Yeremia 7:1-34

  • Tumaini la uwongo katika hekalu la Yehova (1-11)

  • Hekalu litakuwa kama Shilo (12-15)

  • Ibada ya kidesturi yashutumiwa (16-34)

    • “Malkia wa Mbinguni” aabudiwa (18)

    • Kutoa watoto dhabihu huko Hinomu (31)

7  Hili ndilo neno lililomjia Yeremia kutoka kwa Yehova, likisema:  “Simama katika lango la nyumba ya Yehova nawe utangaze hapo ujumbe huu, ‘Sikieni neno la Yehova ninyi watu wote wa Yuda mnaoingia katika malango haya ili kumwinamia Yehova.  Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: “Rekebisheni njia zenu na matendo yenu, nami nitawaruhusu mwendelee kukaa mahali hapa.+  Msiyatumaini maneno ya udanganyifu na kusema, ‘Hili ni* hekalu la Yehova, hekalu la Yehova, hekalu la Yehova!’+  Mkirekebisha kikweli njia zenu na matendo yenu; mkitekeleza haki kikweli kati ya mtu na jirani yake;+  msipowakandamiza wakaaji wageni, mayatima,* na wajane;+ msipomwaga damu isiyo na hatia mahali hapa; na msipoifuata miungu mingine na kujiletea madhara;+  basi nitawaruhusu mwendelee kukaa mahali hapa, katika nchi niliyowapa mababu zenu daima.”’”*  “Lakini mnayatumaini maneno ya udanganyifu+—hayatawaletea faida yoyote.  Je, mnaweza kuiba,+ kuua, kufanya uzinzi, kuapa kwa uwongo,+ kumtolea dhabihu* Baali,+ na kuifuata miungu mingine ambayo hamkuijua, 10  kisha mje na kusimama mbele zangu katika nyumba hii inayoitwa kwa jina langu na kusema, ‘Tutaokolewa,’ ilhali mnafanya mambo hayo yote yanayochukiza? 11  Je, nyumba hii inayoitwa kwa jina langu imekuwa pango la wanyang’anyi machoni penu?+ Nimejionea jambo hilo,” asema Yehova. 12  “‘Hata hivyo, sasa nendeni mahali pangu huko Shilo,+ ambapo mwanzoni nilifanya jina langu likae,+ na kuona nilivyopafanya kwa sababu ya uovu wa watu wangu Waisraeli.+ 13  Lakini mliendelea kufanya mambo hayo yote,’ asema Yehova, ‘na ingawa nilizungumza nanyi tena na tena,* hamkusikiliza.+ Niliendelea kuwaita, lakini hamkujibu.+ 14  Ndivyo nitakavyoitendea nyumba inayoitwa kwa jina langu,+ ambayo mnaitumaini,+ na mahali hapa ambapo niliwapa ninyi na mababu zenu, kama nilivyoitendea Shilo.+ 15  Nitawatupa kutoka mbele za macho yangu, kama nilivyowatupa ndugu zenu wote, wazao wote wa Efraimu.’+ 16  “Lakini wewe, usisali kwa ajili ya watu hawa. Usipaze kilio wala kusali wala kunisihi kwa ajili yao,+ kwa maana sitakusikiliza.+ 17  Je, huoni mambo wanayofanya katika majiji ya Yuda na kwenye barabara za Yerusalemu? 18  Wana wanakusanya kuni, akina baba wanawasha moto, na wake wanakanda unga ili kumwokea Malkia wa Mbinguni*+ keki za dhabihu, nao wanaimiminia miungu mingine matoleo ya kinywaji ili wanikasirishe.+ 19  ‘Lakini je, ni mimi wanayeniumiza?’* auliza Yehova. ‘Je, hawajiumizi wao wenyewe, kwa aibu yao wenyewe?’+ 20  Kwa hiyo Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema, ‘Tazama! Hasira yangu na ghadhabu yangu zitamwagwa mahali hapa,+ juu ya mwanadamu na mnyama, juu ya miti ya shambani na mazao ya ardhi; itateketeza na haitazimwa.’