Yeremia 29:1-32

  • Barua ya Yeremia kwa watu walio uhamishoni Babiloni (1-23)

    • Waisraeli watarudi baada ya miaka 70 (10)

  • Ujumbe kwa Shemaya (24-32)

29  Haya ndiyo maneno ya barua ambayo nabii Yeremia aliwatumia kutoka Yerusalemu wazee waliobaki miongoni mwa watu waliopelekwa uhamishoni, makuhani, manabii, na watu wote, ambao Nebukadneza alikuwa amewatoa Yerusalemu na kuwapeleka uhamishoni Babiloni,  baada ya Mfalme Yekonia+ na mama malkia,+ maofisa wa makao ya mfalme, wakuu wa Yuda na Yerusalemu, na mafundi na wahunzi* kuondoka Yerusalemu.+  Aliituma barua hiyo kwa mkono wa Elasa mwana wa Shafani+ na Gemaria mwana wa Hilkia, ambao Mfalme Sedekia+ wa Yuda aliwatuma kwenda Babiloni kwa Mfalme Nebukadneza wa Babiloni. Barua hiyo ilisema hivi:  “Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anawaambia hivi watu wote waliohamishwa, ambao aliwafanya wapelekwe uhamishoni Babiloni kutoka Yerusalemu,  ‘Jengeni nyumba mkae ndani yake. Pandeni bustani na mle matunda yake.  Oeni wake mzae wana na mabinti; wachukulieni wana wenu wake na kuwaoza mabinti wenu, ili wao pia wazae wana na mabinti. Muwe wengi huko, msipungue.  Nanyi tafuteni amani kwa ajili ya jiji ambamo nimewapeleka uhamishoni, nanyi msali kwa Yehova kwa ajili ya jiji hilo, kwa maana jiji hilo likiwa na amani mtakuwa na amani.+  Kwa maana Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: “Msiwaruhusu manabii wenu na waaguzi* wenu walio miongoni mwenu wawadanganye,+ nanyi msisikilize ndoto wanazoota.  Kwa maana ‘wanawatabiria uwongo katika jina langu. Mimi sijawatuma,’+ asema Yehova.”’” 10  “Kwa maana Yehova anasema hivi: ‘Miaka 70 itakapotimia huko Babiloni nitawakazia ninyi fikira,+ nami nitatimiza ahadi yangu kwa kuwarudisha mahali hapa.’+ 11  “‘Kwa maana ninajua vizuri mawazo ninayofikiria kuwaelekea ninyi,’ asema Yehova, ‘mawazo ya amani, wala si ya msiba,+ ili niwape ninyi wakati ujao na tumaini.+ 12  Nanyi mtaniita na kuja na kusali kwangu, nami nitawasikiliza.’+ 13  “‘Mtanitafuta na kunipata,+ kwa maana mtanitafuta kwa moyo wenu wote.+ 14  Nami nitawaruhusu mnipate,’+ asema Yehova. ‘Nami nitawakusanya mateka wenu na kuwakusanya ninyi pamoja kutoka katika mataifa yote na sehemu zote nilizowatawanya,’+ asema Yehova. ‘Nami nitawarudisha mahali nilipowatoa nikawapeleka uhamishoni.’+ 15  “Lakini ninyi mmesema, ‘Yehova ametuinulia manabii katika Babiloni.’ 16  “Kwa maana Yehova anamwambia hivi mfalme anayeketi kwenye kiti cha ufalme cha Daudi+ na watu wote wanaokaa katika jiji hili, ndugu zenu ambao hawakwenda pamoja nanyi uhamishoni, 17  ‘Yehova wa majeshi anasema hivi: “Tazameni, ninatuma dhidi yao upanga, njaa kali, na ugonjwa hatari,+ nami nitawafanya kuwa kama tini zilizooza* ambazo ni mbaya sana hivi kwamba haziwezi kuliwa.”’+ 18  “‘Nami nitawafuatia kwa upanga,+ kwa njaa kali, na kwa ugonjwa hatari, nami nitawafanya wawe kitu cha kutisha kwa falme zote za dunia,+ na laana, na kitu cha kushangaza, kitu cha kupigiwa mluzi,+ na shutuma miongoni mwa mataifa yote ambako nitawatawanya,+ 19  kwa sababu hawakuyasikiliza maneno yangu niliyowapa kupitia watumishi wangu manabii,’ asema Yehova, ‘ambao niliwatuma tena na tena.’*+ “‘Lakini hamkusikiliza,’+ asema Yehova. 20  “Kwa hiyo, sikieni neno la Yehova, ninyi nyote mliopelekwa uhamishoni, niliowatoa Yerusalemu na kuwapeleka Babiloni. 21  Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi kuhusu Ahabu mwana wa Kolaya na kuhusu Sedekia mwana wa Maaseya, wanaowatabiria uwongo katika jina langu:+ ‘Nitawatia mikononi mwa Mfalme Nebukadneza* wa Babiloni, naye atawaua mbele ya macho yenu. 22  Na kile kitakachowapata kitakuwa laana itakayosemwa na watu wote wa Yuda walio uhamishoni Babiloni: “Yehova na akutendee kama Sedekia na kama Ahabu, ambao mfalme wa Babiloni aliwateketeza motoni!” 23  kwa maana wametenda kwa aibu katika Israeli,+ wakifanya uzinzi na wake za majirani wao na kusema maneno ya uwongo katika jina langu, maneno ambayo sikuwaamuru.+ “‘“Mimi Ndiye ninayejua, nami ni shahidi,”+ asema Yehova.’” 24  “Nawe utamwambia hivi Shemaya+ wa Nehelamu: 25  ‘Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: “Kwa sababu ulituma barua katika jina lako kwa watu wote walio Yerusalemu, kwa Sefania+ mwana wa Maaseya, kuhani, na kwa makuhani wote, ukisema, 26  ‘Yehova amekuweka kuwa kuhani badala ya kuhani Yehoyada, ili uwe mwangalizi wa nyumba ya Yehova, uwe msimamizi wa mwendawazimu yeyote anayetenda kama nabii na kumweka katika mikatale na katika kongwa;*+ 27  basi, kwa nini hujamkemea Yeremia wa Anathothi,+ anayetenda kama nabii wenu?+ 28  Kwa maana hata alitutumia ujumbe Babiloni, akisema: “Muda mrefu utapita! Jengeni nyumba na mkae ndani yake. Pandeni bustani na mle matunda yake,+—”’”’” 29  Kuhani Sefania+ alipoisoma barua hiyo mbele ya nabii Yeremia, 30  Neno la Yehova likamjia Yeremia likisema: 31  “Watumie ujumbe watu wote waliopelekwa uhamishoni, ukisema, ‘Yehova anasema hivi kumhusu Shemaya wa Nehelamu: “Kwa sababu Shemaya aliwatabiria, ingawa sikumtuma, naye akajaribu kuwafanya mtumaini uwongo,+ 32  kwa hiyo Yehova anasema hivi: ‘Ninamkazia fikira Shemaya wa Nehelamu na wazao wake. Hakuna yeyote miongoni mwa watu wake atakayeokoka kati ya watu hawa, naye hataona mema nitakayowatendea watu wangu,’ asema Yehova, ‘kwa maana amewachochea watu wamwasi Yehova.’”’”

Maelezo ya Chini

Au labda, “wajenzi wa maboma ya ulinzi.”
Au “wabashiri.”
Au labda, “zilizopasuka.”
Tnn., “nikiamka mapema na kuwatuma.”
Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.
Au “vyuma vya shingoni.”