Waamuzi 3:1-31

  • Yehova awajaribu Waisraeli (1-6)

  • Othnieli, mwamuzi wa kwanza (7-11)

  • Mwamuzi Ehudi amuua Mfalme Egloni aliyekuwa mnene (12-30)

  • Mwamuzi Shamgari (31)

3  Haya ndiyo mataifa ambayo Yehova aliyaruhusu yabaki ili yawajaribu Waisraeli wote ambao hawakuwa wamepigana vita vyovyote katika nchi ya Kanaani+  (kusudi vizazi vilivyofuata vya Waisraeli, yaani, wale ambao hawakuwa wameona vita wafunzwe vita):  watawala watano wa Wafilisti,+ Wakanaani wote, Wasidoni,+ na Wahivi+ waliokaa katika Mlima Lebanoni+ kutoka Mlima Baal-hermoni mpaka Lebo-hamathi.*+  Nao walitumiwa kuwajaribu Waisraeli ili kuona kama watatii amri ambazo Yehova aliwapa baba zao kupitia Musa.+  Kwa hiyo, Waisraeli waliishi miongoni mwa Wakanaani,+ Wahiti, Waamori, Waperizi, Wahivi, na Wayebusi.  Waisraeli walioa mabinti kutoka mataifa hayo, na kuruhusu mabinti wao waolewe na wana wao, nao wakaanza kuabudu miungu yao.+  Basi Waisraeli wakatenda maovu machoni pa Yehova, wakamsahau Yehova Mungu wao, na kuabudu Mabaali+ na miti mitakatifu.*+  Ndipo hasira ya Yehova ikawaka dhidi ya Waisraeli, naye akawatia* mikononi mwa Kushan-rishathaimu mfalme wa Mesopotamia.* Na Waisraeli wakamtumikia Kushan-rishathaimu kwa miaka minane.  Waisraeli walipomlilia Yehova awasaidie,+ Yehova aliwapa mwokozi ili awaokoe,+ Othnieli+ mwana wa Kenasi, ndugu mdogo wa Kalebu. 10  Roho ya Yehova ikamjia,+ akawa mwamuzi wa Israeli. Alipoenda vitani, Yehova alimtia Kushan-rishathaimu mfalme wa Mesopotamia* mikononi mwake, naye akamshinda Kushan-rishathaimu. 11  Baada ya hapo nchi ikawa na amani* kwa miaka 40. Kisha Othnieli mwana wa Kenasi akafa. 12  Waisraeli wakaanza tena kutenda maovu machoni pa Yehova.+ Basi Yehova akamruhusu Egloni mfalme wa Moabu+ awashinde Waisraeli, kwa sababu walitenda maovu machoni pa Yehova. 13  Isitoshe Egloni akawakusanya Waamoni+ na Waamaleki.+ Nao wakawashambulia Waisraeli na kuliteka jiji la mitende.+ 14  Na Waisraeli wakamtumikia Egloni mfalme wa Moabu kwa miaka 18.+ 15  Ndipo Waisraeli wakamlilia Yehova awasaidie.+ Basi Yehova akawapa mwokozi,+ Ehudi+ mwana wa Gera, Mbenjamini+ aliyetumia mkono wa kushoto.+ Baada ya muda Waisraeli wakamtuma Ehudi apeleke ushuru kwa Egloni mfalme wa Moabu. 16  Ehudi akatengeneza upanga wenye makali pande mbili uliokuwa na urefu wa mkono mmoja,* akaufunga kiunoni ndani ya vazi lake upande wa kulia. 17  Kisha akampelekea Egloni mfalme wa Moabu ushuru huo. Egloni alikuwa mnene sana. 18  Baada ya Ehudi kutoa ule ushuru, akaondoka pamoja na watu waliokuwa wameubeba. 19  Lakini walipofika kwenye sanamu za mawe* huko Gilgali,+ akarudi kwa mfalme na kumwambia: “Nina ujumbe wako wa siri, Ee mfalme.” Basi mfalme akasema, “Ondokeni!” Ndipo watumishi wake wote wakaondoka. 20  Naye Ehudi akamkaribia alipokuwa ameketi peke yake darini katika chumba chake chenye baridi. Kisha Ehudi akasema, “Nina ujumbe wako kutoka kwa Mungu.” Kwa hiyo akasimama kutoka katika kiti chake cha ufalme. 21  Ndipo Ehudi akauchomoa upanga kwa mkono wake wa kushoto kutoka upande wa kulia wa kiuno chake na kumchoma mfalme tumboni. 22  Upanga ukazama tumboni mwake pamoja na mpini wake, na mafuta yakaufunika upanga huo kwa sababu hakuuchomoa, na kinyesi kikatoka. 23  Naye Ehudi akatoka nje kupitia barazani,* akafunga kwa ufunguo milango ya chumba cha darini. 24  Baada ya Ehudi kuondoka, watumishi wa mfalme walirudi na kuona milango ya chumba cha darini ikiwa imefungwa kwa ufunguo. Kwa hiyo wakasema, “Labda ameenda msalani katika chumba chake cha ndani.” 25  Waliendelea kungoja kwa muda mrefu mpaka wakaaibika, lakini walipoona kwamba hafungui milango ya chumba cha darini, wakachukua ufunguo na kuifungua, wakamwona bwana wao ameanguka sakafuni akiwa amekufa! 26  Ehudi akatoroka walipokuwa wanangoja, naye akapita karibu na sanamu za mawe,*+ akafika salama salimini kule Seira. 27  Alipofika huko, akapiga pembe*+ katika eneo lenye milima la Efraimu;+ na Waisraeli wakashuka pamoja naye kutoka milimani, yeye akiwa mbele yao. 28  Ndipo akawaambia, “Nifuateni, kwa sababu Yehova amewatia maadui wenu, Wamoabu, mikononi mwenu.” Nao wakamfuata, wakateka vivuko vya Yordani ili kuwazuia Wamoabu wasikimbie, na hawakumruhusu mtu yeyote avuke. 29  Wakati huo waliwaua Wamoabu wapatao 10,000,+ na wote walikuwa wanaume wenye nguvu na mashujaa; hakuna hata mmoja wao aliyeponyoka.+ 30  Basi siku hiyo Waisraeli wakawashinda Wamoabu; na nchi ikawa na amani* kwa miaka 80.+ 31  Baada ya Ehudi, akaja Shamgari+ mwana wa Anathi, aliyewaua wanaume 600 Wafilisti+ kwa mchokoo wa ng’ombe;+ yeye pia aliwaokoa Waisraeli.

Maelezo ya Chini

Au “njia ya kuingia Hamathi.”
Angalia Kamusi.
Tnn., “akawauza.”
Tnn., “Aram-naharaimu.”
Tnn., “Aramu.”
Tnn., “ikapumzika.”
Huenda ni mkono mfupi wenye urefu wa sentimita 38 hivi (inchi 15). Angalia Nyongeza B14.
Au labda, “machimbo ya mawe.”
Au labda, “sehemu ya kuingizia hewa.”
Au labda, “kwenye machimbo.”
Au “tarumbeta.”
Tnn., “ikapumzika.”