Yeremia 28:1-17

  • Nabii wa uwongo Hanania ampinga nabii Yeremia (1-17)

28  Mwaka huohuo, mwanzoni mwa utawala wa Mfalme Sedekia+ wa Yuda, katika mwaka wa nne, mwezi wa tano, nabii Hanania mwana wa Azuri kutoka Gibeoni+ aliniambia hivi katika nyumba ya Yehova mbele ya makuhani na watu wote:  “Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi, ‘Nitaivunja nira ya mfalme wa Babiloni.+  Katika muda wa miaka miwili* nitavirudisha mahali hapa vyombo vyote vya nyumba ya Yehova ambavyo Mfalme Nebukadneza wa Babiloni alivichukua mahali hapa na kuvipeleka Babiloni.’”+  “‘Nami nitamrudisha mahali hapa Yekonia+ mwana wa Yehoyakimu,+ mfalme wa Yuda, na watu wote wa Yuda waliohamishwa na kupelekwa Babiloni,’+ asema Yehova, ‘kwa maana nitaivunja nira ya mfalme wa Babiloni.’”  Kisha nabii Yeremia akazungumza na nabii Hanania mbele ya makuhani na watu wote waliokuwa wamesimama katika nyumba ya Yehova.  Nabii Yeremia akasema: “Amina!* Yehova na afanye hivyo! Yehova na atimize maneno yako uliyotabiri kwa kuvirudisha mahali hapa vyombo vya nyumba ya Yehova kutoka Babiloni na pia watu wote waliopelekwa uhamishoni!  Hata hivyo, tafadhali sikia ujumbe huu ninaosema masikioni mwako na masikioni mwa watu wote.  Zamani za kale manabii walionitangulia mimi na waliokutangulia wewe walikuwa wakitabiri kuhusu nchi nyingi na falme kubwa, kuhusu vita, misiba, na magonjwa hatari.  Nabii akitabiri amani na neno la nabii huyo litimie, basi itajulikana kwamba kwa kweli Yehova amemtuma nabii huyo.” 10  Ndipo nabii Hanania akaichukua ile nira kutoka shingoni mwa nabii Yeremia na kuivunja.+ 11  Kisha Hanania akasema mbele ya watu wote: “Yehova anasema hivi: ‘Hivyo ndivyo nitakavyoivunja nira ya Mfalme Nebukadneza wa Babiloni kutoka shingoni mwa mataifa yote katika muda wa miaka miwili.’”+ Kisha nabii Yeremia akaenda zake. 12  Baada ya nabii Hanania kuivunja ile nira kutoka shingoni mwa nabii Yeremia, ujumbe huu wa Yehova ukamjia Yeremia: 13  “Nenda umwambie Hanania, ‘Yehova anasema hivi: “Umevunja nira za mbao,+ lakini badala yake utatengeneza nira za chuma.” 14  Kwa maana Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: “Nitaweka nira ya chuma juu ya shingo ya mataifa haya yote, ili yamtumikie Mfalme Nebukadneza wa Babiloni, nayo lazima yamtumikie.+ Nitampa hata wanyama wa mwituni.”’”+ 15  Kisha nabii Yeremia akamwambia nabii Hanania:+ “Tafadhali, sikiliza, ewe Hanania! Yehova hakukutuma wewe, bali umewafanya watu hawa wautumaini uwongo.+ 16  Kwa hiyo Yehova anasema hivi: ‘Tazama! Ninakuondoa katika uso wa nchi. Utakufa mwaka huu, kwa maana umewachochea watu wamwasi Yehova.’”+ 17  Basi nabii Hanania akafa mwaka huo, katika mwezi wa saba.

Maelezo ya Chini

Tnn., “miaka miwili ya siku.”
Au “Na iwe hivyo!”