Waamuzi 12:1-15

  • Apigana na Waefraimu (1-7)

    • Jaribio la kutamka Shibolethi (6)

  • Waamuzi Ibzani, Eloni, na Abdoni (8-15)

12  Watu wa kabila la Efraimu wakaitwa, nao wakavuka na kufika Zafoni,* wakamuuliza Yeftha, “Kwa nini hukutuita ulipovuka kwenda kupigana na Waamoni?+ Tutakuteketeza pamoja na nyumba yako.”  Lakini Yeftha akawaambia, “Mimi na watu wangu tulikuwa na ugomvi mkubwa pamoja na Waamoni. Nikawaomba ninyi mnisaidie, lakini hamkuniokoa kutoka mikononi mwao.  Nilipoona kwamba hamji kuniokoa, nikaamua kuhatarisha uhai wangu* na kwenda kupigana na Waamoni,+ na Yehova akawatia mikononi mwangu. Basi kwa nini mmekuja kupigana nami leo?”  Ndipo Yeftha akawakusanya watu wote wa Gileadi,+ wakapigana na watu wa Efraimu; na watu wa Gileadi wakawashinda Waefraimu kwa kuwa walisema, “Ninyi watu wa Gileadi ni wakimbizi tu kutoka Efraimu na kutoka Manase.”  Watu wa Gileadi wakateka vivuko vya Yordani+ ili kuwazuia Waefraimu wasivuke; na Waefraimu waliokuwa wakikimbia waliposema: “Naomba nivuke”; watu wa Gileadi walimuuliza kila mmoja wao, “Wewe ni Mwefraimu?” Aliposema: “Hapana!”  walimwambia, “Tafadhali sema Shibolethi.” Lakini alisema, “Sibolethi,” kwa kuwa hangeweza kutamka neno hilo kwa usahihi. Kwa hiyo walimkamata na kumuua kwenye vivuko vya Yordani. Basi Waefraimu 42,000 wakauawa wakati huo.  Yeftha alikuwa mwamuzi wa Israeli kwa miaka sita, kisha Yeftha Mgileadi akafa na kuzikwa katika jiji lake kule Gileadi.  Baada yake, Ibzani kutoka Bethlehemu akawa mwamuzi wa Israeli.+  Alikuwa na watoto wa kiume 30 na wa kike 30. Akawaoza binti zake 30 nje ya ukoo wake, na akaleta wanawake 30 kutoka nje ya ukoo wake ili waolewe na watoto wake wa kiume. Alikuwa mwamuzi wa Israeli kwa miaka saba. 10  Kisha Ibzani akafa na kuzikwa Bethlehemu. 11  Na baada yake, Eloni Mzabuloni akawa mwamuzi wa Israeli kwa miaka kumi. 12  Kisha Eloni Mzabuloni akafa na kuzikwa Aiyaloni katika nchi ya Zabuloni. 13  Na baada yake, Abdoni mwana wa Hileli Mpirathoni akawa mwamuzi wa Israeli. 14  Alikuwa na wana 40 na wajukuu 30 waliopanda juu ya punda 70. Alikuwa mwamuzi wa Israeli kwa miaka minane. 15  Kisha Abdoni mwana wa Hileli Mpirathoni akafa na kuzikwa Pirathoni katika nchi ya Efraimu katika mlima wa Mwamaleki.+

Maelezo ya Chini

Au labda, “wakavuka kuelekea kaskazini.”
Au “Niliiweka nafsi yangu mikononi mwangu.”