Yeremia 19:1-15

  • Yeremia aambiwa avunje chupa ya udongo (1-15)

    • Kumtolea Baali dhabihu za watoto (5)

19  Yehova alisema hivi: “Nenda ukanunue chupa ya udongo kwa mfinyanzi.+ Uwachukue baadhi ya wazee wa watu na baadhi ya wazee wa makuhani,  nawe uende katika Bonde la Mwana wa Hinomu,+ kwenye njia inayoelekea kwenye Lango la Vigae. Na huko utangaze maneno ninayokuambia.  Utasema, ‘Sikieni neno la Yehova, enyi wafalme wa Yuda na wakaaji wa Yerusalemu. Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: “‘“Niko karibu kuleta msiba mahali hapa, na masikio ya yeyote anayesikia kuuhusu yatawasha.  Ni kwa sababu waliniacha+ na kufanya mahali hapa pasitambuliwe.+ Hapa wanaitolea dhabihu miungu mingine ambayo wao na mababu zao na wafalme wa Yuda hawakuijua, nao wamepajaza mahali hapa damu ya watu wasio na hatia.+  Walijenga mahali pa juu pa Baali ili kuwateketeza motoni wana wao kuwa dhabihu nzima za kuteketezwa kwa Baali,+ jambo ambalo sikuamuru wala kusema na ambalo hata halijawahi kamwe kuingia moyoni mwangu.”’*+  “‘“Kwa hiyo tazameni! siku zinakuja,” asema Yehova, “wakati mahali hapa hapataitwa tena Tofethi au Bonde la Mwana wa Hinomu bali Bonde la Mauaji.+  Nitavunja mipango ya Yuda na Yerusalemu mahali hapa, nami nitawaacha maadui wao wawaangamize kwa upanga na pia wataangamizwa kwa mkono wa wale wanaotaka kuwaua.* Nami nitawapa ndege wa angani na wanyama wa duniani maiti zao kuwa chakula chao.+  Nitalifanya jiji hili kuwa kitu cha kutisha na kitu cha kupigiwa mluzi. Kila mtu atakayepita kando yake atatazama kwa mshtuko na kupiga mluzi kwa sababu ya mapigo yake yote.+  Nami nitawafanya wale nyama ya wana wao na ya mabinti wao, nao watakula kila mmoja nyama ya mwenzake, kwa sababu ya kuzingirwa na kukata tamaa watakapobanwa na maadui wao wanaotaka kuwaua.”’*+ 10  “Kisha uivunje ile chupa mbele ya macho ya wanaume watakaoenda pamoja nawe, 11  nawe uwaambie, ‘Yehova wa majeshi anasema hivi: “Hivi ndivyo nitakavyowavunja watu hawa na jiji hili, kama mtu anavyovunja chombo cha mfinyanzi hivi kwamba hakiwezi kurekebishwa kamwe; nao watawazika wafu katika Tofethi hivi kwamba hakutakuwa na nafasi zaidi ya kuwazika.”’+ 12  “‘Hivyo ndivyo nitakavyopatendea mahali hapa,’ asema Yehova, ‘na wakaaji wake, ili kulifanya jiji hili liwe kama Tofethi. 13  Na nyumba za Yerusalemu na nyumba za wafalme wa Yuda zitakuwa chafu kama mahali hapa, Tofethi,+ naam, nyumba zote ambazo juu ya paa zake walilitolea dhabihu jeshi lote la mbinguni+ na ambako waliimiminia miungu mingine matoleo ya kinywaji.’”+ 14  Yeremia aliporudi kutoka Tofethi ambako Yehova alikuwa amemtuma ili atabiri huko, akasimama katika ua wa nyumba ya Yehova na kuwaambia hivi watu wote: 15  “Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: ‘Tazameni, ninaliletea jiji hili na miji yake yote msiba wote ambao nimetangaza dhidi yake, kwa sababu walikataa kwa ukaidi kuyatii* maneno yangu.’”+

Maelezo ya Chini

Au “sijawahi kamwe kulifikiria.”
Au “wanaotafuta nafsi yao.”
Au “wanaotafuta nafsi yao.”
Tnn., “walizifanya shingo zao kuwa ngumu ili wasitii.”