Kwa Waroma 2:1-29

  • Hukumu ya Mungu dhidi ya Wayahudi na Wagiriki (1-16)

    • Jinsi dhamiri inavyofanya kazi (14, 15)

  • Wayahudi na Sheria (17-24)

  • Kutahiriwa moyoni (25-29)

2  Kwa hiyo huwezi kujitetea, ewe mwanadamu, hata uwe nani,+ ikiwa unahukumu; kwa maana unapomhukumu mwingine, unajihukumu wewe mwenyewe, kwa sababu wewe unayehukumu umezoea kufanya mambo hayohayo.+  Sasa tunajua kwamba, hukumu ya Mungu inapatana na kweli, dhidi ya wale wanaozoea kufanya mambo hayo.  Lakini ewe mwanadamu, unadhani utaponyoka hukumu ya Mungu unapowahukumu wale wanaozoea kufanya mambo hayo na bado wewe unayafanya?  Au je, wewe unadharau utajiri wa fadhili zake+ na uvumilivu*+ na subira,+ kwa sababu hujui kwamba Mungu kwa fadhili zake anajaribu kukuongoza wewe kwenye toba?+  Lakini kulingana na ukaidi wako na moyo wako usiotubu, unajiwekea akiba ya ghadhabu katika siku ya ghadhabu na ya kufunuliwa kwa hukumu ya uadilifu ya Mungu.+  Naye atamlipa kila mmoja kulingana na matendo yake:+  uzima wa milele kwa wale wanaotafuta utukufu na heshima na kutoharibika,+ kwa uvumilivu katika kazi iliyo njema;  hata hivyo, kwa wale wenye ugomvi na wale wasioitii kweli lakini wanatii ukosefu wa uadilifu, kutakuwa na ghadhabu na hasira.+  Kutakuwa na dhiki na taabu kwa kila mtu* anayefanya mabaya, kwanza kwa Myahudi na pia kwa Mgiriki; 10  bali utukufu na heshima na amani kwa kila mtu anayefanya mema, kwanza kwa Myahudi+ na pia kwa Mgiriki.+ 11  Kwa maana Mungu hana ubaguzi.+ 12  Kwa kuwa wote waliofanya dhambi bila sheria wataangamia pia bila sheria;+ bali wote waliofanya dhambi chini ya sheria watahukumiwa kwa sheria.+ 13  Kwa maana wale wanaosikia sheria sio waadilifu mbele za Mungu, bali wale wanaoshika sheria watatangazwa kuwa waadilifu.+ 14  Kwa maana watu wa mataifa wasio na sheria+ wanapofanya kwa asili mambo ya sheria, watu hawa, ingawa hawana sheria, wao ni sheria kwao wenyewe. 15  Wao wenyewe wanaonyesha kuwa yaliyomo katika sheria yameandikwa ndani ya mioyo yao, huku dhamiri yao ikiwatolea ushahidi, na kwa* fikira zao wenyewe wanashtakiwa au hata kutetewa. 16  Hili litatendeka siku ambayo Mungu kupitia Kristo Yesu atahukumu mambo ya siri ya wanadamu,+ kulingana na habari njema ninayoitangaza. 17  Sasa, ikiwa wewe ni Myahudi kwa jina+ na unategemea sheria na kujivunia Mungu, 18  na unajua mapenzi yake na unakubali mambo yaliyo bora kabisa kwa sababu unafundishwa* kutokana na Sheria,+ 19  nawe unasadiki kwamba wewe ni kiongozi wa vipofu, nuru kwa walio gizani, 20  mrekebishaji wa wale wasio na akili, mwalimu wa watoto wadogo, na una picha ya ujuzi na ya ile kweli katika Sheria— 21  hata hivyo, je, wewe unayemfundisha mtu mwingine, hujifundishi mwenyewe?+ Wewe unayehubiri, “Usiibe,”+ je, wewe huiba? 22  Wewe unayesema, “Usifanye uzinzi,”+ je, wewe hufanya uzinzi? Wewe unayechukia sanamu, je, wewe huiba katika mahekalu? 23  Wewe unayejivunia sheria, je, unamvunjia Mungu heshima kwa kuivunja Sheria? 24  Kwa maana “watu wanalikufuru jina la Mungu miongoni mwa mataifa kwa sababu yenu,” kama ilivyoandikwa.+ 25  Kwa kweli, kutahiriwa+ kuna faida ikiwa tu umezoea kuifuata sheria;+ lakini ikiwa wewe huvunja sheria, kutahiriwa kwako kumekuwa kutotahiriwa. 26  Kwa hiyo, ikiwa mtu asiyetahiriwa+ huyashika matakwa ya uadilifu ya Sheria, kutotahiriwa kwake kutahesabiwa kuwa kutahiriwa, sivyo?+ 27  Na mtu asiyetahiriwa kimwili, akiishika Sheria, atakuhukumu wewe ambaye huvunja sheria ingawa una sheria zilizoandikwa na umetahiriwa. 28  Kwa kuwa yeye si Myahudi aliye hivyo kwa nje,+ wala kutahiriwa si kitu kilicho nje, juu ya mwili.+ 29  Bali yeye ni Myahudi aliye hivyo kwa ndani,+ na kutahiriwa kwake ni kule kwa moyo+ kupitia roho, wala si kupitia sheria zilizoandikwa.+ Sifa ya mtu huyo hutoka kwa Mungu, si kwa wanadamu.+

Maelezo ya Chini

Au “ustahimilivu.”
Au “nafsi ya kila mtu.”
Tnn., “katikati ya.”
Au “unafundishwa kwa mdomo.”