Yeremia 26:1-24

  • Maadui watishia kumuua Yeremia (1-15)

  • Yeremia aokolewa (16-19)

    • Unabii wa Mika wanukuliwa (18)

  • Nabii Uriya (20-24)

26  Mwanzoni mwa utawala wa Yehoyakimu+ mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda, neno hili lilikuja kutoka kwa Yehova:  “Yehova anasema hivi: ‘Simama katika ua wa nyumba ya Yehova useme kuhusu* watu wote wa majiji ya Yuda wanaoingia ili kuabudu* katika nyumba ya Yehova. Waambie kila kitu ninachokuamuru; usiondoe hata neno moja.  Labda watasikiliza na kila mmoja ataiacha njia yake ovu, nami nitabadili nia yangu* kuhusu msiba ninaokusudia kuwaletea kwa sababu ya matendo yao maovu.+  Waambie, “Yehova anasema hivi: ‘Ikiwa hamtanisikiliza kwa kufuata sheria* yangu niliyoweka mbele yenu,  kwa kuyasikiliza maneno ya watumishi wangu manabii, ninaowatuma kwenu tena na tena,* ambao hamjawasikiliza,+  basi nitaifanya nyumba hii kama Shilo,+ nami nitalifanya jiji hili kuwa kitu cha kulaaniwa na mataifa yote ya dunia.’”’”+  Na makuhani na manabii na watu wote wakamsikia Yeremia akisema maneno hayo ndani ya nyumba ya Yehova.+  Yeremia alipomaliza kusema mambo yote ambayo Yehova alimwamuru awaambie watu wote, ndipo makuhani na manabii na watu wote wakamkamata na kusema: “Hakika utakufa.  Kwa nini umetabiri katika jina la Yehova, ukisema, ‘Nyumba hii itakuwa kama Shilo, na jiji hili litaangamizwa na kuachwa bila mkaaji’?” Na watu wote wakakusanyika kumzunguka Yeremia ndani ya nyumba ya Yehova. 10  Wakuu wa Yuda waliposikia maneno hayo, wakapanda kutoka katika nyumba ya* mfalme wakaenda katika nyumba ya Yehova na kuketi kwenye njia inayoelekea kwenye lango jipya la Yehova.+ 11  Makuhani na manabii wakawaambia hivi wakuu na watu wote: “Mtu huyu anastahili hukumu ya kifo,+ kwa sababu ametabiri dhidi ya jiji hili kama mlivyosikia kwa masikio yenu wenyewe.”+ 12  Ndipo Yeremia akawaambia wakuu wote na watu wote: “Yehova ndiye aliyenituma kutabiri dhidi ya nyumba hii na dhidi ya jiji hili maneno yote ambayo mmeyasikia.+ 13  Basi sasa rekebisheni njia zenu na matendo yenu nanyi mtii sauti ya Yehova Mungu wenu, naye Yehova atabadili nia yake* kuhusu msiba aliotangaza dhidi yenu.+ 14  Lakini mimi niko mikononi mwenu. Nitendeeni jambo lolote mnaloona kuwa jema na sawa machoni penu. 15  Ila tu mjue kwa hakika kwamba mkiniua, mtajiletea damu isiyo na hatia juu yenu na juu ya jiji hili na juu ya wakaaji wake, kwa maana kwa kweli Yehova alinituma kwenu ili niseme maneno haya mkiyasikia.” 16  Ndipo wakuu na watu wote wakawaambia makuhani na manabii: “Mtu huyu hastahili hukumu ya kifo, kwa maana alizungumza nasi katika jina la Yehova Mungu wetu.” 17  Zaidi ya hayo, baadhi ya wazee wa nchi wakasimama na kuanza kuliambia hivi kutaniko lote la watu: 18  “Mika+ wa Moreshethi alikuwa akitabiri katika siku za utawala wa Mfalme Hezekia+ wa Yuda, akawaambia watu wote wa Yuda, ‘Yehova wa majeshi anasema hivi: “Sayuni litalimwa kama shamba,Yerusalemu litakuwa marundo ya magofu,+Na mlima wa Nyumba* utakuwa kama vilima msituni.”’*+ 19  “Je, Mfalme Hezekia wa Yuda na watu wote wa Yuda walimuua? Je, hakumwogopa Yehova na kumwomba Yehova kibali,* hivi kwamba Yehova akabadili nia yake* kuhusu msiba aliotangaza dhidi yao?+ Basi tuko karibu kujiletea msiba mkubwa. 20  “Na kulikuwa na mtu mwingine aliyetabiri katika jina la Yehova, Uriya mwana wa Shemaya kutoka Kiriath-yearimu,+ aliyetabiri dhidi ya jiji hili na dhidi ya nchi hii kwa maneno kama ya Yeremia. 21  Mfalme Yehoyakimu+ na wanaume wake wote hodari na wakuu wote wakayasikia maneno yake, na mfalme alitaka kumuua.+ Uriya aliposikia jambo hilo, mara moja akaogopa na kukimbilia Misri. 22  Kisha Mfalme Yehoyakimu akamtuma Elnathani+ mwana wa Akbori pamoja na watu wengine kwenda Misri. 23  Wakamchukua Uriya kutoka Misri na kumpeleka kwa Mfalme Yehoyakimu, naye akamuua kwa upanga+ na kuitupa maiti yake katika makaburi ya watu wa kawaida.” 24  Lakini Ahikamu+ mwana wa Shafani+ alimsaidia Yeremia, ili asitiwe mikononi mwa watu na kuuawa.+

Maelezo ya Chini

Au “uwaambie.”
Au “kuinama.”
Au “nitaghairi.”
Au “mafundisho.”
Tnn., “ambao ninaamka mapema na kuwatuma.”
Au “jumba la.”
Au “ataghairi.”
Au “mlima wa hekalu.”
Au “kilima chenye msitu.”
Au “akaghairi.”
Au “hakujaribu kuutuliza uso wa Yehova.”