Kulingana na Yohana 5:1-47

  • Mwanamume mgonjwa aponywa Bethzatha (1-18)

  • Yesu apewa mamlaka na baba yake (19-24)

  • Wafu watasikia sauti ya Yesu (25-30)

  • Ushahidi kumhusu Yesu (31-47)

5  Baada ya hayo kulikuwa na sherehe+ ya Wayahudi, na Yesu akapanda kwenda Yerusalemu.  Huko Yerusalemu kwenye Lango la Kondoo+ kulikuwa na dimbwi lililoitwa kwa Kiebrania Bethzatha, lenye safu tano za nguzo.  Wagonjwa wengi, vipofu, vilema, na wenye viungo vilivyopooza walikuwa wamelala hapo. 4 * ——  Lakini hapo palikuwa na mtu fulani aliyekuwa mgonjwa kwa miaka 38.  Yesu alipomwona mtu huyo amelala hapo, na akijua kwamba alikuwa mgonjwa kwa muda mrefu, akamuuliza: “Je, unataka kupona?”+  Mgonjwa huyo akamjibu: “Bwana, sina mtu wa kuniweka ndani ya dimbwi maji yanapotibuliwa, lakini ninapotaka kuingia, mtu mwingine huingia kabla yangu.”  Yesu akamwambia: “Simama! Chukua mkeka wako,* utembee.”+  Mtu huyo akapona mara moja, akabeba mkeka wake* na kuanza kutembea. Hiyo ilikuwa siku ya Sabato. 10  Basi Wayahudi wakaanza kumwambia mtu huyo aliyeponywa: “Ni Sabato, hupaswi kubeba mkeka.”*+ 11  Lakini akawajibu: “Yule aliyeniponya aliniambia, ‘Beba mkeka* wako utembee.’” 12  Wakamuuliza: “Ni nani huyo aliyekuambia, ‘Beba mkeka wako utembee’?” 13  Lakini mwanamume huyo aliyeponywa hakujua ni nani, kwa maana Yesu alikuwa ameingia katika umati uliokuwa hapo. 14  Baadaye, Yesu alimkuta hekaluni akamwambia: “Ona, sasa umepona. Usifanye dhambi tena, ili usipatwe na jambo baya zaidi.” 15  Yule mtu akaenda na kuwaambia Wayahudi kwamba Yesu ndiye aliyemponya. 16  Kwa hiyo Wayahudi walikuwa wakimtesa Yesu, kwa sababu alikuwa akifanya mambo hayo siku ya Sabato. 17  Lakini akawajibu: “Baba yangu anaendelea kufanya kazi mpaka sasa, nami ninaendelea kufanya kazi.”+ 18  Basi Wayahudi wakazidi kutafuta njia ya kumuua, kwa sababu hakuwa tu akivunja Sabato bali pia alikuwa akimwita Mungu Baba yake,+ akijifanya kuwa sawa na Mungu.+ 19  Kwa hiyo, Yesu akawajibu: “Kwa kweli ninawaambia, Mwana hawezi kufanya hata jambo moja kwa uamuzi wake mwenyewe, ila tu lile analomwona Baba akifanya.+ Kwa maana mambo yote ambayo Baba hufanya, vivyo hivyo Mwana hufanya mambo hayo. 20  Kwa maana Baba anampenda Mwana+ na humwonyesha mambo yote anayofanya, naye atamwonyesha kazi kubwa kuliko hizi, ili ninyi mshangae.+ 21  Kwa maana kama vile Baba anavyowafufua wafu na kuwafanya kuwa hai,+ ndivyo Mwana pia anavyowafanya kuwa hai wale anaotaka.+ 22  Kwa maana Baba hamhukumu mtu yeyote kamwe, bali amemkabidhi Mwana kazi yote ya kuhukumu,+ 23  ili wote wamheshimu Mwana kama vile wanavyomheshimu Baba. Yeyote ambaye hamheshimu Mwana hamheshimu Baba aliyemtuma.