Kwa Waroma 7:1-25

  • Kuwekwa huru kutoka katika Sheria kwafafanuliwa (1-6)

  • Dhambi yafunuliwa kupitia Sheria (7-12)

  • Kupambana na dhambi (13-25)

7  Akina ndugu, je, inawezekana kwamba hamjui (kwa maana ninasema na wale wanaoijua sheria) kuwa Sheria ni bwana juu ya mtu anapokuwa hai?  Kwa mfano, mwanamke aliyeolewa amefungwa na sheria kwa mume wake akiwa hai; lakini mume wake akifa, yuko huru kutoka katika sheria ya mume wake.+  Hivyo basi, mume wake akiwa hai, mwanamke huyo ataitwa mzinzi ikiwa atakuwa wa mwanamume mwingine.+ Lakini mume wake akifa, yuko huru kutoka kwa sheria ya mume, basi mwanamke huyo si mzinzi ikiwa ataolewa na mwanamume mwingine.+  Basi, ndugu zangu, ninyi pia mlifanywa wafu kuhusiana na Sheria kupitia mwili wa Kristo, ili muwe wa mwingine,+ yule aliyefufuliwa kutoka kwa wafu,+ ili tumzalie Mungu matunda.+  Kwa maana tulipokuwa tukiishi kulingana na mwili, tamaa zenye dhambi zilizoamshwa na Sheria zilikuwa zikifanya kazi katika miili yetu* ili kuzaa matunda ya kifo.+  Lakini sasa tumewekwa huru kutoka katika Sheria,+ kwa sababu tumekufa kwa kile ambacho kilituzuia, ili tuwe watumwa katika maana mpya kwa roho,+ wala si katika maana ya zamani kwa sheria zilizoandikwa.+  Basi, tuseme nini? Je, Sheria ni dhambi? La hasha! Kwa kweli, singejua dhambi ikiwa Sheria haingekuwapo.+ Kwa mfano, mimi singejua tamaa ikiwa Sheria haingesema: “Usitamani.”+  Lakini dhambi, kwa kutumia amri hiyo ilipata nafasi ya kutokeza ndani yangu tamaa ya kila aina, kwa maana bila sheria dhambi ilikuwa imekufa.+  Kwa kweli, wakati mmoja nilikuwa hai bila sheria. Lakini amri ilipofika, dhambi ikawa hai tena, lakini mimi nikafa.+ 10  Na amri iliyokuwa ya kuongoza kwenye uzima,+ niliiona kuwa inaongoza kwenye kifo. 11  Kwa maana dhambi kwa kutumia amri hiyo ilipata nafasi ya kunishawishi na kuniua kupitia amri. 12  Basi Sheria yenyewe ni takatifu, na amri ni takatifu na yenye uadilifu na ni njema.+ 13  Kwa hiyo, je, lililo jema lilinisababishia kifo? La hasha! Lakini dhambi ilifanya hivyo, ili ionyeshwe kuwa dhambi ndiyo inayoniletea kifo kupitia lile lililo jema,+ ili kupitia amri dhambi iwe mbaya zaidi.+ 14  Kwa maana tunajua kwamba Sheria ni ya kiroho, lakini mimi ni wa kimwili, nimeuzwa kwenye dhambi.+ 15  Kwa kuwa sielewi kile ninachokifanya. Kwa maana sifanyi kile ninachotaka, bali ninafanya kile ninachochukia. 16  Hata hivyo, ikiwa ninafanya jambo nisilotaka, nakubali kwamba Sheria ni nzuri. 17  Lakini sasa si mimi tena ninayelifanya, bali ni dhambi inayokaa ndani yangu.+ 18  Kwa maana najua kwamba ndani yangu, yaani, katika mwili wangu, halikai jambo lolote jema; kwa kuwa nina tamaa ya kufanya mambo mema lakini sina uwezo wa kuyafanya.+ 19  Kwa maana sifanyi jambo jema ninalotaka, bali ninafanya jambo baya nisilotaka. 20  Basi, ikiwa ninafanya jambo nisilotaka, si mimi tena ninayelifanya, bali ni dhambi inayokaa ndani yangu. 21  Basi, mimi naona sheria hii katika hali yangu: Ninapotaka kufanya yaliyo sawa, yaliyo mabaya yapo pamoja nami.+ 22  Kwa kweli naipenda sheria ya Mungu kulingana na mtu niliye kwa ndani,+ 23  lakini ninaona ndani ya mwili wangu* sheria nyingine ikipigana na sheria ya akili yangu+ na kunichukua mateka kwa sheria ya dhambi+ iliyo ndani ya mwili wangu.* 24  Maskini mimi! Ni nani atakayeniokoa kutoka katika mwili unaopatwa na kifo hiki? 25  Shukrani kwa Mungu kupitia Yesu Kristo Bwana wetu! Basi, kwa akili yangu mimi ni mtumwa wa sheria ya Mungu, lakini kwa mwili wangu mimi ni mtumwa wa sheria ya dhambi.+

Maelezo ya Chini

Tnn., “viungo vyetu.”
Tnn., “viungo vyangu.”
Tnn., “viungo vyangu.”