu wetu kwa sababu tumekuacha na kuabudu Mabaali.”+ 11  Lakini Yehova akawaambia Waisraeli, “Je, sikuwaokoa kutoka Misri+ na kutoka mikononi mwa Waamori,+ Waamoni, Wafilisti,+ 12  Wasidoni, Waamaleki, na Wamidiani walipokuwa wakiwakandamiza? Mliponililia, niliwaokoa kutoka mikononi mwao. 13  Lakini mliniacha na kuabudu miungu mingine.+ Ndiyo sababu sitawaokoa tena.+ 14  Nendeni mkaililie miungu mliyochagua iwasaidie.+ Na iwaokoe kutoka katika taabu yenu.”+ 15  Lakini Waisraeli wakamwambia Yehova, “Tumetenda dhambi. Tutendee upendavyo. Lakini tunakusihi utuokoe leo hii.” 16  Wakaondoa miungu ya kigeni waliyokuwa nayo na kumtumikia Yehova,+ naye hakuweza tena kuvumilia* kuwaona Waisraeli wakiteseka.+ 17  Baadaye Waamoni+ wakakusanyika na kupiga kambi huko Gileadi. Nao Waisraeli wakakusanyika na kupiga kambi huko Mispa. 18  Ndipo wakaaji wa Gileadi na wakuu wao wakaulizana, “Ni nani atakayetuongoza kupigana na Waamoni?+ Atakayefanya hivyo atakuwa kiongozi wa wakaaji wote wa Gileadi.”

Maelezo ya Chini

Au “Siria.”
Au “na nafsi yake ikakosa subira kwa sababu ya.”