Yeremia 35:1-19

  • Warekabu waonyesha utii wa pekee (1-19)

35  Neno lililomjia Yeremia kutoka kwa Yehova katika siku za Yehoyakimu+ mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda likisema:  “Nenda katika nyumba ya Warekabu+ na uzungumze nao na kuwaleta katika nyumba ya Yehova, katika mojawapo ya vyumba vya kulia chakula;* nawe uwape divai wanywe.”  Basi nikampeleka Yaazania mwana wa Yeremia mwana wa Habasinia, ndugu zake, wanawe wote, na nyumba yote ya Warekabu  kwenye nyumba ya Yehova. Niliwapeleka katika chumba cha kulia chakula cha wana wa Hanani mwana wa Igdalia, mtu wa Mungu wa kweli, kilichokuwa kando ya chumba cha kulia chakula cha wakuu ambacho kilikuwa juu ya chumba cha kulia chakula cha Maaseya mwana wa Shalumu mlinzi wa mlango.  Kisha nikaweka vikombe na bilauri zilizojaa divai mbele ya watu wa nyumba ya Warekabu na kuwaambia: “Kunyweni divai.”  Lakini wakasema: “Hatutakunywa divai, kwa sababu Yehonadabu*+ mwana wa Rekabu, babu yetu, alituamuru hivi: ‘Ninyi wala wana wenu hampaswi kamwe kunywa divai.  Nanyi hampaswi kujenga nyumba, kupanda mbegu, au kupanda shamba la mizabibu au kulimiliki. Badala yake, mnapaswa kukaa katika mahema sikuzote, ili mwishi kwa muda mrefu katika nchi mnayoishi ndani yake mkiwa wageni.’  Basi tunaendelea kuitii sauti ya Yehonadabu mwana wa Rekabu babu yetu kuhusu mambo yote aliyotuamuru, kwa kutokunywa kamwe divai—sisi, wake zetu, wana wetu, na mabinti wetu.  Nasi hatujengi nyumba za kuishi humo, wala hatuna mizabibu wala mashamba wala mbegu. 10  Tunaendelea kuishi katika mahema na kutii mambo yote ambayo babu yetu Yehonadabu* alituamuru. 11  Lakini Mfalme Nebukadneza* wa Babiloni alipoishambulia nchi,+ tukasema, ‘Njooni, tuingie ndani ya Yerusalemu ili kuepuka jeshi la Wakaldayo na la Wasiria, na sasa tunaishi Yerusalemu.’” 12  Na neno la Yehova likamjia Yeremia likisema: 13  “Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: ‘Nenda uwaambie watu wa Yuda na wakaaji wa Yerusalemu: “Je, hamkuendelea kuhimizwa myatii maneno yangu?”+ asema Yehova. 14  “Yehonadabu mwana wa Rekabu aliwaamuru wazao wake wasinywe divai, nao wamefuata maneno yake kwa kutokunywa divai mpaka leo hii, na hivyo wameitii amri ya babu yao.+ Hata hivyo, nimezungumza nanyi tena na tena,* lakini hamjatii.+ 15  Nami niliendelea kuwatuma kwenu watumishi wangu wote manabii, nikiwatuma tena na tena,*+ na kusema, ‘Tafadhali geukeni, kila mmoja wenu kutoka kwenye njia zenu za uovu,+ nanyi mfanye yaliyo sawa! Msifuate miungu mingine na kuiabudu. Ndipo mtakapoendelea kukaa katika nchi niliyowapa ninyi na mababu zenu.’+ Lakini hamkutega sikio lenu wala hamkunisikiliza. 16  Wazao wa Yehonadabu mwana wa Rekabu wamefuata agizo ambalo babu yao aliwapa,+ lakini watu hawa hawajanisikiliza.”’” 17  “Kwa hiyo Yehova, Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: ‘Ninawaletea watu wa Yuda na wakaaji wote wa Yerusalemu msiba wote niliowaonya kuuhusu,+ kwa maana nimezungumza nao, lakini walikataa kusikiliza, nami nikaendelea kuwaita, lakini walikataa kujibu.’”+ 18  Naye Yeremia akawaambia hivi watu wa nyumba ya Warekabu: “Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: ‘Kwa sababu mmetii agizo la babu yenu Yehonadabu nanyi mnaendelea kufuata maagizo yake yote, na kufanya sawasawa na alivyowaagiza, 19  Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: “Hatakosekana kamwe mzao wa Yehonadabu* mwana wa Rekabu atakayetumikia mbele zangu.”’”

Maelezo ya Chini

Au “vile vyumba.”
Tnn., “Yonadabu,” ufupisho wa jina Yehonadabu.
Tnn., “Yonadabu,” ufupisho wa jina Yehonadabu.
Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.
Tnn., “niliamka mapema na kuzungumza nanyi.”
Tnn., “nikiamka mapema na kuwatuma.”
Tnn., “Yonadabu,” ufupisho wa jina Yehonadabu.