Yeremia 32:1-44

  • Yeremia anunua shamba (1-15)

  • Sala ya Yeremia (16-25)

  • Jibu la Yehova (26-44)

32  Neno lililomjia Yeremia kutoka kwa Yehova katika mwaka wa 10 wa utawala wa Mfalme Sedekia wa Yuda, yaani, mwaka wa 18 wa utawala wa Nebukadneza.*+  Wakati huo majeshi ya mfalme wa Babiloni yalikuwa yakizingira Yerusalemu, naye nabii Yeremia alikuwa amezuiliwa katika Ua wa Walinzi+ katika nyumba ya* mfalme wa Yuda.  Kwa maana Mfalme Sedekia wa Yuda alikuwa amemzuilia,+ akisema: “Kwa nini unatabiri hivi? Unasema, ‘Yehova anasema hivi: “Nitalitia jiji hili mikononi mwa mfalme wa Babiloni, naye ataliteka,+  na Mfalme Sedekia wa Yuda hataponyoka kutoka kwa Wakaldayo, kwa maana hakika atatiwa mikononi mwa mfalme wa Babiloni, naye atazungumza naye uso kwa uso na kumwona jicho kwa jicho.”+  ‘Atampeleka Sedekia Babiloni, naye atakaa huko mpaka nitakapomkazia fikira,’ asema Yehova. ‘Ingawa mnaendelea kupigana na Wakaldayo, hamtafanikiwa.’”+  Yeremia akasema: “Neno la Yehova limenijia likisema,  ‘Hanameli mwana wa Shalumu ndugu ya baba yako atakuja kwako na kukuambia: “Nunua shamba langu lililo Anathothi,+ kwa sababu una haki ya kwanza ya kulikomboa.”’”+  Hanameli mwana wa ndugu ya baba yangu akaja kwangu, kama Yehova alivyosema, katika Ua wa Walinzi, naye akaniambia: “Tafadhali nunua shamba langu lililo Anathothi, katika nchi ya Benjamini, kwa maana una haki ya kulimiliki na kulikomboa. Linunue liwe lako.” Ndipo nikajua kwamba hilo lilikuwa neno la Yehova.  Basi nikalinunua shamba lililokuwa Anathothi kutoka kwa Hanameli mwana wa ndugu ya baba yangu. Nikampimia pesa,+ shekeli saba* na vipande kumi vya fedha. 10  Kisha nikaandika katika hati,+ nikaitia muhuri, nikawaita mashahidi,+ nami nikapima pesa kwa mizani. 11  Nikaichukua ile hati ya ununuzi, iliyotiwa muhuri kulingana na amri na masharti ya kisheria, na pia hati ambayo haikuwa na muhuri, 12  kisha nikampa hati hiyo ya ununuzi Baruku+ mwana wa Neria+ mwana wa Mahseya mbele ya Hanameli mwana wa ndugu ya baba yangu, wale mashahidi walioandika kwenye hati ya ununuzi, na Wayahudi wote waliokuwa wameketi katika Ua wa Walinzi.+ 13  Sasa nikamwamuru Baruku mbele yao, nikisema: 14  “Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: ‘Chukua hati hizi, hati hii ya ununuzi, iliyotiwa muhuri na ile hati nyingine isiyo na muhuri, nawe uziweke katika chombo cha udongo, ili zihifadhiwe kwa muda mrefu.’ 15  Kwa maana Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: ‘Nyumba na mashamba na mashamba ya mizabibu yatanunuliwa tena katika nchi hii.’”+ 16  Kisha nikasali kwa Yehova baada ya kumpa Baruku mwana wa Neria ile hati ya ununuzi, nikisema: 17  “Ole wangu, Ee Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova! Tazama! Uliumba mbingu na dunia kwa nguvu zako kuu+ na kwa mkono wako ulionyooshwa. Hakuna jambo la ajabu sana kwako, 18  Wewe unayewatendea kwa upendo mshikamanifu maelfu ya watu, lakini unawaadhibu wana kwa sababu ya makosa ya baba zao,+ Mungu wa kweli, uliye mkuu na Mwenye nguvu, ambaye jina lako ni Yehova wa majeshi. 19  Wewe ni mkuu katika kutoa mashauri* na matendo yako ni yenye nguvu,+ wewe ambaye macho yako huchunguza njia zote za wanadamu,+ ili kumlipa kila mtu kulingana na njia zake na matendo yake.+ 20  Umefanya ishara na miujiza katika nchi ya Misri, nayo inajulikana mpaka leo hii, na hivyo umejijengea jina katika Israeli na kati ya wanadamu,+ kama ilivyo leo. 21  Nawe uliwatoa watu wako Waisraeli nchini Misri, kwa ishara, kwa miujiza, kwa mkono wenye nguvu, kwa mkono ulionyooshwa, na kwa matendo yanayoogopesha.+ 22  “Baada ya muda ukawapa nchi hii ambayo uliapa kwamba utawapa mababu zao,+ nchi inayotiririka maziwa na asali.+ 23  Nao wakaingia na kuimiliki, lakini hawakuitii sauti yako wala kutembea katika sheria yako. Hawakufanya lolote kati ya mambo uliyowaamuru wafanye, hivi kwamba ukawaletea msiba huu wote.