Kwa Waebrania 11:1-40

  • Maana ya imani (1, 2)

  • Mifano ya imani (3-40)

    • Haiwezekani kumpendeza Mungu bila imani (6)

11  Imani ni tarajio lililohakikishwa la mambo yanayotumainiwa,+ uthibitisho ulio wazi* wa mambo halisi ambayo hayaonekani.  Kwa maana kupitia imani, watu wa nyakati za kale* walitolewa ushahidi.  Kwa imani tunatambua kwamba mifumo ya mambo* ilipangwa kwa utaratibu kwa neno la Mungu, hivi kwamba kile kinachoonekana, kimekuwapo kutokana na vitu visivyoonekana.  Kwa imani, Abeli alimtolea Mungu dhabihu ya thamani kubwa zaidi kuliko ile ya Kaini,+ na kupitia imani hiyo alitolewa ushahidi kwamba alikuwa mwadilifu, kwa kuwa Mungu alikubali* zawadi zake,+ na ingawa alikufa, bado anazungumza+ kupitia imani yake.  Kwa imani, Enoko+ alihamishwa ili asione kifo, naye hakupatikana popote kwa sababu Mungu alikuwa amemhamisha;+ kwa maana kabla ya kuhamishwa alikuwa ametolewa ushahidi kwamba amempendeza Mungu vema.  Isitoshe, bila imani haiwezekani kumpendeza Mungu vema, kwa maana yule anayemkaribia Mungu lazima aamini kuwa yuko* na kwamba yeye huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.+  Kwa imani, Noa+ baada ya kuonywa na Mungu kuhusu mambo ambayo bado hayakuwa yameonekana,+ alimtii Mungu* kwa kujenga safina+ kwa ajili ya kuiokoa nyumba yake; na kupitia imani hiyo aliuhukumu ulimwengu,+ naye akawa mrithi wa uadilifu unaotokana na imani.  Kwa imani, Abrahamu+ alipoitwa alitii kwa kutoka na kwenda mahali ambapo angepokea kuwa urithi; aliondoka, ingawa hakujua mahali alipokuwa akienda.+  Kwa imani aliishi akiwa mgeni katika nchi ya ahadi kama katika nchi ya kigeni,+ akiishi kwenye mahema+ pamoja na Isaka na Yakobo, warithi pamoja naye wa ahadi ileile.+ 10  Kwa maana alikuwa akingojea jiji lililo na misingi ya kweli, ambalo mbuni* na mjenzi wake ni Mungu.+ 11  Kwa imani, Sara pia alipokea nguvu za kupata uzao,* ingawa alikuwa amepita umri,+ kwa kuwa alimwona kuwa mwaminifu* Yule aliyekuwa ameahidi. 12  Kwa sababu hiyo, kutoka kwa mwanamume mmoja, ambaye alikuwa kama mfu,+ walizaliwa watoto+ wengi kama nyota za mbinguni na wasiohesabika kama mchanga ulio kando ya bahari.+ 13  Katika imani hawa wote walikufa, ingawa hawakupokea utimizo wa zile ahadi;+ bali waliziona kwa mbali+ na kuzikaribisha na kutangaza hadharani kwamba walikuwa wageni na wakaaji wa muda katika nchi.⁠ 14  Kwa maana wale wanaozungumza hivyo wanathibitisha kwamba wanatafuta kwa bidii mahali pao wenyewe. 15  Na bado, kama wangeendelea kukumbuka mahali walipokuwa wametoka,+ wangepata nafasi ya kurudi. 16  Lakini sasa wanajitahidi kufikia mahali bora zaidi, yaani, panapohusiana na mbinguni. Kwa hiyo, Mungu haoni aibu kuwahusu, anapoitwa Mungu wao,+ kwa maana ametayarisha jiji kwa ajili yao.+ 17  Kwa imani, Abrahamu alipojaribiwa,+ ni kana kwamba alimtoa Isaka—mtu huyo aliyekuwa amezipokea ahadi kwa furaha alijaribu kumtoa mwana wake mzaliwa-pekee+ 18  ingawa alikuwa ameambiwa: “Ule utakaoitwa uzao* wako utapitia kwa Isaka.”+ 19  Lakini alifikia uamuzi kwamba Mungu angeweza kumfufua hata kutoka kwa wafu, naye alimpokea kutoka huko kwa njia ya mfano.