Kwa Waebrania 12:1-29

  • Yesu, Mkamilishaji wa imani yetu (1-3)

    • Wingu kubwa la mashahidi (1)

  • Usiipuuze nidhamu ya Yehova (4-11)

  • Fanyia miguu yako mapito yaliyonyooka (12-17)

  • Kukaribia Yerusalemu la mbinguni (18-29)

12  Hivyo basi, kwa kuwa tuna wingu kubwa hivyo la mashahidi linalotuzunguka, acheni sisi pia tuondoe kila uzito na dhambi inayotutatanisha kwa urahisi,+ na tukimbie kwa uvumilivu shindano la mbio lililowekwa mbele yetu,+  huku tukimtazama kwa makini Wakili Mkuu na Mkamilishaji wa imani yetu, Yesu.+ Kwa sababu ya shangwe iliyowekwa mbele yake, alivumilia mti wa mateso,* akaidharau aibu, naye ameketi kwenye mkono wa kuume wa kiti cha ufalme cha Mungu.+  Kwa kweli, mfikirieni sana yule ambaye amevumilia maneno makali kama hayo kutoka kwa watenda dhambi+ kinyume cha faida zao wenyewe, ili msichoke na kukata tamaa.*+  Katika pambano lenu na dhambi, hamjapambana kamwe kufikia hatua ya kumwaga damu.  Nanyi mmesahau kabisa lile himizo linalosema nanyi kama wana: “Mwanangu, usiipuuze nidhamu kutoka kwa Yehova,* wala usikate tamaa anapokurekebisha;  kwa maana Yehova* huwatia nidhamu wale anaowapenda, kwa kweli, humpiga fimbo* kila mtu ambaye amempokea kuwa mwana.”+  Mnahitaji kuvumilia kama sehemu ya nidhamu* yenu. Mungu anawatendea ninyi kama wana.+ Kwa maana ni mwana gani ambaye hatiwi nidhamu na baba yake?+  Lakini ikiwa ninyi nyote hamjashiriki katika kupokea nidhamu hii, kwa kweli ninyi ni watoto haramu, bali si wana.  Zaidi ya hayo, baba zetu wa kibinadamu* walikuwa wakitutia nidhamu, nasi tuliwapa heshima. Je, hatupaswi kujitiisha hata zaidi kwa Baba wa maisha yetu ya kiroho na kuishi?+ 10  Kwa maana walitutia nidhamu kwa muda mfupi kulingana na jinsi walivyoona kuwa inafaa, lakini yeye hufanya hivyo kwa faida yetu ili tuushiriki utakatifu wake.+ 11  Ni kweli, hakuna nidhamu inayoonekana kwa sasa kuwa yenye shangwe, bali inaumiza;* lakini baadaye hutokeza amani na uadilifu* kwa wale ambao wamezoezwa nayo. 12  Kwa hiyo, imarisheni mikono inayolegea na magoti yaliyo dhaifu,+ 13  nanyi endeleeni kuifanyia miguu yenu mapito yaliyonyooka,+ ili kile ambacho ni kilemavu kisiteguke, badala yake, kiponywe. 14  Fuatilieni amani pamoja na watu wote+ na utakaso*+ ambao bila huo hakuna mtu atakayemwona Bwana. 15  Iweni waangalifu kwamba yeyote asikose kupata fadhili zisizostahiliwa za Mungu, ili mzizi wowote wenye sumu usichipuke na kusababisha taabu na wengi watiwe unajisi nao;+ 16  na muwe waangalifu ili miongoni mwenu kusiwe na mwasherati* wala yeyote asiyethamini mambo matakatifu, kama Esau, aliyetoa haki zake za kuwa mzaliwa wa kwanza kwa kubadilishana na mlo mmoja.+ 17  Kwa kuwa mnajua kwamba baadaye alipotaka kuirithi baraka, alikataliwa; kwa maana, ingawa alijaribu kwa bidii kubadili fikira* kwa machozi,+ hakufaulu.* 18  Kwa maana hamkukaribia kitu kinachoweza kuguswa+ na ambacho kimewashwa moto,+ na wingu jeusi na giza zito na dhoruba,+ 19  na mlio wa tarumbeta+ na sauti ya maneno yanayosemwa,+ ambayo watu walipoisikia waliomba kwamba wasiambiwe neno lingine lolote.+ 20  Kwa maana hawakuweza kuivumilia amri hii: “Hata mnyama akiugusa mlima, lazima apigwe mawe.”+ 21  Pia, wonyesho huo ulikuwa wa kutisha sana hivi kwamba Musa akasema: “Ninaogopa na kutetemeka.”+ 22  Lakini ninyi mmeukaribia Mlima Sayuni,+ jiji la Mungu aliye hai, yaani, Yerusalemu la mbinguni,+ na makumi ya maelfu ya malaika 23  katika kusanyiko kuu,+ na kutaniko la wazaliwa wa kwanza ambao wameandikishwa mbinguni, na Mungu Mwamuzi wa wote,+ na maisha ya kiroho+ ya waadilifu ambao wamefanywa wakamilifu,+ 24  na Yesu mpatanishi+ wa agano jipya,+ na damu iliyonyunyizwa, ambayo husema kwa njia bora kuliko damu ya Abeli.+ 25  Angalieni kwamba msikatae kumsikiliza* yule anayezungumza. Kwa maana ikiwa wale waliokataa kumsikiliza yule aliyetoa onyo kutoka kwa Mungu duniani hawakuponyoka, je, kweli sisi tutaponyoka ikiwa tutamwacha yule anayezungumza kutoka mbinguni?+ 26  Wakati huo sauti yake iliitikisa dunia,+ lakini sasa ameahidi: “Nitatikisa kwa mara nyingine tena, si dunia tu bali pia mbingu.”+ 27  Sasa maneno “kwa mara nyingine tena” yanaonyesha kuondolewa kwa vitu vinavyotikiswa, vitu vilivyotengenezwa, ili vitu ambavyo havitikiswi vibaki. 28  Kwa hiyo, kwa kuwa tutapokea Ufalme usioweza kutikiswa, acheni tuendelee kupokea fadhili zisizostahiliwa, ambazo zitatuwezesha kumtolea Mungu utumishi mtakatifu kwa njia inayokubalika, kwa kumwogopa Mungu na kumheshimu. 29  Kwa maana Mungu wetu ni moto unaoteketeza.+

Maelezo ya Chini

Angalia Kamusi.
Au “msizimie katika nafsi zenu.”
Au “humwadhibu.”
Au “mazoezi.”
Tnn., “baba zetu wa mwili.”
Au “inahuzunisha.”
Tnn., “huzaa tunda lenye kufanya amani la uadilifu.”
Au “utakatifu.”
Angalia Kamusi, “Uasherati.”
Yaani, fikira za baba yake.
Tnn., “hakupata nafasi kwa ajili ya hilo.”
Au “msimpe visingizio: msimpuuze.”