+ 24  Tazama! Watu wamekuja na maboma ya kuzingira ili kuliteka jiji hili,+ na kwa sababu ya upanga,+ njaa kali, na ugonjwa hatari,+ hakika jiji litaanguka mikononi mwa Wakaldayo wanaolishambulia; mambo uliyosema yametimia yote, kama unavyoona sasa. 25  Lakini umeniambia, Ee Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, ‘Nunua shamba kwa pesa na uwaite mashahidi,’ ingawa kwa hakika jiji litatiwa mikononi mwa Wakaldayo.” 26  Ndipo neno la Yehova likamjia Yeremia likisema: 27  “Mimi ndimi, Yehova, Mungu wa wanadamu wote.* Je, kuna jambo lolote ambalo ni la ajabu sana kwangu? 28  Basi Yehova anasema hivi: ‘Tazama, ninalitia jiji hili mikononi mwa Wakaldayo na mikononi mwa Mfalme Nebukadneza* wa Babiloni, naye ataliteka.+ 29  Na Wakaldayo wanaolishambulia jiji hili wataingia na kulichoma moto jiji hili na kuliteketeza+ pamoja na nyumba ambazo juu ya paa zake watu walimtolea dhabihu Baali na kuitolea miungu mingine matoleo ya kinywaji ili kunikasirisha.’+ 30  “‘Kwa maana watu wa Israeli na wa Yuda wametenda maovu tu machoni pangu, tangu ujana wao;+ watu wa Israeli wanaendelea kunikasirisha kwa kazi ya mikono yao,’ asema Yehova. 31  ‘Kwa maana jiji hili, tangu siku walipolijenga mpaka leo hii, limekuwa tu likinikasirisha na kunitia ghadhabu,+ hivi kwamba ni lazima liondolewe mbele za uso wangu,+ 32  kwa sababu ya uovu wote ambao watu wa Israeli na wa Yuda walifanya ili kunikasirisha—wao, wafalme wao,+ wakuu wao,+ makuhani wao, manabii wao,+ na watu wa Yuda na wakaaji wa Yerusalemu. 33  Waliendelea kunigeuzia migongo yao, si nyuso zao;+ ingawa nilijaribu kuwafundisha tena na tena,* hakuna hata mmoja wao aliyesikiliza ili kupokea nidhamu.+ 34  Nao waliweka sanamu zao zinazochukiza katika nyumba inayoitwa kwa jina langu, ili kuitia unajisi.+ 35  Isitoshe, walijenga mahali pa juu pa Baali katika Bonde la Mwana wa Hinomu,*+ ili kuwateketeza* motoni wana wao na mabinti wao kwa ajili ya Moleki,+ jambo ambalo sikuwaamuru,+ na ambalo halijawahi kamwe kuingia moyoni mwangu,* kufanya jambo kama hilo linalochukiza, na kusababisha watu wa Yuda watende dhambi.’ 36  “Kwa hiyo Yehova Mungu wa Israeli anasema hivi kuhusu jiji hili ambalo mnasema litatiwa mikononi mwa mfalme wa Babiloni kwa upanga, kwa njaa kali, na kwa ugonjwa hatari, 37  ‘Nitawakusanya pamoja kutoka katika nchi zote ambako niliwatawanya kwa hasira yangu na kwa ghadhabu yangu na kwa ukali mwingi,+ nami nitawarudisha mahali hapa na kufanya wakae kwa usalama.+ 38  Nao watakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wao.+ 39  Nami nitawapa moyo mmoja+ na njia moja ili waniogope sikuzote, kwa faida yao wenyewe na kwa faida ya watoto wao baada yao.+ 40  Nami nitafanya pamoja nao agano linalodumu milele,+ kwamba sitaacha kuwatendea mema;+ nami nitatia hofu yangu katika mioyo yao, hivi kwamba hawataniacha.+ 41  Nitafurahia kuwatendea mema,+ nami nitawapanda kwa uthabiti katika nchi hii,+ kwa moyo wangu wote na kwa nafsi* yangu yote.’” 42  “Kwa maana Yehova anasema hivi: ‘Kama nilivyowaletea watu hawa msiba huu mkubwa, ndivyo nitakavyowaletea mema yote ninayowaahidi.*+ 43  Na mashamba yatanunuliwa tena katika nchi hii,+ ingawa mnasema: “Ni nchi yenye ukiwa isiyo na mwanadamu wala mnyama, nayo imetiwa mikononi mwa Wakaldayo.”’ 44  “‘Mashamba yatanunuliwa kwa pesa, hati za ununuzi zitaandikwa na kutiwa muhuri, nao mashahidi wataitwa katika nchi ya Benjamini,+ katika maeneo yanayozunguka Yerusalemu, katika majiji ya Yuda,+ katika majiji ya eneo lenye milima, na katika majiji ya eneo la chini,+ na katika majiji ya kusini, kwa sababu nitawarudisha mateka wao,’+ asema Yehova.”

Maelezo ya Chini

Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.
Au “jumba la.”
Shekeli moja ilikuwa na uzito wa gramu 11.4. Angalia Nyongeza B14.
Au “mkuu kuhusiana na makusudi yako.”
Tnn., “wote wenye mwili wa nyama.”
Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.
Tnn., “kuamka mapema na kuwafundisha.”
Angalia Kamusi, “Gehena.”
Tnn., “kuwapitisha.”
Au “sijawahi kamwe kulifikiria.”
Angalia Kamusi.
Au “vitu vyote vizuri ninavyowaahidi.”