Kwa Waroma 11:1-36

  • Israeli hawakukataliwa wote (1-16)

  • Mfano wa mzeituni (17-32)

  • Kina cha hekima ya Mungu (33-36)

11  Basi ninauliza, je, Mungu aliwakataa watu wake?+ La hasha! Kwa maana mimi pia ni Mwisraeli, wa uzao wa* Abrahamu, kutoka kabila la Benjamini.  Mungu hakuwakataa watu wake, aliowatambua kwanza.+ Je, hamjui andiko linavyosema kumhusu Eliya, anapomsihi Mungu dhidi ya Israeli?  “Yehova,* wamewaua manabii wako, wamezibomoa madhabahu zako, nami peke yangu nimebaki, na sasa wanajaribu kuniua.”*+  Lakini neno la Mungu linamwambia nini? “Nimeacha watu 7,000 kwa ajili yangu, watu ambao hawakumpigia goti Baali.”+  Basi, kwa njia hiyohiyo, wakati huu pia, kuna mabaki kulingana na kuchaguliwa+ kupitia fadhili zisizostahiliwa.  Basi ikiwa ni kupitia fadhili zisizostahiliwa,+ si kupitia matendo tena;+ la sivyo, fadhili zisizostahiliwa hazingekuwa tena fadhili zisizostahiliwa.  Tuseme nini, basi? Jambo lilelile ambalo Israeli anatafuta kwa bidii hakulipata, lakini wale waliochaguliwa walilipata.+ Hisia za wale wengine zilifanywa kuwa nzito,+  kama ilivyoandikwa: “Mungu amewapa roho ya usingizi mzito,+ macho yasiyoona na masikio yasiyosikia, mpaka leo hii.”+  Pia, Daudi anasema: “Meza yao na iwe kitu kinachonasa na mtego na kikwazo na malipo kwao. 10  Acha macho yao yatiwe giza wasiweze kuona, na sikuzote uwafanye wainamishe migongo yao.”+ 11  Basi ninauliza, Je, walijikwaa na kuanguka kabisa? La hasha! Lakini kwa kujikwaa kwao, kuna wokovu kwa watu wa mataifa, ili kuwachochea wawe na wivu.+ 12  Sasa ikiwa kujikwaa kwao humaanisha utajiri kwa ulimwengu, na kupungua kwao humaanisha utajiri kwa watu wa mataifa,+ je, idadi yao kamili haitamaanisha hivyo hata zaidi? 13  Sasa ninazungumza nanyi mlio watu wa mataifa. Kwa kuwa mimi ni mtume kwa mataifa,+ ninaitukuza* huduma yangu,+ 14  ili kuona ikiwa ninaweza kwa njia fulani kuwachochea watu wangu wawe* na wivu na kuwaokoa baadhi yao. 15  Kwa maana ikiwa kutupwa kwao+ humaanisha upatanisho kwa ulimwengu, kukubaliwa kwao kutamaanisha nini isipokuwa uzima kutoka kwa wafu? 16  Isitoshe, ikiwa sehemu ya donge inayochukuliwa iwe matunda ya kwanza ni takatifu, donge lote pia ni takatifu; na ikiwa mzizi ni mtakatifu, matawi pia yako hivyo. 17  Hata hivyo, ikiwa baadhi ya matawi yalikatwa, na ingawa wewe ni mzeituni wa mwituni, ulipandikizwa kati yake na kuwa mshiriki wa utajiri wa mzizi wa mzeituni, 18  usijivune* dhidi ya matawi. Kama ukijivuna* dhidi yake,+ kumbuka kwamba, si wewe unayebeba mzizi, bali ni mzizi unaokubeba wewe. 19  Basi, utasema: “Matawi yalikatwa ili mimi nipandikizwe.”+ 20  Hilo ni kweli! Walikatwa+ kwa sababu walikosa imani, lakini wewe umesimama kwa imani.+ Usiwe na majivuno, bali uwe na woga. 21  Kwa maana ikiwa Mungu hakuyaacha matawi ya asili, vivyo hivyo hatakuacha wewe. 22  Kwa hiyo, fikiria fadhili+ na ukali wa Mungu. Kuna ukali kuwaelekea wale walioanguka,+ lakini kukuelekea wewe kuna fadhili za Mungu mradi tu ukae katika fadhili zake; la sivyo, wewe pia utakatwa. 23  Wao pia, ikiwa hawataendelea kukosa imani, watapandikizwa,+ kwa kuwa Mungu anaweza kuwapandikiza tena. 24  Kwa maana ikiwa wewe ulikatwa kutoka kwenye mzeituni wa mwituni na kupandikizwa kinyume cha asili kwenye mzeituni wa bustani, je, hawa walio wa asili hawatapandikizwa tena kwenye mzeituni wao wenyewe? 25  Kwa maana sitaki ninyi, akina ndugu, mkose kuijua siri hii takatifu,+ ili msiwe wenye hekima machoni penu wenyewe: Hisia za Israeli zimetiwa uzito kwa kiasi fulani mpaka idadi kamili ya watu wa mataifa itakapoingia, 26  na kwa njia hii Israeli wote+ wataokolewa. Kama ilivyoandikwa: “Mkombozi* atakuja kutoka Sayuni+ na kuondoa mazoea ya kutomwogopa Mungu kutoka katika Yakobo. 27  Na hili ndilo agano langu pamoja nao,+ nitakapoondoa dhambi zao.”+ 28  Ni kweli, kuhusu habari njema wao ni adui kwa ajili yenu, lakini kuhusu uchaguzi wa Mungu wao ni wapendwa kwa ajili ya mababu zao.+ 29  Kwa kuwa Mungu hataghairi kwa sababu ya zawadi na mwito anaotoa. 30  Kwa maana kama vile ninyi wakati fulani mlivyokuwa watu wasiomtii Mungu+ lakini sasa mmeonyeshwa rehema+ kwa sababu ya kutotii kwao,+ 31  ndivyo pia hawa sasa wamekuwa wasiotii na hivyo mkaonyeshwa rehema, ili wao wenyewe pia waonyeshwe rehema sasa. 32  Kwa maana Mungu amewaweka wote pamoja katika kutotii,+ ili awaonyeshe wote rehema.+ 33  Lo! Jinsi kilivyo kina cha utajiri wa Mungu na hekima na ujuzi! Jinsi hukumu zake zisivyochunguzika na njia zake zisivyotafutika! 34  Kwa maana “ni nani ameijua akili ya Yehova,* au ni nani amekuwa mshauri wake?”+ 35  Au, “Ni nani amempa yeye kwanza, hivi kwamba iwe lazima arudishiwe?”+ 36  Kwa sababu vitu vyote vimetoka kwake, kupitia yeye na kwa ajili yake. Kwake yeye na kuwe na utukufu milele. Amina.

Maelezo ya Chini

Tnn., “mbegu ya.”
Au “kuchukua uhai (nafsi) wangu.”
Au “ninaisifu.”
Tnn., “mwili wangu uwe.”
Au “ukijigamba.”
Au “usijigambe.”
Au “Mwokozi.”