Waamuzi 18:1-31

  • Watu wa kabila la Dani watafuta nchi (1-31)

    • Kuchukuliwa kwa sanamu za Mika na kuhani wake (14-20)

    • Jiji la Laishi lachukuliwa na kuitwa Dani (27-29)

    • Ibada ya sanamu katika jiji la Dani (30, 31)

18  Siku hizo hakukuwa na mfalme katika Israeli.+ Na siku hizo watu wa kabila la Dani+ walikuwa wakitafuta mahali pa kukaa, kwa sababu kufikia wakati huo hawakuwa wamepata urithi miongoni mwa makabila ya Israeli.+  Watu wa kabila la Dani wakawatuma wanaume watano mashujaa kutoka miongoni mwao, waliotoka Sora na Eshtaoli,+ ili waipeleleze nchi na kuichunguza. Wakawaambia, “Nendeni mkaichunguze nchi.” Walipofika kwenye eneo lenye milima la Efraimu, nyumbani kwa Mika,+ wakalala huko usiku huo.  Walipokaribia nyumba ya Mika, walimsikia* yule kijana na kutambua kwamba alikuwa Mlawi, basi wakaenda kumuuliza, “Ni nani aliyekuleta huku? Unafanya nini hapa? Ni kazi gani iliyokuleta hapa?”  Akawaeleza mambo ambayo Mika alimtendea na kuwaambia, “Ameniajiri ili niwe kuhani wake.”+  Ndipo wakamwambia, “Tafadhali, muulize Mungu ikiwa safari yetu itafanikiwa.”  Kuhani huyo akawaambia, “Nendeni kwa amani. Yehova yuko pamoja nanyi katika safari yenu.”  Basi wanaume hao watano wakaendelea na safari na kufika Laishi.+ Wakaona jinsi wakaaji wa huko walivyoishi kama Wasidoni bila kumtegemea yeyote. Walikuwa watu watulivu wasio na wasiwasi,+ na hakukuwa na mtawala yeyote aliyewakandamiza wala kuwasumbua. Waliishi mbali sana na Wasidoni, na hawakushughulika na watu wengine.  Wanaume hao waliporudi kwa ndugu zao huko Sora na Eshtaoli,+ ndugu zao wakawauliza, “Mambo yaliendaje?”  Wakajibu, “Twendeni tukapigane nao, kwa kuwa tumeona nchi yao ni nzuri sana. Kwa nini mnasitasita? Msikawie kwenda kumiliki nchi hiyo. 10  Mtakapofika, mtakuta watu wasio na wasiwasi,+ na nchi yao ni kubwa. Mungu amewapa ninyi nchi hiyo ambayo haipungukiwi na kitu chochote duniani.”+ 11  Basi wanaume 600 wa kabila la Dani wenye silaha wakatoka Sora na Eshtaoli.+ 12  Nao wakaenda na kupiga kambi karibu na Kiriath-yearimu+ kule Yuda. Ndiyo sababu eneo hilo lililo upande wa magharibi wa Kiriath-yearimu, linaitwa Mahane-dani*+ mpaka leo. 13  Wakatoka huko na kwenda kwenye eneo lenye milima la Efraimu, wakafika nyumbani kwa Mika.+ 14  Kisha wale wanaume watano waliokuwa wameenda kuipeleleza nchi ya Laishi+ wakawaambia hivi ndugu zao: “Je, mnajua kwamba nyumba hizi zina efodi,* terafimu,* sanamu ya kuchongwa, na sanamu ya chuma?*+ Fikirieni mtakalofanya.” 15  Basi wakaenda kwenye nyumba ya yule kijana Mlawi,+ nyumbani kwa Mika, ili kumjulia hali. 16  Wakati huo, wale wanaume 600 wa kabila la Dani+ wenye silaha, walikuwa wamesimama langoni. 17  Wale wanaume watano walioenda kuipeleleza nchi+ wakaingia ndani ili kuchukua ile sanamu ya kuchongwa, ile efodi,*+ zile terafimu,*+ na ile sanamu ya chuma.