Yeremia 27:1-22

  • Nira ya Babiloni (1-11)

  • Sedekia aambiwa ajitiishe kwa Babiloni (12-22)

27  Mwanzoni mwa utawala wa Yehoyakimu mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda, neno hili lilimjia Yeremia kutoka kwa Yehova:  “Yehova ameniambia hivi: ‘Jitengenezee mikanda na nira, nawe uziweke kwenye shingo yako.  Kisha upeleke vitu hivyo kwa mfalme wa Edomu,+ mfalme wa Moabu,+ mfalme wa Waamoni,+ mfalme wa Tiro,+ na kwa mfalme wa Sidoni+ kwa mkono wa wajumbe waliokuja Yerusalemu kwa Mfalme Sedekia wa Yuda.  Uwape amri hii kwa ajili ya mabwana wao: “‘“Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema; waambieni hivi mabwana wenu:  ‘Mimi ndiye niliyeiumba dunia, wanadamu, na wanyama walio duniani kwa nguvu zangu kuu na kwa mkono wangu ulionyooshwa; nami nimempa yeyote ninayetaka.*+  Na sasa mimi mwenyewe nimezitia nchi hizi zote mikononi mwa mtumishi wangu Mfalme Nebukadneza+ wa Babiloni; nimempa hata wanyama wa mwituni ili wamtumikie.  Mataifa yote yatamtumikia yeye na mwanawe na mjukuu wake mpaka wakati wa nchi yake utakapofika,+ wakati ambapo mataifa mengi na wafalme wakuu watamfanya kuwa mtumwa wao.’+  “‘“‘Ikiwa taifa lolote au ufalme utakataa kumtumikia Mfalme Nebukadneza wa Babiloni na kukataa kuweka shingo yake chini ya nira ya mfalme wa Babiloni, nitaliadhibu taifa hilo kwa upanga,+ kwa njaa kali, na kwa ugonjwa hatari,’ asema Yehova, ‘mpaka nitakapowaangamiza kwa mkono wake.’  “‘“‘Kwa hiyo, msiwasikilize manabii wenu, waaguzi* wenu, waota-ndoto wenu, wachawi wenu, na walozi wenu, wanaowaambia: “Hamtamtumikia mfalme wa Babiloni.” 10  Kwa maana wanawatabiria uwongo, ili mpelekwe mbali na nchi yenu, nami nitawatawanya ninyi, nanyi mtaangamia. 11  “‘“‘Lakini taifa litakaloweka shingo yake chini ya nira ya mfalme wa Babiloni na kumtumikia, nitaliruhusu libaki* kwenye nchi yake,’ asema Yehova, ‘ili kuilima na kukaa ndani yake.’”’” 12  Pia nilimwambia Mfalme Sedekia+ wa Yuda maneno hayohayo, nikisema: “Wekeni shingo zenu chini ya nira ya mfalme wa Babiloni na mumtumikie yeye na watu wake, nanyi mtaendelea kuishi.+ 13  Kwa nini wewe na watu wako mfe kwa upanga,+ kwa njaa kali,+ na kwa ugonjwa hatari,+ kama Yehova alivyosema kuhusu taifa ambalo halitamtumikia mfalme wa Babiloni? 14  Msiyasikilize maneno ya manabii wanaowaambia, ‘Hamtamtumikia mfalme wa Babiloni,’+ kwa sababu wanawatabiria uwongo.+ 15  “‘Kwa maana sijawatuma,’ asema Yehova, ‘lakini wanatabiri uwongo katika jina langu, ili mwishowe niwatawanye na mwangamie, ninyi na manabii wanaowatabiria ninyi.’”+ 16  Nami nikawaambia makuhani na watu hawa wote, “Yehova anasema hivi: ‘Msiyasikilize maneno ya manabii wenu wanaowatabiria wakisema: “Tazameni! Vyombo vya nyumba ya Yehova vitarudishwa kutoka Babiloni hivi karibuni!”+ kwa maana wanawatabiria uwongo.+ 17  Msiwasikilize. Mtumikieni mfalme wa Babiloni nanyi mtaendelea kuishi.+ Kwa nini jiji hili liwe magofu? 18  Lakini ikiwa wao ni manabii na ikiwa wana neno la Yehova, tafadhali acheni wamwombe Yehova wa majeshi kwamba vyombo vilivyobaki katika nyumba ya Yehova, katika nyumba ya* mfalme wa Yuda, na Yerusalemu visipelekwe Babiloni.’ 19  “Kwa maana Yehova wa majeshi anasema hivi kuhusu zile nguzo,+ ile Bahari,*+ yale magari,+ na vyombo vilivyobaki vilivyoachwa katika jiji hili, 20  ambavyo Mfalme Nebukadneza wa Babiloni hakuvichukua alipompeleka uhamishoni Yekonia mwana wa Yehoyakimu, mfalme wa Yuda, kutoka Yerusalemu hadi Babiloni, pamoja na watu wote wenye vyeo wa Yuda na Yerusalemu;+ 21  naam, Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli anasema hivi kuhusu vyombo vilivyobaki katika nyumba ya Yehova, katika nyumba ya* mfalme wa Yuda, na Yerusalemu: 22  ‘“Vitapelekwa Babiloni,+ navyo vitabaki huko mpaka siku nitakapovikazia fikira,” asema Yehova. “Kisha nitavileta na kuvirudisha mahali hapa.”’”+

Maelezo ya Chini

Tnn., “yule anayefaa machoni pangu.”
Au “wabashiri.”
Tnn., “lipumzike.”
Au “jumba la.”
Yaani, Bahari ya shaba ya hekalu.
Au “jumba la.”