Yeremia 42:1-22

  • Watu wamwomba Yeremia asali ili wapate mwongozo (1-6)

  • Yehova ajibu hivi: “Msiende Misri” (7-22)

42  Kisha wakuu wote wa jeshi, na Yohanani+ mwana wa Karea, Yezania mwana wa Hoshaya, na watu wote, kuanzia mdogo zaidi mpaka mkubwa zaidi, wakakaribia  na kumwambia nabii Yeremia: “Tafadhali, sikia ombi letu la kutaka kibali nawe usali kwa ajili yetu kwa Yehova Mungu wako, kwa ajili ya watu hawa wote waliobaki, kwa maana kati ya watu wengi, wachache ndio waliobaki,+ kama unavyoona.  Yehova Mungu wako na atuambie njia tunayopaswa kuifuata na jambo tunalopaswa kufanya.”  Nabii Yeremia akawajibu: “Nimewasikia, nami ninasali kwa Yehova Mungu wenu kulingana na ombi lenu; na kila neno ambalo Yehova atawajibu, nitawaambia. Sitawaficha neno lolote.”  Wakamjibu Yeremia: “Yehova na awe shahidi wa kweli na mwaminifu dhidi yetu ikiwa hatutafanya sawasawa kama anavyotuagiza Yehova Mungu wako kupitia wewe.  Iwe ni jambo jema au baya, tutaitii sauti ya Yehova Mungu wetu ambaye tunakutuma kwake, ili mambo yatuendee vema kwa sababu tunaitii sauti ya Yehova Mungu wetu.”  Baada ya siku kumi neno la Yehova likamjia Yeremia.  Basi akamwita Yohanani mwana wa Karea na wakuu wote wa jeshi waliokuwa pamoja naye na watu wote, kuanzia mdogo zaidi mpaka mkubwa zaidi.+  Akawaambia: “Yehova Mungu wa Israeli, ambaye mlinituma kwake ili kupeleka ombi lenu la kutaka kibali mbele zake, anasema hivi: 10  ‘Ikiwa kwa kweli mtakaa katika nchi hii, basi nitawajenga nami sitawabomoa, nitawapanda nami sitawang’oa, kwa maana nitaghairi* kuhusu msiba ambao nimewaletea.+ 11  Msimwogope mfalme wa Babiloni, mnayemwogopa.’+ “‘Msimwogope,’ asema Yehova, ‘kwa maana niko pamoja nanyi, ili kuwaokoa na kuwakomboa kutoka mikononi mwake. 12  Nami nitawaonyesha rehema,+ naye atawaonyesha rehema na kuwarudisha kwenye nchi yenu wenyewe. 13  “‘Lakini mkisema, “Hapana, hatutakaa katika nchi hii!” nanyi mkose kuitii sauti ya Yehova Mungu wenu 14  kwa kusema: “Hapana, badala yake tutaenda katika nchi ya Misri,+ ambako hatutaona vita wala kusikia sauti ya pembe wala kuwa na njaa kwa kukosa mkate; huko ndiko tutakakoishi,” 15  basi sikieni neno la Yehova, enyi watu wa Yuda mliobaki. Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: “Ikiwa mmeazimia kabisa kwenda Misri nanyi mwende kukaa huko,* 16  ndipo upanga uleule ambao mnaogopa utawafikia huko katika nchi ya Misri, na njaa ileile ambayo mnaogopa itawafuata huko Misri, nanyi mtafia huko.+ 17  Na watu wote walioazimia kwenda Misri ili kukaa huko watakufa kwa upanga, kwa njaa kali, na kwa ugonjwa hatari. Hakuna yeyote kati yao atakayeokoka au kuponyoka msiba nitakaowaletea.”’ 18  “Kwa maana Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: ‘Kama hasira yangu na ghadhabu yangu ilivyomwagwa juu ya wakaaji wa Yerusalemu,+ ndivyo ghadhabu yangu itakavyomwagwa juu yenu ikiwa mtaenda Misri, nanyi mtakuwa laana, kitu cha kutisha, matusi, na shutuma,+ nanyi hamtapaona tena kamwe mahali hapa.’ 19  “Yehova amewakataza, enyi watu wa Yuda mliobaki. Msiende Misri. Mnapaswa kujua kwa hakika kwamba nimewaonya leo, 20  kwamba kosa lenu litawagharimu uhai wenu.* Kwa maana mlinituma kwa Yehova Mungu wenu, mkisema, ‘Sali kwa ajili yetu kwa Yehova Mungu wetu, nawe utuambie kila jambo ambalo Yehova Mungu wetu anasema, nasi tutalifanya.’+ 21  Nami nimewaambia leo, lakini hamtaitii sauti ya Yehova Mungu wenu wala kufanya jambo lolote alilonituma niwaambie.+ 22  Kwa hiyo, jueni kwa hakika kwamba mtakufa kwa upanga, kwa njaa kali, na kwa ugonjwa hatari mahali mnapotamani kwenda kuishi.”+

Maelezo ya Chini

Au “nitahuzunika.”
Au “mwende kukaa huko kwa muda.”
Au “nafsi zenu.”