Kwa Waroma 16:1-27

  • Paulo amtambulisha Fibi, mhudumu (1, 2)

  • Salamu kwa Wakristo huko Roma (3-16)

  • Waonywa kuhusu migawanyiko (17-20)

  • Salamu kutoka kwa wafanyakazi wenzi wa Paulo (21-24)

  • Siri takatifu yafunuliwa (25-27)

16  Ninamtambulisha* kwenu Fibi dada yetu, ambaye ni mhudumu wa kutaniko lililo huko Kenkrea,+  ili mumkaribishe katika Bwana kwa njia inayowastahili watakatifu, na kumpa msaada wowote ambao huenda akahitaji,+ kwa maana yeye pia alikuwa mtetezi wa wengi, kutia ndani mimi mwenyewe.  Wapeni salamu zangu Priska na Akila,+ wafanyakazi wenzangu katika Kristo Yesu,  ambao wamehatarisha shingo zao kwa ajili yangu,*+ na si mimi tu ninayewashukuru bali pia makutaniko yote ya mataifa.  Pia salimuni kutaniko lililo katika nyumba yao.+ Msalimuni Epaineto mpendwa wangu, aliye matunda ya kwanza ya Asia kwa ajili ya Kristo.  Msalimuni Maria, ambaye amefanya kazi kwa bidii kwa ajili yenu.  Wasalimuni Androniko na Yunia, watu wangu wa ukoo+ na wafungwa wenzangu, ambao ni watu wanaojulikana kwa mitume na ambao wamekuwa katika muungano na Kristo muda mrefu zaidi yangu.  Mpeni salamu zangu Ampliato, mpendwa wangu katika Bwana.  Salimuni Urbano mfanyakazi mwenzetu katika Kristo, na Stako mpendwa wangu. 10  Msalimuni Apele, aliyekubaliwa katika Kristo. Wasalimuni wale wa nyumbani mwa Aristobulo. 11  Msalimuni Herodioni, mtu wangu wa ukoo. Wasalimuni wale wa nyumbani mwa Narkiso walio katika Bwana. 12  Wasalimuni Trifaina na Trifosa, wanawake wanaofanya kazi kwa bidii katika Bwana. Msalimuni Persisi mpendwa wetu, kwa maana mwanamke huyo amefanya kazi kwa bidii katika Bwana. 13  Salimuni Rufo aliyechaguliwa katika Bwana, na mama yake ambaye pia ni mama yangu. 14  Wasalimuni Asinkrito, Flegoni, Hermesi, Patroba, Hermasi, na akina ndugu walio pamoja nao. 15  Wasalimuni Filologo na Yulia, Nerea na dada yake, na Olimpa, na watakatifu wote walio pamoja nao. 16  Salimianeni kwa busu takatifu. Makutaniko yote ya Kristo yanawasalimu ninyi. 17  Sasa ninawahimiza ninyi, akina ndugu, waangalieni wale wanaosababisha migawanyiko na kuweka vikwazo kinyume cha fundisho ambalo mmejifunza, nanyi mjiepushe nao.+ 18  Kwa maana watu wa namna hiyo ni watumwa, si wa Bwana wetu Kristo, bali wa hamu* yao wenyewe, na kwa maneno laini na maneno ya kusifusifu wao huishawishi mioyo ya wasiotambua. 19  Utii wenu umejulikana na watu wote, basi ninashangilia kwa sababu yenu. Hata hivyo, ninataka muwe na hekima kuhusu yaliyo mema, lakini wasio na hatia kuhusu yaliyo maovu.+ 20  Kwa upande wake, Mungu anayetoa amani atamponda Shetani+ chini ya miguu yenu hivi karibuni. Fadhili zisizostahiliwa za Bwana wetu Yesu na ziwe pamoja nanyi. 21  Timotheo, mfanyakazi mwenzangu anawasalimu ninyi, na pia Lukio, Yasoni, na Sosipata, watu wangu wa ukoo.+ 22  Mimi, Tertio, ambaye nimeiandika barua hii, ninawasalimu ninyi katika Bwana. 23  Gayo,+ aliyenikaribisha mimi na kutaniko lote, anawasalimu ninyi. Erasto, mweka hazina* wa jiji, anawasalimu ninyi, na pia Kwarto, ndugu yake. 24 * —— 25  Sasa kwa Yule anayeweza kuwaimarisha ninyi kulingana na habari njema ninayotangaza na kuhubiriwa kwa Yesu Kristo, kulingana na ufunuo wa siri takatifu+ ambayo ilikuwa imefichwa tangu nyakati za zamani 26  lakini sasa imeonyeshwa wazi* na kujulishwa kupitia Maandiko ya kinabii kati ya mataifa yote kulingana na amri ya Mungu anayedumu milele, ili kuendeleza utii kwa imani; 27  kwa Mungu, ambaye peke yake ndiye mwenye hekima,+ kuwe na utukufu kupitia Yesu Kristo milele. Amina.

Maelezo ya Chini

Au “Ninampendekeza.”
Au “nafsi yangu.”
Au “matumbo.”
Au “msimamizi.”
Au “imefunuliwa.”