+ 24  Kwa kweli ninawaambia, yeyote ambaye husikia neno langu na kumwamini Yule aliyenituma ana uzima wa milele,+ naye hahukumiwi bali amevuka kutoka katika kifo na kuingia kwenye uzima.+ 25  “Kwa kweli ninawaambia, saa inakuja, nayo imefika, ambapo wafu wataisikia sauti ya Mwana wa Mungu, na wale ambao wamesikiliza wataishi. 26  Kwa maana kama vile Baba alivyo na uzima ndani yake mwenyewe,*+ ndivyo pia amemruhusu Mwana awe na uzima ndani yake mwenyewe.+ 27  Naye amempa mamlaka ya kuhukumu,+ kwa sababu yeye ndiye Mwana wa binadamu.+ 28  Msishangazwe na jambo hili, kwa maana saa inakuja ambayo wote walio katika makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake+ 29  na kutoka, wale waliotenda mema kwenye ufufuo wa uzima, na wale waliozoea kutenda maovu kwenye ufufuo wa hukumu.+ 30  Siwezi kufanya jambo lolote kwa uamuzi wangu mwenyewe. Kama vile ninavyosikia, ndivyo ninavyohukumu; na hukumu yangu ni ya uadilifu+ kwa sababu sitafuti mapenzi yangu mwenyewe, bali mapenzi ya yule aliyenituma.+ 31  “Ikiwa mimi peke yangu ndiye ninayetoa ushahidi juu yangu mwenyewe, ushahidi wangu si wa kweli.+ 32  Kuna mwingine anayetoa ushahidi kunihusu, nami ninajua ushahidi anaotoa kunihusu ni wa kweli.+ 33  Mmewatuma watu kwa Yohana, naye ametoa ushahidi kuhusu kweli.+ 34  Hata hivyo, sikubali ushahidi wa mwanadamu, bali ninasema mambo haya ili mwokolewe. 35  Mtu huyo alikuwa taa inayowaka na kung’aa, na kwa wakati mfupi mlikuwa tayari kufurahia sana mwangaza wake.+ 36  Lakini nina ushahidi mkubwa kuliko wa Yohana, kwa maana kazi ambazo Baba yangu alinipa nitimize, yaani, kazi hizi ninazofanya zinatoa ushahidi kwamba Baba alinituma.+ 37  Naye Baba aliyenituma ametoa ushahidi kunihusu.+ Ninyi hamjasikia sauti yake wakati wowote wala kuona umbo lake,+ 38  nanyi hamna neno lake ndani yenu, kwa sababu hammwamini yule ambaye alimtuma. 39  “Mnayachunguza Maandiko+ mkifikiri mtapata uzima wa milele kupitia Maandiko hayo; nayo* ndiyo yanayotoa ushahidi kunihusu.+ 40  Hata hivyo, hamtaki kuja kwangu+ ili mpate uzima. 41  Mimi sikubali utukufu kutoka kwa wanadamu, 42  lakini ninajua kwamba hamna upendo wa Mungu ndani yenu. 43  Nimekuja katika jina la Baba yangu, lakini hamnikubali. Ikiwa mtu mwingine angekuja kwa jina lake mwenyewe, mngemkubali. 44  Mnawezaje kuniamini, huku mkipeana utukufu ninyi wenyewe lakini hamtafuti utukufu unaotoka kwa Mungu wa pekee?+ 45  Msifikiri kwamba nitawashtaki kwa Baba. Kuna yule anayewashtaki, Musa,+ ambaye mmeweka tumaini lenu kwake. 46  Kwa kweli, ikiwa mngemwamini Musa mngeniamini pia, kwa sababu aliandika kunihusu.+ 47  Lakini ikiwa hamwamini mambo aliyoandika, mnawezaje kuamini mambo ninayosema?”

Maelezo ya Chini

Au “kitanda chako.”
Au “kitanda chake.”
Au “kitanda.”
Au “kitanda.”
Au “alivyo na zawadi ya uhai ndani yake mwenyewe.”
Yaani, Maandiko.