*+ (Yule kuhani+ alikuwa amesimama langoni pamoja na wale wanaume 600 wenye silaha.) 18  Nao wakaingia katika nyumba ya Mika wakachukua ile sanamu ya kuchongwa, ile efodi,* zile terafimu,* na ile sanamu ya chuma.* Kuhani huyo akawauliza, “Mnafanya nini?” 19  Lakini wakamwambia, “Nyamaza. Funika kinywa chako kwa mkono wako, tufuate ili uwe baba* na kuhani wetu. Je, ni bora kwako kuwa kuhani wa nyumba ya mtu mmoja+ au kuhani wa kabila na ukoo katika Israeli?”+ 20  Ndipo kuhani huyo akaridhika, akachukua ile efodi,* zile terafimu,* na ile sanamu ya kuchongwa,+ akaenda nao. 21  Basi wakaanza safari yao, huku wakitanguliwa na watoto, mifugo, na vitu vyao vyenye thamani. 22  Walipokuwa umbali fulani kutoka nyumbani kwa Mika, wanaume walioishi karibu na Mika walikusanyika pamoja, wakawafuatia na kuwafikia wale watu wa kabila la Dani. 23  Walipowapigia kelele watu wa kabila la Dani, waligeuka na kumuuliza Mika, “Una shida gani? Kwa nini umekuja na umati huu?” 24  Basi akasema, “Mmechukua miungu niliyojitengenezea na kuondoka na kuhani wangu pia. Mkaniacha bila chochote. Mnawezaje kuniuliza, ‘Una shida gani?’” 25  Ndipo wale wanaume wa kabila la Dani wakamwambia, “Usitufokee; la sivyo, wanaume hawa wenye hasira watakushambulia na kukuua wewe na watu wa nyumbani mwako.” 26  Basi watu wa kabila la Dani wakaendelea na safari, na Mika alipoona kwamba wamemzidi nguvu, akageuka na kurudi nyumbani kwake. 27  Baada ya kuchukua miungu ya Mika, pamoja na kuhani wake, wakaenda kuwashambulia watu watulivu na wasio na wasiwasi+ wa Laishi.+ Wakawaua kwa upanga na kuteketeza jiji lao. 28  Hawakuwa na mtu wa kuwaokoa, kwa sababu waliishi mbali sana na Wasidoni katika bonde* la Beth-rehobu,+ nao hawakushughulika na watu wengine. Watu wa kabila la Dani wakalijenga upya jiji hilo na kuishi humo. 29  Wakaliita jiji hilo Dani+ sawa na jina la baba yao, Dani, mtoto wa Israeli.+ Lakini mwanzoni jiji hilo liliitwa Laishi.+ 30  Kisha watu wa kabila la Dani wakaanza kuabudu ile sanamu ya kuchongwa,+ naye Yonathani+ mwana wa Gershomu,+ mwana wa Musa, na wanawe wakawa makuhani wa kabila la Dani mpaka wakaaji walipopelekwa uhamishoni. 31  Nao wakaisimamisha ile sanamu ya kuchongwa iliyotengenezwa na Mika, na sanamu hiyo ikaendelea kuwa huko sikuzote ambazo nyumba ya Mungu wa kweli ilikuwa Shilo.+

Maelezo ya Chini

Au “walitambua lafudhi ya.”
Maana yake “Kambi ya Dani.”
Au “kizibao cha kuhani.”
Au “miungu ya familia; sanamu.”
Au “sanamu ya kuyeyushwa.”
Au “sanamu ya kuyeyushwa.”
Au “miungu ya familia; sanamu.”
Au “kizibao cha kuhani.”
Au “kizibao cha kuhani.”
Au “miungu ya familia; sanamu.”
Au “sanamu ya kuyeyushwa.”
Au “mshauri.”
Au “miungu ya familia; sanamu.”
Au “kizibao cha kuhani.”
Au “nchi tambarare ya chini.”