Yeremia 20:1-18

  • Pashuri ampiga Yeremia (1-6)

  • Yeremia hawezi kuacha kuhubiri (7-13)

    • Ujumbe wa Mungu ni kama moto unaowaka (9)

    • Yehova ni kama shujaa anayetisha (11)

  • Yeremia alalamika (14-18)

20  Sasa Pashuri mwana wa Imeri, kuhani, ambaye pia alikuwa msimamizi mkuu katika nyumba ya Yehova, alikuwa akisikiliza Yeremia alipokuwa akitabiri mambo hayo.  Kisha Pashuri akampiga nabii Yeremia na kumweka katika mikatale+ iliyokuwa kwenye Lango la Juu la Benjamini, lililokuwa katika nyumba ya Yehova.  Lakini siku iliyofuata Pashuri alipomtoa Yeremia katika ile mikatale, Yeremia akamwambia: “Yehova hatakuita tena Pashuri, bali Hofu Kila Upande.+  Kwa maana Yehova anasema hivi: ‘Nitakufanya uwe kitu cha kutia hofu kwako mwenyewe na kwa marafiki wako wote, nao watauawa kwa upanga wa maadui wao huku macho yako yakitazama;+ nami nitawatia watu wote wa Yuda mikononi mwa mfalme wa Babiloni, naye atawapeleka uhamishoni kule Babiloni na kuwaua kwa upanga.+  Nami nitatia mikononi mwa maadui wao utajiri wote wa jiji hili, mali zake zote, vitu vyake vyote vyenye thamani, na hazina zote za wafalme wa Yuda.+ Nao watapora vitu hivyo na kuvichukua na kuvipeleka Babiloni.+  Lakini wewe, Pashuri, na wote wanaoishi katika nyumba yako, mtapelekwa utekwani. Utapelekwa Babiloni na kufia huko, nawe utazikwa huko pamoja na marafiki wako wote, kwa sababu umewatabiria uwongo.’”+   Umenipumbaza, Ee Yehova, nami nikapumbazika. Ulizitumia nguvu zako kunipinga, nawe ukashinda.+ Nimekuwa kitu cha kuchekwa mchana kutwa;Kila mtu ananidhihaki.+   Kwa maana kila mara ninapozungumza, lazima nipaze sauti na kutangaza,“Ukatili na uharibifu!” Kwa maana neno la Yehova limesababisha nitukanwe na kudhihakiwa siku nzima.+   Basi nikasema: “Sitamtaja tena,Wala sitasema tena katika jina lake.”+ Lakini moyoni mwangu neno hilo lilikuwa kama moto unaowaka uliofungiwa mifupani mwangu,Nami nikachoka kulizuia ndani yangu;Singeweza tena kuvumilia.+ 10  Kwa maana nilisikia uvumi mwingi wa uovu;Hofu ilinizunguka.+ “Mshutumuni; na tumshtumu!” Kila mtu aliyenitakia amani alisubiri nianguke:+ “Labda atafanya kosa la kipumbavu,Nasi tutamshinda na kujilipizia kisasi dhidi yake.” 11  Lakini Yehova alikuwa pamoja nami kama shujaa anayetisha.+ Ndiyo sababu wale wanaonitesa watajikwaa nao hawatashinda.+ Wataaibishwa sana, kwa maana hawatafanikiwa. Fedheha yao ya milele haitasahauliwa.+ 12  Lakini wewe, Ee Yehova wa majeshi, unamchunguza mwadilifu;Unaona mawazo ya ndani kabisa* na pia moyo.+ Acha nione ukiwalipiza kisasi,+Kwa maana nimeileta kesi yangu kwako.+ 13  Mwimbieni Yehova! Msifuni Yehova! Kwa maana amemwokoa maskini* kutoka mikononi mwa watenda maovu. 14  Ilaaniwe siku niliyozaliwa! Isibarikiwe siku ambayo mama yangu alinizaa!+ 15  Alaaniwe mtu aliyemletea baba yangu habari njema, akisema: “Umepata mwana, mvulana!” Na kumfanya ashangilie sana. 16  Mtu huyo na awe kama majiji ambayo Yehova aliyaangamiza bila kughairi. Na asikie kilio asubuhi na sauti ya king’ora adhuhuri. 17  Kwa nini hakuniua ndani ya tumbo la uzazi,Ili mama yangu awe kaburi languNa tumbo lake liwe na mimba sikuzote?+ 18  Kwa nini nilitoka tumboniIli kuona taabu na huzuni,Na kumaliza siku zangu kwa aibu?+

Maelezo ya Chini

Au “hisia za ndani kabisa.” Tnn., “figo.”
Au “ameiokoa nafsi ya maskini.”