Kwa Waebrania 6:1-20

  • Kusonga mbele kuelekea ukomavu (1-3)

  • Wale wanaoanguka wanamtundika tena Mwana kwenye mti (4-8)

  • Fanyeni tumaini lenu kuwa hakika (9-12)

  • Uhakika wa ahadi ya Mungu (13-20)

    • Ahadi na kiapo cha Mungu havibadiliki (17, 18)

6  Kwa hiyo, kwa kuwa sasa tumeliacha nyuma fundisho la msingi+ kumhusu Kristo, na tusonge mbele kuelekea ukomavu,+ tusiweke msingi tena, yaani, kutubu matendo yaliyokufa na imani katika Mungu,  fundisho kuhusu aina mbalimbali za ubatizo na kuweka mikono,+ kufufuliwa kwa wafu+ na hukumu ya milele.  Na tutafanya hivyo ikiwa kwa kweli Mungu ataruhusu.  Kwa maana kuhusu wale ambao wakati fulani walikuwa kwenye nuru,+ na ambao wameonja zawadi ya bure ya kimbingu na ambao wamekuwa washiriki wa roho takatifu  na ambao wameonja neno zuri la Mungu na nguvu za mfumo wa mambo* unaokuja,  lakini wameanguka,+ haiwezekani kuwarudisha tena kwenye toba, kwa sababu wanamtundika tena mtini Mwana wa Mungu kwa ajili yao wenyewe na kumwaibisha hadharani.+  Kwa maana udongo hupokea baraka kutoka kwa Mungu unapokunywa mvua inayonyesha juu yake mara kwa mara, na kisha huzaa mimea inayowanufaisha wale wanaoulima.  Lakini ukizaa miiba na michongoma, hukataliwa na huwa karibu kulaaniwa, na mwishowe huchomwa.  Lakini wapendwa, ingawa tunazungumza hivyo, tuna hakika mna hali bora, yaani, hali inayohusiana na wokovu. 10  Kwa maana Mungu hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake,+ kwa kuhudumu na kuendelea kuwahudumia watakatifu. 11  Lakini tunatamani kila mmoja wenu awe na bidii ileile ili kuwa na uhakikisho kamili wa tumaini+ mpaka mwisho,+ 12  ili msiwe goigoi,+ bali muwe waigaji wa wale ambao kupitia imani na subira huzirithi ahadi. 13  Kwa maana Mungu alipotoa ahadi yake kwa Abrahamu, kwa kuwa hangeweza kuapa kwa yeyote aliye mkubwa zaidi, aliapa kwa jina lake mwenyewe,+ 14  akisema: “Hakika nitakubariki nami hakika nitaufanya uzao wako uwe mwingi.”+ 15  Basi, baada ya Abrahamu kuonyesha subira, aliipata ahadi hiyo. 16  Kwa maana watu huapa kwa mtu aliye mkubwa zaidi yao, na kiapo chao ndicho mwisho wa kila bishano, kwa kuwa ndicho uhakikisho wao wa kisheria.+ 17  Vivyo hivyo, Mungu alipoamua kuwaonyesha waziwazi warithi wa ile ahadi+ jinsi kusudi* lake lisivyobadilika, alitoa uhakikisho* kwa kiapo, 18  ili kupitia mambo mawili yasiyobadilika ambayo kuhusiana nayo Mungu hawezi kamwe kusema uwongo,+ sisi ambao tumekimbia kwenda katika kimbilio tutiwe moyo kabisa ili tushike imara tumaini lililowekwa mbele yetu. 19  Tuna tumaini hilo+ kama nanga ya nafsi,* likiwa hakika na imara, nalo huingia ndani ya pazia,+ 20  ambamo mtangulizi ameingia kwa ajili yetu, Yesu,+ ambaye amekuwa kuhani mkuu milele kama Melkizedeki.+

Maelezo ya Chini

Angalia Kamusi.
Au “shauri.”
Au “aliingilia kati.” Tnn., “alifanya upatanisho.”
Au “ya uhai wetu.”