Yoshua 11:1-23

  • Majiji ya kaskazini yatekwa (1-15)

  • Muhtasari wa ushindi wa Yoshua (16-23)

11  Mara tu Yabini mfalme wa Hasori aliposikia habari hizo, akatuma ujumbe kwa Yobabu mfalme wa Madoni,+ na kwa mfalme wa Shimroni, na mfalme wa Akshafi,+  wafalme wa eneo la kaskazini lenye milima, wa maeneo tambarare* upande wa kusini wa Kinerethi, wale waliokuwa Shefela na kwenye miteremko ya Dori+ upande wa magharibi,  Wakanaani+ upande wa mashariki na magharibi, Waamori,+ Wahiti, Waperizi, Wayebusi katika eneo lenye milima, na Wahivi+ chini ya Mlima Hermoni+ katika nchi ya Mispa.  Basi wakatoka na majeshi yao yote, watu wengi sana kama chembe za mchanga kwenye ufuo wa bahari, pamoja na farasi na magari mengi sana ya vita.  Wafalme hao wote wakakubaliana kukutana, nao wakaja na kupiga kambi karibu na chemchemi ya Meromu ili kupigana na Waisraeli.  Ndipo Yehova akamwambia Yoshua: “Usiwaogope+ kwa sababu kesho, wakati kama huu, nitawatia wote mikononi mwa Waisraeli, nanyi mtawaangamiza. Mtakata mishipa ya miguu ya farasi wao,+ na kuyachoma moto magari yao.”  Basi Yoshua na wanajeshi wake wote wakawashambulia ghafla karibu na chemchemi ya Meromu.  Yehova akawatia mikononi mwa Waisraeli,+ nao wakawashinda na kuwakimbiza mpaka Sidoni Kuu+ na Misrefoth-maimu+ na Bonde la Mispe upande wa mashariki, nao wakawaangamiza, na hakuna yeyote aliyebaki.+  Kisha Yoshua akawatendea kama Yehova alivyokuwa amemwambia; akakata mishipa ya miguu ya farasi wao na kuchoma moto magari yao.+ 10  Yoshua akarudi na kuliteka Hasori, akamuua mfalme wake kwa upanga,+ kwa sababu Hasori lilikuwa jiji kuu kati ya falme hizo zote. 11  Wakawaangamiza wakaaji wote* kwa upanga.+ Hakuna kiumbe yeyote anayepumua aliyebaki.+ Kisha akaliteketeza Hasori. 12  Yoshua akayateka majiji yote ya wafalme hao na kuwashinda wafalme wote kwa upanga.+ Akawaangamiza,+ kama Musa mtumishi wa Yehova alivyoamuru. 13  Hata hivyo, Waisraeli hawakuteketeza jiji lolote lililokuwa vilimani isipokuwa Hasori ambalo liliteketezwa na Yoshua. 14  Waisraeli wakajichukulia nyara zote na mifugo katika majiji hayo.+ Lakini wakawaangamiza wanadamu wote kwa upanga.+ Hawakumwacha mtu yeyote anayepumua.+ 15  Kama Yehova alivyomwamuru Musa mtumishi wake, ndivyo Musa alivyomwamuru Yoshua,+ na ndivyo Yoshua alivyofanya. Hakuna jambo lolote ambalo hakufanya kati ya mambo yote ambayo Yehova alimwamuru Musa.+ 16  Yoshua aliiteka nchi hii yote: eneo lenye milima, eneo lote la Negebu,+ nchi yote ya Gosheni, Shefela,+ Araba,+ na eneo lenye milima la Israeli na maeneo yake ya Shefela,* 17  kuanzia Mlima Halaki, unaopanda hadi Seiri, na hadi Baal-gadi+ katika Bonde la Lebanoni chini ya Mlima Hermoni,+ naye akawashinda, akawakamata, na kuwaua wafalme wote wa maeneo hayo. 18  Yoshua alipigana na wafalme hao wote kwa muda mrefu. 19  Hakuna jiji lolote lililofanya amani na Waisraeli isipokuwa Wahivi waliokaa Gibeoni.+ Waisraeli walipigana na majiji mengine yote na kuyashinda.+ 20  Yehova aliacha mioyo yao iwe mikaidi+ hivi kwamba wakapigana na Waisraeli, ili awaangamize bila huruma.+ Walipaswa kuangamizwa, kama Yehova alivyomwamuru Musa.+ 21  Wakati huo, Yoshua aliwaangamiza kabisa Waanaki+ kutoka katika eneo lenye milima, Hebroni, Debiri, Anabu, na kutoka katika eneo lote lenye milima la Yuda na Israeli. Yoshua aliwaangamiza watu hao na majiji yao.+ 22  Waanaki hawakubaki katika nchi ya Waisraeli; walibaki+ tu Gaza,+ Gathi,+ na Ashdodi.+ 23  Basi Yoshua akachukua nchi yote, kama Yehova alivyomwahidi Musa,+ Yoshua akawapa Waisraeli iwe urithi wao ili igawanywe kulingana na makabila yao.+ Nchi ikawa na amani bila vita.+

Maelezo ya Chini

Au “Araba.”
Au “Wakaziangamiza nafsi zote.”
Au “maeneo yake yaliyo chini ya milima.”