Yona 4:1-11

  • Yona akasirika, atamani kufa (1-3)

  • Yehova amfundisha Yona kuhusu rehema (4-11)

    • “Je, una sababu nzuri ya kuwaka hasira?” (4)

    • Somo la mmung’unye (6-10)

4  Lakini jambo hilo lilimchukiza sana Yona, akakasirika sana.  Basi akasali hivi kwa Yehova: “Ee Yehova, je, sikujua utafanya jambo hili nilipokuwa katika nchi yangu? Ndiyo sababu tangu awali nilijaribu kukimbilia Tarshishi;+ kwa maana nilijua kwamba wewe ni Mungu mwenye huruma* na rehema, hukasiriki upesi, una upendo mwingi mshikamanifu,+ na unahuzunishwa na msiba.  Sasa, Ee Yehova, nakusihi uniue, kwa maana afadhali nife badala ya kuishi.”+  Yehova akamuuliza: “Je, una sababu nzuri ya kuwaka hasira?”  Ndipo Yona akatoka jijini, akaketi chini upande wa mashariki wa jiji. Akajenga kibanda hapo na kuketi kivulini ili aone jambo litakalolipata jiji hilo.+  Kisha Yehova Mungu akaotesha mmung’unye* ili Yona apate kivuli kwa ajili ya kichwa chake na ili kupunguza taabu yake. Basi Yona akaufurahia sana mmung’unye huo.  Lakini siku iliyofuata, wakati wa mapambazuko, Mungu wa kweli akamwamuru kiwavi aushambulie mmung’unye huo, nao ukanyauka.  Joto la jua lilipoanza kuongezeka, Mungu akaleta pia upepo wa mashariki wenye joto kali, na jua likamchoma Yona kichwani, karibu azimie. Akaendelea kuomba afe,* na kuendelea kusema: “Afadhali nife badala ya kuishi.”+  Mungu akamuuliza Yona: “Je, una sababu nzuri ya kuwaka hasira kwa sababu ya mmung’unye?”+ Ndipo Yona akasema: “Nina sababu nzuri ya kukasirika, nimekasirika sana hivi kwamba natamani kufa.” 10  Lakini Yehova akamwambia: “Uliuhurumia mmung’unye ambao hukuufanyia kazi yoyote wala kuukuza; uliota na kukua usiku mmoja na kunyauka usiku uliofuata. 11  Je, mimi pia sipaswi kulihurumia jiji kubwa la Ninawi,+ ambalo lina watu zaidi ya 120,000 ambao hata hawajui kutofautisha jema na baya,* na kuwahurumia pia wanyama wao wengi?”+

Maelezo ya Chini

Au “neema.”
Au labda, “mbarika; mnyoyo; mbono.”
Au “kuomba nafsi yake ife.”
Au “tofauti kati ya mkono wao wa kulia na wa kushoto.”