Waamuzi 2:1-23

  • Onyo kutoka kwa malaika wa Yehova (1-5)

  • Kifo cha Yoshua (6-10)

  • Mungu atuma waamuzi kuwaokoa Waisraeli (11-23)

2  Kisha malaika wa Yehova+ akatoka Gilgali+ na kwenda Bokimu na kusema: “Niliwatoa Misri na kuwaleta katika nchi ambayo niliapa kwamba ningewapa mababu zenu.+ Pia nikasema, ‘Sitavunja kamwe agano langu pamoja nanyi.+  Nanyi msifanye agano na wakaaji wa nchi hii,+ bomoeni madhabahu zao.’+ Lakini hamkutii sauti yangu.+ Kwa nini hamkutii?  Ndiyo maana nilisema, ‘Sitawafukuza kutoka mbele yenu,+ nao watakuwa mtego kwenu,+ nanyi mtashawishiwa kuifuata miungu yao.’”+  Malaika wa Yehova alipowaambia Waisraeli wote maneno hayo, watu wakaanza kulia kwa sauti kubwa.  Kwa hiyo wakapaita mahali hapo Bokimu,* nao wakamtolea Yehova dhabihu hapo.  Yoshua alipowaruhusu watu waende zao, kila Mwisraeli alienda kwenye eneo lake la urithi ili kuimiliki nchi.+  Na watu wakaendelea kumtumikia Yehova sikuzote za Yoshua na sikuzote za wazee walioendelea kuishi baada ya Yoshua kufa ambao walikuwa wameona mambo yote makuu ambayo Yehova aliwatendea Waisraeli.+  Kisha Yoshua mwana wa Nuni, mtumishi wa Yehova, akafa akiwa na umri wa miaka 110.+  Basi wakamzika kwenye eneo lake la urithi kule Timnath-heresi+ katika eneo lenye milima la Efraimu, upande wa kaskazini wa Mlima Gaashi.+ 10  Na watu wote wa kizazi hicho wakafa na kuzikwa kama walivyozikwa mababu zao,* na kizazi kingine kikatokea ambacho hakikumjua Yehova wala mambo aliyowafanyia Waisraeli. 11  Na Waisraeli wakatenda maovu machoni pa Yehova, wakaabudu* Mabaali.+ 12  Basi wakamwacha Yehova, Mungu wa baba zao, aliyewatoa katika nchi ya Misri.+ Nao wakafuata miungu mingine, miungu ya watu waliowazunguka,+ wakaiinamia, na hivyo wakamkasirisha Yehova.+ 13  Wakamwacha Yehova na kuabudu Baali na sanamu za Ashtorethi.+ 14  Ndipo hasira ya Yehova ikawaka dhidi ya Waisraeli, akawatia mikononi mwa waporaji, nao wakapora mali zao.+ Akawatia* mikononi mwa maadui waliowazunguka+ wala hawakuweza tena kuwashinda maadui wao.+ 15  Popote walipoenda, mkono wa Yehova uliwapinga na kuwaletea msiba,+ kama Yehova alivyokuwa amesema na kama Yehova alivyokuwa amewaapia,+ nao wakateseka sana.+ 16  Basi Yehova alikuwa akiwapa waamuzi ambao waliwaokoa kutoka mikononi mwa waporaji.+ 17  Lakini walikataa kuwasikiliza hata waamuzi hao, nao walifanya ukahaba na miungu mingine na kuiinamia. Waliacha haraka njia ambayo mababu zao walifuata, ambao walitii amri za Yehova.+ Walikataa kutii. 18  Wakati wowote Yehova alipowapa waamuzi,+ Yehova alikuwa pamoja na mwamuzi huyo, akawaokoa kutoka mikononi mwa maadui wao sikuzote za mwamuzi huyo; kwa maana Yehova aliwahurumia*+ kwa sababu ya kilio chao cha uchungu kilichosababishwa na wale waliowakandamiza+ na wale waliowatesa. 19  Hata hivyo mwamuzi huyo alipokufa, walitenda tena mambo maovu zaidi kuliko baba zao kwa kuifuata miungu mingine, kuiabudu na kuiinamia.+ Hawakuacha mazoea yao na tabia yao ya ukaidi. 20  Mwishowe hasira ya Yehova ikawaka dhidi ya Waisraeli,+ akasema, “Kwa sababu taifa hili limevunja agano langu+ nililofanya na mababu zao, na halijanitii,+ 21  basi mimi sitafukuza kutoka mbele yao taifa hata moja ambalo Yoshua aliacha alipokufa.+ 22  Nitafanya hivyo ili kuwajaribu Waisraeli nione kama wataishika njia yangu mimi, Yehova,+ na kutembea katika njia hiyo kama baba zao walivyofanya.” 23  Kwa hiyo Yehova akaruhusu mataifa hayo yabaki. Hakuyafukuza haraka, wala hakuyatia mikononi mwa Yoshua.

Maelezo ya Chini

Maana yake “Wanaolia.”
Tnn., “wakakusanywa kwa mababu zao.” Huu ni msemo wa kishairi unaorejelea kifo.
Au “wakatumikia.”
Tnn., “Akawauza.”
Au “alighairi.”