Yeremia 52:1-34

  • Sedekia aasi Babiloni (1-3)

  • Nebukadneza azingira Yerusalemu (4-11)

  • Kuharibiwa kwa jiji na hekalu (12-23)

  • Watu wapelekwa uhamishoni Babiloni (24-30)

  • Yehoyakini aachiliwa huru kutoka gerezani (31-34)

52  Sedekia+ alikuwa na umri wa miaka 21 alipoanza kutawala, naye alitawala kwa miaka 11 huko Yerusalemu. Mama yake aliitwa Hamutali+ binti ya Yeremia kutoka Libna.  Aliendelea kutenda maovu machoni pa Yehova, alitenda mambo yote ambayo Yehoyakimu alitenda.+  Mambo hayo yalitukia Yerusalemu na Yuda kwa sababu ya hasira ya Yehova, mpaka alipowatupa mbali kutoka machoni pake.+ Na Sedekia akamwasi mfalme wa Babiloni.+  Katika mwaka wa tisa wa utawala wa Sedekia, katika mwezi wa kumi, siku ya kumi ya mwezi huo, Mfalme Nebukadneza* wa Babiloni alikuja na jeshi lake lote kushambulia Yerusalemu. Walipiga kambi na kujenga ukuta kulizingira jiji hilo pande zote.+  Nao walilizingira jiji hilo mpaka mwaka wa 11 wa utawala wa Mfalme Sedekia.  Katika mwezi wa nne, siku ya tisa ya mwezi huo,+ njaa ilikuwa kali sana jijini, na watu waliokuwemo hawakuwa na chakula.+  Mwishowe sehemu ya ukuta wa jiji ikabomolewa, na wanajeshi wote wakakimbia kutoka jijini wakati wa usiku kupitia lango lililokuwa kati ya kuta mbili karibu na bustani ya mfalme, wakati Wakaldayo walipokuwa wakilizingira jiji; nao wakafuata njia inayoelekea Araba.+  Lakini jeshi la Wakaldayo likamfuatia mfalme, nalo likamfikia Sedekia+ katika jangwa tambarare la Yeriko, na wanajeshi wake wote wakatawanyika na kumwacha.  Kisha wakamkamata mfalme na kumpeleka mpaka kwa mfalme wa Babiloni kule Ribla katika nchi ya Hamathi, naye akamhukumu. 10  Na mfalme wa Babiloni akawachinja wana wa Sedekia huku Sedekia akitazama, na pia akawachinja wakuu wote wa Yuda huko Ribla. 11  Kisha mfalme wa Babiloni akampofusha macho Sedekia,+ akamfunga kwa pingu za shaba, akampeleka Babiloni, na kumfunga gerezani mpaka siku aliyokufa. 12  Katika mwezi wa tano, siku ya kumi ya mwezi huo, yaani, mwaka wa 19 wa utawala wa Mfalme Nebukadneza* wa Babiloni, Nebuzaradani mkuu wa walinzi, aliyekuwa mhudumu wa mfalme wa Babiloni, aliingia Yerusalemu.+ 13  Akateketeza kabisa nyumba ya Yehova,+ nyumba ya* mfalme, na nyumba zote za Yerusalemu; aliteketeza pia kila nyumba kubwa. 14  Na jeshi lote la Wakaldayo lililokuwa pamoja na mkuu wa walinzi lilibomoa kuta zilizozunguka Yerusalemu.+ 15  Nebuzaradani mkuu wa walinzi akawapeleka uhamishoni baadhi ya watu wa hali ya chini na watu wengine waliobaki jijini. Pia aliwachukua watu waliojisalimisha kwa mfalme wa Babiloni na pia mafundi stadi waliobaki.+ 16  Lakini Nebuzaradani mkuu wa walinzi aliwaacha baadhi ya watu maskini kabisa nchini ili watunze mashamba ya mizabibu na kufanya kazi za kulazimishwa.+ 17  Pia Wakaldayo walivunja vipandevipande nguzo za shaba+ za nyumba ya Yehova na magari+ na Bahari ya shaba,+ vitu vilivyokuwa katika nyumba ya Yehova, nao wakaipeleka shaba yote hiyo Babiloni.+ 18  Walichukua pia ndoo za kuondolea majivu, sepetu, mikasi ya kukatia tambi za taa, mabakuli,+ vikombe,+ na vyombo vyote vya shaba vilivyotumiwa katika utumishi wa hekaluni. 