Yeremia 37:1-21

  • Wakaldayo wataondoka kwa muda mfupi tu (1-10)

  • Yeremia afungwa gerezani (11-16)

  • Sedekia akutana na Yeremia (17-21)

    • Yeremia apewa mkate (21)

37  Na Mfalme Sedekia+ mwana wa Yosia akaanza kutawala baada ya Konia*+ mwana wa Yehoyakimu, kwa maana Mfalme Nebukadneza* wa Babiloni alikuwa amemweka kuwa mfalme katika nchi ya Yuda.+  Lakini yeye na watumishi wake na watu wa nchi hawakuyasikiliza maneno ya Yehova yaliyosemwa kupitia nabii Yeremia.  Na Mfalme Sedekia akamtuma Yehukali+ mwana wa Shelemia na Sefania+ mwana wa kuhani Maaseya kwa nabii Yeremia, akisema: “Tafadhali sali kwa ajili yetu kwa Yehova Mungu wetu.”  Yeremia alikuwa akitembea kwa uhuru miongoni mwa watu, kwa maana bado hakuwa ametiwa gerezani.+  Sasa jeshi la Farao lilikuwa limeondoka Misri,+ na Wakaldayo waliokuwa wakizingira Yerusalemu wakasikia habari kulihusu. Basi wakaondoka Yerusalemu.+  Kisha neno la Yehova likamjia nabii Yeremia likisema:  “Yehova Mungu wa Israeli anasema hivi: ‘Mnapaswa kumwambia hivi mfalme wa Yuda, aliyewatuma kwangu kutafuta habari: “Tazama! Jeshi la Farao linalokuja kuwasaidia litalazimika kurudi nchini kwao, Misri.+  Na Wakaldayo watarudi tena na kulishambulia jiji hili na kuliteka na kuliteketeza kwa moto.”+  Yehova anasema hivi: “Msijidanganye* kwa kusema, ‘Hakika Wakaldayo wataondoka na kutuacha,’ kwa sababu hawataondoka. 10  Hata kama mngeliangamiza jeshi lote la Wakaldayo wanaopigana nanyi na wabaki tu wale waliojeruhiwa, bado wangetoka katika mahema yao na kuliteketeza jiji hili kwa moto.”’”+ 11  Jeshi la Wakaldayo lilipoondoka Yerusalemu kwa sababu ya jeshi la Farao,+ 12  Yeremia akaondoka Yerusalemu na kwenda kwenye nchi ya Benjamini+ ili apate fungu lake huko miongoni mwa watu wake. 13  Lakini alipofika kwenye Lango la Benjamini, ofisa aliyesimamia walinzi, aliyeitwa Iriya mwana wa Shelemia mwana wa Hanania, akamkamata nabii Yeremia na kumwambia: “Unakimbia kwenda kwa Wakaldayo!” 14  Lakini Yeremia akasema: “Si kweli! Mimi sikimbii kwenda kwa Wakaldayo.” Lakini hakumsikiliza. Basi Iriya akamkamata Yeremia na kumpeleka kwa wakuu. 15  Wakuu wakamkasirikia vikali Yeremia,+ nao wakampiga na kumfunga*+ katika nyumba ya mwandishi Yehonathani, iliyokuwa imefanywa kuwa gereza. 16  Yeremia alitiwa katika gereza lililo chini ya ardhi,* kwenye vyumba vyenye ngome, naye akakaa humo kwa siku nyingi. 17  Kisha Mfalme Sedekia akaagiza aletwe, naye mfalme akaanza kumuuliza maswali kisiri katika nyumba yake.*+ Akamuuliza, “Je, kuna neno lolote kutoka kwa Yehova?” Yeremia akasema: “Lipo!” naye akaendelea kusema: “Utatiwa mikononi mwa mfalme wa Babiloni!”+ 18  Pia Yeremia akamwambia hivi Mfalme Sedekia: “Nimekutendea dhambi gani wewe na watumishi wako na watu hawa, hivi kwamba mmenifunga gerezani? 19  Wako wapi sasa manabii wenu waliowatabiria kwamba ‘Mfalme wa Babiloni hatakushambulia wewe wala nchi hii’?+ 20  Sasa sikiliza, tafadhali, ewe bwana wangu mfalme. Tafadhali, kubali ombi langu la kupata kibali. Usinirudishe katika nyumba ya mwandishi Yehonathani,+ la sivyo nitafia humo.”+ 21  Basi Mfalme Sedekia akaamuru Yeremia awekwe kifungoni katika Ua wa Walinzi,+ naye alipewa mkate wa mviringo kila siku kutoka kwenye barabara ya waokaji+ mpaka mikate yote ilipokwisha jijini.+ Na Yeremia akaendelea kukaa katika Ua wa Walinzi.

Maelezo ya Chini

Pia anaitwa Yehoyakini na Yekonia.
Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.
Au “msizidanganye nafsi zenu.”
Tnn., “wakamtia katika nyumba ya pingu.”
Tnn., “nyumba ya tangi.”
Au “jumba lake la mfalme.”