Kwa Wagalatia 3:1-29

  • Tofauti kati ya matendo ya Sheria na imani (1-14)

    • Mwadilifu ataishi kupitia imani (11)

  • Ahadi kwa Abrahamu haikuwa kupitia Sheria (15-18)

    • Kristo, uzao wa Abrahamu (16)

  • Chanzo na kusudi la Sheria (19-25)

  • Wana wa Mungu kupitia imani (26-29)

    • Wazao wa Abrahamu, wale walio wa Kristo (29)

3  Enyi Wagalatia wasio na akili! Ni nani aliyewaleta chini ya uvutano huu mwovu,+ ninyi mliofafanuliwa waziwazi jinsi Yesu Kristo alivyotundikwa mtini?+  Ninataka kuwauliza* jambo hili moja: Je, mlipokea roho kupitia matendo ya sheria au kwa sababu ya kuamini mambo mliyosikia?+  Je, ninyi hamna akili kabisa? Baada ya kuanza mwendo wa kiroho,* je, mnamalizia katika mwendo wa kimwili?*+  Je, mlipatwa na mateso mengi sana bila sababu? Ikiwa kwa kweli ilikuwa bila sababu.  Kwa hiyo, je, yule anayewapa ninyi roho na kufanya matendo yenye nguvu+ kati yenu, anayafanya kwa sababu ya matendo ya sheria au kwa sababu mnaamini mambo mliyosikia?  Kama vile Abrahamu “alivyokuwa na imani katika Yehova,* na ikahesabiwa kwake kuwa ni uadilifu.”+  Bila shaka mnajua kwamba wale wanaoshikamana na imani ni wana wa Abrahamu.+  Kwa hiyo, andiko likitangulia kuona kwamba Mungu atawatangaza watu wa mataifa kuwa waadilifu kupitia imani, lilitangaza habari njema mwanzoni kwa Abrahamu, yaani: “Kupitia kwako mataifa yote yatabarikiwa.”+  Basi wale wanaoshikamana na imani wanabarikiwa pamoja na Abrahamu, aliyekuwa na imani.+ 10  Wote wanaotegemea matendo ya sheria wako chini ya laana, kwa maana imeandikwa: “Amelaaniwa kila mtu asiyedumu katika mambo yote yaliyoandikwa katika kitabu cha kukunjwa cha Sheria kwa kuyatenda.”+ 11  Isitoshe, ni wazi kwamba kupitia sheria hakuna mtu atakayetangazwa kuwa mwadilifu mbele za Mungu,+ kwa maana “mwadilifu ataishi kupitia imani.”+ 12  Sasa Sheria haitegemei imani. Badala yake, “yeyote anayefanya mambo hayo ataishi kupitia mambo hayo.”+ 13  Kristo alitununua,+ akatuweka huru+ kutoka katika laana ya Sheria akawa laana badala yetu, kwa sababu imeandikwa: “Amelaaniwa kila mtu aliyetundikwa kwenye mti.”+ 14  Ilikuwa hivyo ili baraka ya Abrahamu ije kwa mataifa kupitia Kristo Yesu,+ ili tuipokee roho iliyoahidiwa+ kupitia imani yetu. 15  Akina ndugu, ninazungumza kwa kutumia mfano wa mwanadamu: Agano linapohalalishwa, hata kama ni kupitia mwanadamu, hakuna mtu anayelifuta au kuliongezea jambo lolote. 16  Sasa ahadi zilitolewa kwa Abrahamu na kwa uzao wake.*+ Haisemi, “na kwa wazao wako,”* kana kwamba ni wengi. Badala yake, inasema, “na kwa uzao wako,”* kana kwamba ni kwa mmoja, ambaye ni Kristo.+ 17  Isitoshe, ninasema hivi: Sheria iliyotokezwa miaka 430 baadaye,+ haivunji agano lililofanywa na Mungu mwanzoni, na haifuti ahadi. 18  Kwa maana ikiwa urithi unategemea sheria, hautegemei tena ahadi; lakini Mungu amempa Abrahamu urithi kwa fadhili kupitia ahadi.+ 19  Basi, kwa nini Sheria? Iliongezwa ili kufanya makosa yawe wazi,+ mpaka ufike ule uzao*+ ambao ulikuwa umepewa ahadi; na ilipitishwa kupitia malaika+ kwa mkono wa mpatanishi.+ 20  Sasa hakuna mpatanishi wakati mtu mmoja tu ndiye anayehusika, lakini Mungu ni mmoja tu. 21  Kwa hiyo, je, Sheria inapinga ahadi za Mungu? La hasha! Kwa maana ikiwa kungekuwa na sheria inayoweza kuleta uhai, kwa kweli uadilifu ungekuwa kupitia sheria. 22  Lakini Andiko liliyafunga mambo yote katika kifungo cha dhambi, ili ahadi inayotokana na imani katika Yesu Kristo ipewe wale wanaoamini.* 23  Hata hivyo, kabla ya imani kufika, tulikuwa tukilindwa chini ya sheria, tukiwekwa kifungoni, tukiitazamia imani iliyokusudiwa kufunuliwa.+ 24  Basi Sheria imekuwa mtunzaji* wetu ikituongoza kwa Kristo,+ ili tutangazwe kuwa waadilifu kupitia imani.+ 25  Lakini sasa kwa kuwa imani imefika,+ hatuko tena chini ya mtunzaji.*+ 26  Kwa kweli, ninyi nyote ni wana wa Mungu+ kupitia imani yenu katika Kristo Yesu.+ 27  Kwa maana ninyi nyote mliobatizwa katika Kristo mmemvaa Kristo.+ 28  Hakuna Myahudi wala Mgiriki,+ hakuna mtumwa wala mtu huru,+ hakuna mwanamume wala mwanamke,+ kwa maana ninyi nyote ni kitu kimoja katika muungano na Kristo Yesu.+ 29  Isitoshe, ikiwa ninyi ni wa Kristo, ninyi kwa kweli ni uzao wa* Abrahamu,+ warithi+ kuhusiana na ahadi.+

Maelezo ya Chini

Tnn., “kujifunza kutoka kwenu.”
Tnn., “kuanza katika roho.”
Tnn., “mnakamilishwa katika mwili.”
Tnn., “mbegu yako.”
Tnn., “mbegu zako.”
Tnn., “mbegu yake.”
Tnn., “ile mbegu.”
Au “wanaoonyesha imani.”
Au “mfundishaji; mlezi.”
Au “mfundishaji; mlezi.”
Tnn., “mbegu ya.”