19  Mkuu wa walinzi alichukua mabeseni,+ vyetezo, mabakuli, ndoo za kuondolea majivu, vinara vya taa,+ vikombe, na mabakuli yaliyotengenezwa kwa dhahabu na fedha halisi.+ 20  Shaba yote iliyotumiwa kutengeneza zile nguzo mbili, wale ng’ombe dume 12 wa shaba+ waliokuwa chini ya ile Bahari, na yale magari ambayo Mfalme Sulemani alitengeneza kwa ajili ya nyumba ya Yehova, haingeweza kupimwa uzito. 21  Kuhusu nguzo, kila nguzo ilikuwa na kimo cha mikono 18,* na kamba ya kupimia yenye urefu wa mikono 12 ingeweza kuizunguka;+ unene wake ulikuwa upana wa vidole vinne,* na ndani ilikuwa wazi. 22  Na kifuniko cha nguzo kilikuwa cha shaba; na urefu wa kila kifuniko ulikuwa mikono mitano;+ na wavu pamoja na makomamanga yote yaliyozunguka kifuniko hicho yalitengenezwa kwa shaba. Nguzo ya pili ilifanana na nguzo ya kwanza, pia yale makomamanga. 23  Kulikuwa na makomamanga 96 kandokando; jumla, kulikuwa na makomamanga 100 kuzunguka ule wavu.+ 24  Mkuu wa walinzi alimchukua pia Seraya mkuu wa makuhani,+ Sefania+ kuhani wa pili, na walinzi watatu wa milango.+ 25  Pia alimchukua kutoka jijini ofisa mmoja wa makao ya mfalme aliyekuwa msimamizi wa wanajeshi, watu saba waliopatikana jijini walioshirikiana kwa ukaribu na mfalme, na pia mwandishi wa mkuu wa jeshi, aliyewaandikisha watu jeshini, na wanaume 60 kutoka miongoni mwa watu wa kawaida waliokuwa bado jijini. 26  Nebuzaradani mkuu wa walinzi aliwachukua na kuwapeleka kwa mfalme wa Babiloni kule Ribla. 27  Mfalme wa Babiloni aliwapiga na kuwaangamiza huko Ribla+ katika nchi ya Hamathi. Hivyo watu wa Yuda wakapelekwa uhamishoni kutoka katika nchi yao.+ 28  Hawa ndio watu ambao Nebukadneza* aliwapeleka uhamishoni: katika mwaka wa 7, Wayahudi 3,023.+ 29  Katika mwaka wa 18 wa utawala wa Nebukadneza,*+ watu 832 walichukuliwa kutoka Yerusalemu. 30  Katika mwaka wa 23 wa utawala wa Nebukadneza,* Nebuzaradani mkuu wa walinzi aliwapeleka Wayahudi uhamishoni, watu 745.+ Jumla ya watu 4,600 walipelekwa uhamishoni. 31  Kisha katika mwaka wa 37 tangu Mfalme Yehoyakini+ wa Yuda alipopelekwa uhamishoni, katika mwezi wa 12, siku ya 25 ya mwezi huo, Mfalme Evil-merodaki wa Babiloni, katika mwaka alioanza kutawala, alimwachilia huru Mfalme Yehoyakini wa Yuda na kumtoa gerezani.+ 32  Alizungumza naye kwa fadhili na kukikweza kiti chake cha ufalme juu zaidi kuliko viti vya wafalme wengine waliokuwa pamoja naye Babiloni. 33  Basi Yehoyakini akavua mavazi yake ya gerezani, na sikuzote za maisha yake alikuwa akila kwenye meza ya mfalme. 34  Naye alipewa chakula kwa ukawaida kutoka kwa mfalme wa Babiloni, siku baada ya siku, mpaka siku aliyokufa, siku zote za maisha yake.

Maelezo ya Chini

Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.
Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.
Au “jumba la.”
Mkono mmoja ulilingana na sentimita 44.5 (inchi 17.5). Angalia Nyongeza B14.
Upana wa kidole ulilingana na sentimita 1.85 (inchi 0.73). Angalia Nyongeza B14.
Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.
Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.
Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.