Yeremia 24:1-10

  • Tini nzuri na tini mbaya (1-10)

24  Kisha Yehova akanionyesha vikapu viwili vya tini vilivyowekwa mbele ya hekalu la Yehova, baada ya Mfalme Nebukadneza* wa Babiloni kumpeleka uhamishoni Yekonia*+ mwana wa Yehoyakimu,+ mfalme wa Yuda, pamoja na wakuu wa Yuda, mafundi, na wahunzi;* aliwatoa Yerusalemu na kuwapeleka Babiloni.+  Kikapu kimoja kilikuwa na tini nzuri sana, kama tini za mapema, lakini kile kikapu kingine kilikuwa na tini mbaya sana, zilikuwa mbaya sana hivi kwamba hazingeweza kuliwa.  Kisha Yehova akaniuliza: “Unaona nini, Yeremia?” Basi nikasema: “Tini; tini nzuri ni nzuri sana, na tini mbaya ni mbaya sana, hivi kwamba haziwezi kuliwa.”+  Ndipo neno la Yehova likanijia likisema:  “Yehova Mungu wa Israeli anasema hivi: ‘Kama hizi tini nzuri, ndivyo nitakavyowaona kwa njia nzuri wale watu wa Yuda waliohamishwa, ambao nimewatoa mahali hapa na kuwapeleka katika nchi ya Wakaldayo.  Jicho langu litaendelea kuwatazama kwa faida yao, nami nitawarudisha katika nchi hii.+ Nitawajenga, nami sitawabomoa; nitawapanda, nami sitawang’oa.+  Nami nitawapa moyo wa kunijua, kwamba mimi ni Yehova.+ Watakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wao,+ kwa maana watarudi kwangu kwa moyo wao wote.+  “‘Lakini kuhusu tini mbaya ambazo ni mbaya sana hivi kwamba haziwezi kuliwa,+ Yehova anasema hivi: “Ndivyo nitakavyomwona Mfalme Sedekia+ wa Yuda, wakuu wake, wakaaji wa Yerusalemu waliobaki katika nchi hii, na wale wanaokaa nchini Misri.+  Nitawafanya wawe kitu cha kutisha na msiba kwa falme zote za dunia,+ shutuma, methali, kitu cha kudhihakiwa, na laana+ kila mahali nitakapowatawanya.+ 10  Nami nitawaletea upanga,+ njaa kali, na ugonjwa hatari,+ mpaka waangamie kutoka katika nchi niliyowapa wao na mababu zao.”’”

Maelezo ya Chini

Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.
Pia anaitwa Yehoyakini na Yekonia.
Au labda, “wajenzi wa maboma ya ulinzi.”