Kwa Waebrania 7:1-28

  • Melkizedeki, mfalme na kuhani wa pekee (1-10)

  • Ubora wa ukuhani wa Kristo (11-28)

    • Kristo anaweza kuokoa kikamili (25)

7  Kwa maana huyu Melkizedeki, mfalme wa Salemu, kuhani wa Mungu Aliye Juu Zaidi, alikutana na Abrahamu akirudi baada ya kuwaangamiza wafalme kisha akambariki,+  naye Abrahamu akampa* sehemu ya kumi ya vitu vyote. Kwanza, jina lake linatafsiriwa “Mfalme wa Uadilifu,” kisha pia mfalme wa Salemu, yaani, “Mfalme wa Amani.”  Hana baba wala mama, hana ukoo, na hana mwanzo wa siku wala mwisho wa uzima, bali akiwa amefanywa kama Mwana wa Mungu, anadumu akiwa kuhani daima.*+  Oneni jinsi mtu huyu alivyokuwa mkuu, ambaye Abrahamu yule kichwa cha familia,* alimpa sehemu ya kumi kutoka kwa zile nyara bora.+  Ni kweli, kulingana na Sheria, wazao wa Lawi+ ambao hupokea cheo chao cha ukuhani, wana amri ya kukusanya sehemu za kumi kutoka kwa watu,+ yaani, kutoka kwa ndugu zao, ingawa hao ni wazao wa* Abrahamu.  Lakini mtu huyu ambaye ukoo wake haukutokana nao, alichukua sehemu za kumi kutoka kwa Abrahamu na kumbariki yule aliyekuwa na zile ahadi.+  Basi hakuna shaka kwamba mdogo hubarikiwa na mkubwa.  Na kwa upande mmoja, watu wanaokufa ndio wanaopokea sehemu za kumi, lakini kwa upande mwingine, ni mtu ambaye ushahidi unatolewa kwamba anaishi.+  Na inaweza kusemwa kwamba hata Lawi, ambaye hupokea sehemu za kumi, amelipa sehemu za kumi kupitia Abrahamu, 10  kwa maana bado alikuwa mzao wa wakati ujao wa* babu yake wakati Melkizedeki alipokutana naye.+ 11  Basi, ikiwa ukamilifu ungeweza kupatikana kupitia ukuhani wa Walawi+ (kwa maana ulikuwa sehemu ya Sheria ambayo watu walipewa), kungekuwa na umuhimu gani wa kuhani mwingine kusimama anayesemwa kuwa kwa mfano wa Melkizedeki+ na si kwa mfano wa Haruni? 12  Kwa kuwa ukuhani unabadilishwa, inakuwa muhimu kubadilisha Sheria pia.+ 13  Kwa maana mtu ambaye mambo haya yanasemwa kumhusu alitoka katika kabila lingine, na hakuna mtu wa kabila hilo ambaye amewahi kuhudumu kwenye madhabahu.+ 14  Kwa kuwa ni wazi kwamba Bwana wetu ametokana na Yuda,+ naye Musa hakusema kwamba makuhani wangetoka katika kabila hilo. 15  Na hilo linakuwa wazi hata zaidi kuhani mwingine+ anaposimama ambaye ni kama Melkizedeki,+ 16  ambaye amekuwa hivyo, si kupitia matakwa ya kisheria yanayotegemea uzao wa kimwili, bali kupitia nguvu za uzima usioweza kuharibika.+ 17  Kwa maana imesemwa katika ushahidi kumhusu: “Wewe ni kuhani milele kwa mfano wa Melkizedeki.”+ 18  Basi, ile amri ya zamani inawekwa kando kwa sababu ni dhaifu na haifai.+ 19  Kwa maana Sheria haikufanya kitu chochote kiwe kikamilifu,+ lakini kuletwa kwa tumaini bora+ kulifanya hivyo, na kupitia tumaini hilo tunamkaribia Mungu.+ 20  Pia, kwa kuwa jambo hilo halikufanywa bila kiapo rasmi 21  (kwa kweli, kuna watu ambao wamekuwa makuhani bila kiapo rasmi, lakini huyu amekuwa kuhani kupitia kiapo kilichotolewa kumhusu na Yule aliyesema hivi: “Yehova* ameapa naye hatabadili nia yake,* ‘Wewe ni kuhani milele’”),+ 22  kwa hiyo Yesu amekuwa uhakikisho* wa agano bora.+ 23  Zaidi ya hayo, wengi walikuwa makuhani mmoja baada ya mwingine+ kwa sababu kifo kiliwazuia wasiendelee kuwa makuhani, 24  lakini kwa sababu yeye anaendelea kuishi milele,+ hakuna anayerithi ukuhani wake. 25  Basi anaweza pia kuwaokoa kikamili wale wanaomkaribia Mungu kupitia yeye, kwa sababu sikuzote yuko hai ili kuwaombea.+ 26  Kwa maana inafaa tuwe na kuhani mkuu kama huyo ambaye ni mshikamanifu, asiye na hatia, asiye na unajisi,+ aliyetenganishwa na watenda dhambi, na aliyeinuliwa juu ya mbingu.+ 27  Tofauti na makuhani hao wakuu, hahitaji kutoa dhabihu kila siku,+ kwanza kwa ajili ya dhambi zake mwenyewe kisha kwa ajili ya dhambi za watu,+ kwa sababu alifanya hivyo mara moja kwa wakati wote alipojitoa mwenyewe.+ 28  Kwa maana Sheria huweka rasmi watu walio na udhaifu wawe makuhani wakuu,+ lakini neno la kiapo+ rasmi baada ya Sheria humweka rasmi Mwana, ambaye amefanywa kuwa mkamilifu+ milele.

Maelezo ya Chini

Tnn., “akamgawia.”
Au “kwa wakati wote.”
Au “mzee wa ukoo.”
Tnn., “wametoka katika kiuno cha.”
Tnn., “katika kiuno cha.”
Au “hataghairi.”
Au “yule aliyewekwa kuwa rehani.”