Kulingana na Yohana 7:1-52

  • Yesu akiwa kwenye Sherehe ya Vibanda (1-13)

  • Yesu afundisha kwenye sherehe (14-24)

  • Maoni mbalimbali kumhusu Yesu (25-52)

7  Baada ya mambo hayo Yesu aliendelea kusafiri* huko Galilaya, kwa maana hakutaka kwenda Yudea kwa sababu Wayahudi walitaka kumuua.+  Hata hivyo, Sherehe ya Vibanda ya Wayahudi,+ ilikuwa imekaribia.  Basi ndugu zake+ wakamwambia: “Ondoka hapa uende Yudea, ili wanafunzi wako pia waone kazi unazofanya.  Kwa maana mtu yeyote anayetaka kujulikana hadharani hafanyi jambo lolote kisiri. Ikiwa unafanya mambo haya jionyeshe kwa ulimwengu.”  Kwa kweli, ndugu zake hawakuwa wakimwamini.*+  Basi Yesu akawaambia: “Bado wakati wangu haujafika,+ lakini wakati wenu upo sikuzote.  Ulimwengu hauna sababu ya kuwachukia ninyi, lakini unanichukia mimi kwa sababu ninatoa ushahidi kuuhusu kwamba matendo yake ni maovu.+  Ninyi nendeni kwenye sherehe; mimi bado siendi kwenye sherehe hiyo, kwa sababu bado wakati wangu haujafika kikamili.”+  Basi baada ya kuwaambia mambo hayo, akabaki Galilaya. 10  Lakini ndugu zake walipopanda kwenda kwenye sherehe, yeye pia alienda, lakini kisiri. 11  Basi Wayahudi wakaanza kumtafuta kwenye sherehe wakiuliza: “Yuko wapi yule mtu?” 12  Kulikuwa na minong’ono mingi kumhusu katika umati. Baadhi yao walisema: “Yeye ni mtu mwema.” Nao wengine wakasema: “Hapana. Anaupotosha umati.”+ 13  Bila shaka, hakuna mtu aliyesema waziwazi kumhusu kwa sababu waliwaogopa Wayahudi.+ 14  Sherehe ilipofika katikati, Yesu akapanda kuingia hekaluni na kuanza kufundisha. 15  Wayahudi wakashangaa na kuulizana: “Mtu huyu alipataje ujuzi wa Maandiko,*+ ingawa hajafundishwa shuleni?”*+ 16  Naye Yesu akawaambia: “Mambo ninayofundisha si yangu, bali ni ya yule aliyenituma.+ 17  Mtu yeyote anayetamani kufanya mapenzi ya Mungu, atajua kama mafundisho haya yanatoka kwa Mungu+ au ninasema mambo niliyojitungia. 18  Mtu anayesema mambo aliyojitungia anajitafutia utukufu; lakini mtu anayetafuta utukufu wa yule aliyemtuma,+ huyo ni wa kweli, na hana ukosefu wowote wa uadilifu ndani yake. 19  Musa aliwapa Sheria,+ sivyo? Lakini hakuna yeyote kati yenu anayetii Sheria. Kwa nini mnataka kuniua?”+ 20  Umati ukamwambia: “Wewe una roho mwovu. Ni nani anayetaka kukuua?” 21  Yesu akawajibu: “Nilifanya jambo moja tu, nyote mkashangaa. 22  Kwa hiyo Musa aliwapa tohara+—si kwamba inatoka kwa Musa, bali inatoka kwa mababu+—nanyi mnamtahiri mtu siku ya sabato. 23  Ikiwa mtu hutahiriwa siku ya sabato ili Sheria ya Musa isivunjwe, mbona mnanikasirikia sana kwa sababu nilimponya mtu siku ya sabato+ naye akapona kabisa? 24  Acheni kuhukumu kwa kutazama sura ya nje tu, bali hukumuni kwa uadilifu.”+ 25  Kisha baadhi ya wakaaji wa Yerusalemu wakaanza kusema: “Huyu ndiye mtu wanayetaka kumuua, sivyo?+ 26  Na bado oneni! anazungumza hadharani, na hawamwambii chochote. Je, kweli watawala wametambua kwa hakika kwamba huyu ndiye Kristo? 27  Hata hivyo, tunajua mtu huyu ametoka wapi;+ lakini Kristo atakapokuja, hakuna mtu atakayejua alikotoka.” 