Yeremia 41:1-18

  • Ishmaeli amuua Gedalia (1-10)

  • Yohanani amfanya Ishmaeli akimbie (11-18)

41  Katika mwezi wa saba, Ishmaeli+ mwana wa Nethania mwana wa Elishama, aliyekuwa wa uzao wa kifalme* na mmoja kati ya wakuu wa mfalme, akaja pamoja na wanaume wengine kumi kwa Gedalia mwana wa Ahikamu huko Mispa.+ Walipokuwa wakila chakula pamoja huko Mispa,  Ishmaeli mwana wa Nethania na wale watu kumi waliokuwa pamoja naye wakasimama na kumpiga kwa upanga Gedalia mwana wa Ahikamu mwana wa Shafani. Kwa hiyo akamuua mtu ambaye mfalme wa Babiloni alikuwa amemweka kuwa msimamizi nchini.  Ishmaeli aliwaua pia Wayahudi wote waliokuwa pamoja na Gedalia huko Mispa, na pia wanajeshi Wakaldayo waliokuwa huko.  Siku ya pili baada ya Gedalia kuuawa, kabla mtu yeyote hajajua jambo hilo,  wakaja watu 80 kutoka Shekemu,+ kutoka Shilo,+ na kutoka Samaria.+ Ndevu zao zilikuwa zimenyolewa, mavazi yao yalikuwa yameraruka, walikuwa wamejikatakata,+ nao walikuwa na matoleo ya nafaka na uvumba+ mikononi mwao ili wavilete vitu hivyo katika nyumba ya Yehova.  Basi Ishmaeli mwana wa Nethania akatoka Mispa ili kuwapokea, naye alikuwa akitembea huku akilia. Alipokutana nao, akawaambia: “Njooni kwa Gedalia mwana wa Ahikamu.”  Lakini walipoingia jijini, Ishmaeli mwana wa Nethania na watu wake wakawachinja na kuwatupa ndani ya tangi la maji.  Lakini kulikuwa na watu kumi kati yao waliomwambia Ishmaeli: “Usituue, kwa maana shambani tuna maghala yaliyofichwa ya ngano, shayiri, mafuta, na asali.” Basi hakuwaua pamoja na ndugu zao.  Sasa Ishmaeli akazitupa maiti zote za watu aliowaua ndani ya tangi kubwa la maji, tangi ambalo Mfalme Asa alitengeneza kwa sababu ya Mfalme Baasha wa Israeli.+ Hilo ndilo tangi ambalo Ishmaeli mwana wa Nethania alilijaza maiti za watu waliouawa. 10  Ishmaeli akawachukua mateka watu wote waliobaki huko Mispa,+ kutia ndani mabinti wa mfalme na watu wote waliobaki Mispa, ambao Nebuzaradani mkuu wa walinzi alikuwa amewaweka chini ya ulinzi wa Gedalia+ mwana wa Ahikamu. Ishmaeli mwana wa Nethania aliwachukua mateka na kuvuka kwenda kwa Waamoni.+ 11  Yohanani+ mwana wa Karea na wakuu wote wa jeshi waliokuwa pamoja naye waliposikia uovu wote ambao Ishmaeli mwana wa Nethania alikuwa ametenda, 12  wakawachukua wanaume wote na kwenda kupigana na Ishmaeli mwana wa Nethania, nao wakamkuta kando ya maji mengi* kule Gibeoni. 13  Watu wote waliokuwa pamoja na Ishmaeli wakashangilia walipomwona Yohanani mwana wa Karea na wakuu wote wa jeshi waliokuwa pamoja naye. 14  Ndipo watu wote ambao Ishmaeli alikuwa amewachukua mateka kutoka Mispa+ wakageuka na kurudi pamoja na Yohanani mwana wa Karea. 15  Lakini Ishmaeli mwana wa Nethania pamoja na wanaume wanane kati ya watu wake wakamtoroka Yohanani, na kwenda kwa Waamoni. 16  Yohanani mwana wa Karea na wakuu wote wa jeshi waliokuwa pamoja naye wakawachukua watu waliobaki Mispa ambao walikuwa wamewaokoa kutoka kwa Ishmaeli mwana wa Nethania baada ya kumuua Gedalia+ mwana wa Ahikamu. Wakawaleta wanaume, wanajeshi, wanawake, watoto, na maofisa wa makao ya mfalme kutoka Gibeoni. 17  Basi wakaenda na kukaa mahali pa kulala pa Kimhamu kando ya Bethlehemu,+ wakikusudia kwenda Misri,+ 18  kwa sababu ya Wakaldayo. Kwa maana waliwaogopa, kwa sababu Ishmaeli mwana wa Nethania alikuwa amemuua Gedalia mwana wa Ahikamu, ambaye mfalme wa Babiloni alikuwa amemweka kuwa msimamizi wa nchi.+

Maelezo ya Chini

Tnn., “wa mbegu ya ufalme.”
Au labda, “dimbwi kubwa.”