+ 21  “Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema, ‘Endeleeni, ongezeni dhabihu zenu nzima za kuteketezwa kwenye dhabihu zenu nyingine, na mle nyama hizo ninyi wenyewe.+ 22  Kwa maana siku niliyowatoa mababu zenu nchini Misri, sikuwaambia wala kuwaamuru kuhusu dhabihu nzima za kuteketezwa na dhabihu nyingine.+ 23  Lakini niliwaamuru hivi: “Tiini sauti yangu, nami nitakuwa Mungu wenu, nanyi mtakuwa watu wangu.+ Ni lazima mtembee katika njia yote ninayowaamuru, ili mambo yawaendee vema.”’+ 24  Lakini hawakusikiliza wala kutega sikio lao;+ badala yake walitembea katika mipango yao* wenyewe, wakifuata kwa ukaidi moyo wao mwovu,+ nao wakarudi nyuma, badala ya kwenda mbele, 25  tangu siku ambayo mababu zenu walitoka nchini Misri mpaka leo hii.+ Basi nikaendelea kuwatuma kwenu watumishi wangu wote manabii, nilikuwa nikiwatuma kila siku, tena na tena.*+ 26  Lakini walikataa kunisikiliza, nao hawakutega sikio lao.+ Badala yake, walikuwa wakaidi,* nao walitenda mambo mabaya zaidi kuliko mababu zao! 27  “Utawaambia maneno haya yote,+ lakini hawatakusikiliza; utawaita, lakini hawatakujibu. 28  Nawe utawaambia, ‘Hili ndilo taifa ambalo halikuitii sauti ya Yehova Mungu wao, nao walikataa kukubali nidhamu. Uaminifu umetoweka na hata hautajwi miongoni mwao.’*+ 29  “Nyoa nywele zako ambazo hazijanyolewa,* nawe uzitupe, na uimbe wimbo wa huzuni* juu ya vilima vitupu, kwa maana Yehova amekikataa na atakiacha kizazi hiki ambacho kimemkasirisha. 30  ‘Kwa maana watu wa Yuda wametenda maovu machoni pangu,’ asema Yehova. ‘Wameziweka sanamu zao zinazochukiza katika nyumba ambayo imeitwa kwa jina langu, ili kuitia unajisi.+ 31  Wamejenga mahali pa juu pa Tofethi, palipo katika Bonde la Mwana wa Hinomu,*+ ili kuwateketeza motoni wana wao na mabinti wao,+ jambo ambalo sikuamuru na ambalo hata halijawahi kamwe kuingia moyoni mwangu.’*+ 32  “‘Kwa hiyo tazama! siku zinakuja,’ asema Yehova, ‘wakati ambapo bonde hilo halitaitwa tena Tofethi au Bonde la Mwana wa Hinomu* bali Bonde la Mauaji. Watawazika wafu katika Tofethi hivi kwamba hakutakuwa na nafasi zaidi.+ 33  Na maiti za watu hawa zitakuwa chakula cha ndege wa angani na cha wanyama wa duniani, na hakuna mtu atakayewafukuza.+ 34  Nitaikomesha sauti ya furaha na sauti ya shangwe, sauti ya bwana harusi na sauti ya bibi harusi,+ katika majiji ya Yuda na katika barabara za Yerusalemu, kwa maana nchi itakuwa magofu.’”+

Maelezo ya Chini

Tnn., “Haya ni,” yaani majengo yote ya hekalu.
Au “watoto wasio na baba.”
Au “tangu milele mpaka milele.”
Au “moshi wa dhabihu.”
Tnn., “niliamka mapema na kuzungumza.”
Jina la mungu wa kike aliyeabudiwa na Waisraeli waasi imani; huenda ni mungu wa kike wa uzazi.
Au “wanayenikasirisha; wanayenichokoza.”
Au “ushauri wao.”
Tnn., “kila siku niliamka mapema na kuwatuma.”
Tnn., “waliifanya shingo yao iwe ngumu.”
Tnn., “umekatwa kutoka kinywani mwao.”
Au “ambazo zimewekwa wakfu.”
Au “wimbo wa maombolezo.”
Angalia Kamusi, “Gehena.”
Au “sijawahi kamwe kulifikiria.”
Angalia Kamusi, “Gehena.”