28  Kisha Yesu alipokuwa akifundisha hekaluni akasema kwa sauti kubwa: “Ninyi mnanijua na pia mnajua nilikotoka. Nami sikuja kwa uamuzi wangu mwenyewe,+ lakini Yule aliyenituma ni halisi, nanyi hammjui.+ 29  Mimi ninamjua,+ kwa sababu mimi ni mwakilishi kutoka kwake, naye Ndiye aliyenituma.” 30  Basi wakaanza kutafuta njia ya kumkamata,+ lakini hakuna aliyeweza kumkamata, kwa sababu saa yake haikuwa imefika.+ 31  Hata hivyo, wengi katika umati walimwamini,+ nao wakaanza kusema: “Kristo atakapokuja, je, atafanya ishara nyingi kuliko alizofanya mtu huyu?” 32  Mafarisayo walisikia umati ukinong’onezana mambo hayo kumhusu, nao wakuu wa makuhani na Mafarisayo wakawatuma maofisa wamkamate. 33  Kisha Yesu akasema: “Nitakuwa pamoja nanyi kwa muda mfupi kisha nitarudi kwa Yule aliyenituma.+ 34  Mtanitafuta lakini hamtanipata, na mahali nilipo hamwezi kuja.”+ 35  Kwa hiyo, Wayahudi wakaanza kuulizana: “Mtu huyu anakusudia kwenda wapi, hivi kwamba hatutampata? Je, anakusudia kwenda kwa Wayahudi waliotawanyika kati ya Wagiriki ili awafundishe Wagiriki? 36  Anamaanisha nini anaposema, ‘Mtanitafuta, lakini hamtanipata, na mahali nilipo hamwezi kuja’?” 37  Katika siku ya mwisho, siku kuu ya sherehe,+ Yesu alisimama na kusema kwa sauti kubwa: “Ikiwa yeyote ana kiu, na aje kwangu anywe maji.+ 38  Yeyote anayeniamini, kama andiko linavyosema: ‘Vijito vya maji ya uzima vitatiririka kutoka ndani yake.’”+ 39  Hata hivyo, alikuwa akizungumza kuhusu roho, ambayo wale waliomwamini walikuwa karibu kupokea; kwa maana kufikia wakati huo hawakuwa wamepokea roho,+ kwa sababu bado Yesu hakuwa ametukuzwa.+ 40  Baadhi ya watu katika umati waliosikia maneno hayo wakaanza kusema: “Kwa kweli huyu ndiye Nabii.”+ 41  Wengine walikuwa wakisema: “Huyu ndiye Kristo.”+ Lakini wengine wakasema: “Kristo hatakuja kutoka Galilaya, sivyo?+ 42  Je, andiko halisemi kwamba Kristo atatoka katika uzao wa Daudi+ na atatoka Bethlehemu,+ kijiji alichoishi Daudi?”+ 43  Basi kukatokea mgawanyiko kumhusu katika umati. 44  Hata hivyo, baadhi yao walitaka kumkamata, lakini hakuna yeyote aliyemkamata. 45  Kisha wale maofisa wakarudi kwa wakuu wa makuhani na Mafarisayo. Wakawauliza: “Kwa nini hamkumleta?” 46  Maofisa wakajibu: “Hakuna mtu mwingine yeyote ambaye amewahi kuzungumza hivyo.”+ 47  Nao Mafarisayo wakawauliza: “Je, ninyi pia mmepotoshwa? 48  Je, kuna yeyote kati ya watawala au Mafarisayo ambaye amemwamini?+ 49  Lakini umati huu usiojua Sheria ni watu waliolaaniwa.” 50  Nikodemo, aliyekuwa amemwendea hapo mwanzoni, na ambaye pia alikuwa mmoja wao akawaambia: 51  “Kulingana na Sheria yetu, kabla ya kumhukumu mtu, tunapaswa kumsikiliza ili tujue anachofanya, sivyo?”+ 52  Wakamjibu: “Je, wewe pia umetoka Galilaya? Chunguza uone kwamba hakuna nabii atakayeinuliwa kutoka Galilaya.”*

Maelezo ya Chini

Au “kutembea.”
Au “wakionyesha kwamba wanamwamini.”
Tnn., “maandishi.”
Yaani, shule za kirabi.
Baadhi ya hati za kale zinazoaminika hazina mstari wa 53 hadi sura ya 8 mstari wa 11.