Kulingana na Yohana 9:1-41

  • Yesu amponya mwanamume aliyezaliwa kipofu (1-12)

  • Mafarisayo wamuuliza maswali mwanamume aliyeponywa (13-34)

  • Upofu wa Mafarisayo (35-41)

9  Yesu alipokuwa akipita alimwona mtu aliyekuwa kipofu tangu kuzaliwa.  Kisha wanafunzi wake wakamuuliza: “Rabi,+ ni nani aliyetenda dhambi, ni mtu huyu au ni wazazi wake, hivi kwamba akazaliwa kipofu?”  Yesu akajibu: “Mtu huyu hakutenda dhambi wala wazazi wake, bali ilikuwa hivyo ili kazi za Mungu zifunuliwe katika kisa chake.+  Lazima tufanye kazi za Yule aliyenituma kukiwa bado mchana;+ usiku unakuja ambapo hakuna mtu atakayeweza kufanya kazi.  Maadamu nimo ulimwenguni, mimi ndiye nuru ya ulimwengu.”+  Baada ya kusema mambo hayo, akatema mate chini akafanyiza tope kwa mate, na kumpaka mtu huyo kwenye macho+  na kumwambia: “Nenda ukanawe katika dimbwi la Siloamu” (linalotafsiriwa kuwa “Aliyetumwa”). Naye akaenda na kunawa, akarudi akiwa anaona.+  Basi majirani na watu waliokuwa wakimwona akiombaomba wakaanza kuulizana: “Je, huyu si yule mtu aliyekuwa akiketi akiombaomba?”  Baadhi yao walikuwa wakisema: “Ni yeye.” Wengine walikuwa wakisema: “Hapana, lakini anafanana naye.” Yule mtu akaendelea kusema: “Ni mimi.” 10  Basi wakamuuliza: “Macho yako yalifunguliwaje?” 11  Akajibu: “Mtu anayeitwa Yesu alifanyiza tope akanipaka kwenye macho kisha akaniambia, ‘Nenda mpaka Siloamu ukanawe.’+ Basi nikaenda, nikanawa, nikaanza kuona.” 12  Ndipo wakamuuliza: “Yuko wapi mtu huyo?” Akasema: “Sijui.” 13  Wakampeleka kwa Mafarisayo mtu huyo ambaye zamani alikuwa kipofu. 14  Ikawa kwamba siku ambayo Yesu alifanyiza tope na kuyafungua macho ya mtu huyo+ ilikuwa Sabato.+ 15  Basi wakati huo Mafarisayo wakaanza kumuuliza jinsi alivyoanza kuona. Akawaambia: “Alinipaka tope kwenye macho yangu, nami nikanawa, sasa ninaona.” 16  Kisha baadhi ya Mafarisayo wakaanza kusema: “Mtu huyo hatoki kwa Mungu, kwa sababu hashiki Sabato.”+ Wengine wakasema: “Mtenda dhambi anawezaje kufanya ishara kama hizo?”+ Basi kukawa na mgawanyiko kati yao.+ 17  Wakamuuliza tena yule mtu aliyekuwa kipofu: “Unasemaje kumhusu kwa kuwa wewe ndiye uliyefunguliwa macho?” Akajibu: “Yeye ni nabii.” 18  Hata hivyo, Wayahudi hawakuamini kwamba alikuwa kipofu na sasa alikuwa anaona. Basi wakawaita wazazi wake 19  wakawauliza: “Je, huyu ni mwana wenu ambaye mnasema alizaliwa kipofu? Basi, imekuwaje kwamba sasa anaona?” 20  Wazazi wake wakajibu: “Tunajua kwamba huyu ni mwana wetu na alizaliwa akiwa kipofu. 21  Lakini hatujui jinsi alivyoanza kuona, wala hatujui mtu aliyemfungua macho. Muulizeni. Yeye ni mtu mzima. Anaweza kujieleza.” 22  Wazazi wake walisema hivyo kwa sababu waliogopa Wayahudi,+ kwa maana tayari Wayahudi walikuwa wamekubaliana kwamba mtu yeyote ambaye angemkiri kuwa ndiye Kristo, angefukuzwa katika sinagogi.+ 23  Ndiyo maana wazazi wake walisema: “Yeye ni mtu mzima, muulizeni.” 24  Basi wakamwita mara ya pili yule mtu aliyekuwa kipofu na kumwambia: “Mpe Mungu utukufu; tunajua mtu huyu ni mtenda dhambi.” 25  Akawajibu: “Kama yeye ni mtenda dhambi mimi sijui. Ninachojua ni kwamba nilikuwa kipofu, lakini sasa ninaona.” 26  Kisha wakamuuliza: “Alikufanyia nini? Aliyafunguaje macho yako?” 27  Akawajibu: “Tayari nimewaambia, lakini hamkusikiliza. Kwa nini mnataka kusikia tena? Je, ninyi pia mnataka kuwa wanafunzi wake?” 28  Ndipo wakamwambia kwa dharau: “Wewe ni mwanafunzi wa mtu huyo, lakini sisi ni wanafunzi wa Musa. 29  Tunajua kwamba Mungu alizungumza na Musa; lakini mtu huyu, hatujui alikotoka.” 30  Yule mtu akawajibu: “Kwa kweli inashangaza kwamba hamjui alikotoka, ingawa ndiye aliyefungua macho yangu. 31  Tunajua kwamba Mungu hawasikilizi watenda dhambi,+ lakini humsikiliza mtu yeyote anayemwogopa na kufanya mapenzi yake.+ 32  Tangu zamani haijasikiwa kamwe mtu yeyote ameyafungua macho ya mtu aliyezaliwa kipofu. 33  Kama mtu huyu hakutoka kwa Mungu, hangeweza kufanya lolote.”+ 34  Wakamwambia: “Wewe ulizaliwa katika dhambi, na bado unajaribu kutufundisha?” Kwa hiyo, wakamfukuza!+ 35  Yesu akasikia kwamba walikuwa wamemfukuza mtu huyo. Basi alipompata akamuuliza: “Je, unamwamini Mwana wa binadamu?” 36  Yule mtu akauliza: “Bwana, huyo ni nani, niambie ili nimwamini?” 37  Yesu akamwambia: “Tayari umemwona, na kwa kweli, yeye ndiye anayezungumza nawe.”⁠ 38  Akasema: “Ninamwamini, Bwana.” Naye akamsujudia.* 39  Kisha Yesu akasema: “Nilikuja ulimwenguni kwa ajili ya hukumu hii, ili wale wasioona waweze kuona+ na wale wanaoona wawe vipofu.”+ 40  Baadhi ya Mafarisayo waliokuwa pamoja naye waliposikia mambo hayo wakamuuliza: “Je, sisi pia ni vipofu?” 41  Yesu akawaambia: “Kama mngekuwa vipofu, hamngekuwa na dhambi. Lakini sasa mnasema, ‘Tunaona.’ Dhambi yenu inabaki.”+

Maelezo ya Chini

Au “akamwinamia.”