+ 20  Kwa imani pia, Isaka alimbariki Yakobo+ na Esau+ kuhusu mambo yatakayokuja. 21  Kwa imani, Yakobo alipokuwa karibu kufa,+ aliwabariki wana wawili wa Yosefu+ na akaabudu huku akiegemea juu ya fimbo yake.+ 22  Kwa imani, Yosefu akikaribia mwisho wake, alizungumza kuhusu kutoka* kwa wana wa Israeli, naye akawapa maagizo* kuhusu mifupa* yake.+ 23  Kwa imani, Musa alifichwa kwa miezi mitatu na wazazi wake baada ya kuzaliwa,+ kwa sababu waliona kwamba huyo mtoto mchanga alikuwa mwenye kupendeza+ nao hawakuliogopa agizo la mfalme.+ 24  Kwa imani, Musa alipokuwa mtu mzima,+ alikataa kuitwa mwana wa binti ya Farao,+ 25  akachagua kuteswa pamoja na watu wa Mungu badala ya kufurahia dhambi kwa muda, 26  kwa sababu aliona shutuma ya Kristo kuwa utajiri mkubwa kuliko hazina za Misri, kwa maana alikaza macho kwenye malipo ya thawabu. 27  Kwa imani aliondoka Misri,+ lakini hakuogopa hasira ya mfalme,+ kwa maana aliendelea kuwa imara kama mtu anayemwona Yule asiyeonekana.+ 28  Kwa imani alifanya sherehe ya Pasaka na kupaka damu, ili mwangamizaji asiwadhuru* wazaliwa wao wa kwanza.+ 29  Kwa imani walipita katika Bahari Nyekundu kama kwenye nchi kavu,+ lakini Wamisri walipojaribu kupita wakamezwa.+ 30  Kwa imani kuta za Yeriko zilianguka baada ya watu kuzizunguka kwa siku saba.+ 31  Kwa imani, Rahabu yule kahaba hakuangamia pamoja na wale waliokosa kutii, kwa sababu aliwapokea wale wapelelezi kwa amani.+ 32  Nami nitasema nini zaidi? Kwa maana nitakosa wakati nikiendelea kusimulia kuhusu Gideoni,+ Baraka,+ Samsoni,+ Yeftha,+ Daudi,+ na vilevile Samweli+ na wale manabii wengine. 33  Kupitia imani walishinda falme,+ wakaleta uadilifu, wakapata ahadi,+ wakaziba vinywa vya simba,+ 34  wakazima nguvu za moto,+ wakaponyoka makali ya upanga,+ wakafanywa kuwa wenye nguvu kutoka kwenye hali ya udhaifu,+ wakawa mashujaa katika vita,+ wakayashinda kabisa majeshi ya wavamizi.+ 35  Wanawake waliwapokea wafu wao kupitia ufufuo,+ lakini watu wengine waliteswa kwa sababu hawakukubali kuachiliwa kupitia fidia fulani, ili waupate ufufuo ulio bora. 36  Ndiyo, wengine walipata jaribu lao kwa kudhihakiwa na kupigwa kwa mijeledi, naam, isitoshe, kwa kufungwa minyororo+ na magerezani.+ 37  Walipigwa mawe,+ walijaribiwa, walikatwa vipande viwili* kwa msumeno, walichinjwa kwa upanga,+ walitembea huku na huku wakiwa wamevaa ngozi za kondoo na ngozi za mbuzi,+ wakiwa katika uhitaji, katika dhiki,+ wakiteswa;+ 38  na ulimwengu haukuwafaa. Walitembea huku na huku katika majangwa na milima na mapango+ na mashimo ya dunia. 39  Na bado hawa wote, ingawa walitolewa ushahidi unaofaa kwa sababu ya imani yao, hawakupata utimizo wa ile ahadi, 40  kwa sababu Mungu aliona mapema kitu bora kwa ajili yetu,+ ili wasifanywe kuwa wakamilifu bila sisi.

Maelezo ya Chini

Au “uthibitisho wenye kuridhisha.”
Au “mababu zetu.”
Au “vizazi.” Angalia Kamusi.
Au “alitoa ushahidi kwa kukubali.”
Au “yuko hai.”
Au “alimwogopa Mungu.”
Au “msanifu.”
Tnn., “mbegu.”
Au “anayetegemeka.”
Tnn., “mbegu.”
Au “mazishi.”
Yaani, kutoka katika nchi ya Misri.
Au “amri.”
Tnn., “asiwaguse.”
Au “vipandevipande.”