Yoshua 17:1-18

  • Urithi wa kabila la Manase upande wa magharibi (1-13)

  • Maeneo zaidi kwa ajili ya wazao wa Yosefu (14-18)

17  Kisha watu wa kabila la Manase,+ mzaliwa wa kwanza wa Yosefu,+ wakagawiwa nchi yao kwa kura.+ Makiri,+ mzaliwa wa kwanza wa Manase na baba ya Gileadi, alikuwa amepewa nchi ya Gileadi na Bashani+ kwa sababu alikuwa mwanajeshi hodari.  Wazao waliobaki wa Manase waligawiwa nchi yao kwa kura kulingana na koo zao, yaani, wana wa Abiezeri,+ wana wa Heleki, wana wa Asrieli, wana wa Shekemu, wana wa Heferi, na wana wa Shemida. Hao ndio wazao wa kiume wa Manase mwana wa Yosefu, kulingana na koo zao.+  Lakini Selofehadi+ mwana wa Heferi, mwana wa Gileadi, mwana wa Makiri, mwana wa Manase, hakuwa na watoto wa kiume ila mabinti, na majina ya mabinti hao yalikuwa: Mala, Noa, Hogla, Milka, na Tirsa.  Basi wakaja kwa kuhani Eleazari,+ Yoshua mwana wa Nuni, na wakuu na kuwaambia: “Yehova ndiye aliyemwamuru Musa atupe urithi miongoni mwa ndugu zetu.”+ Basi akawapa urithi kati ya ndugu za baba yao kwa agizo la Yehova.+  Na watu wa kabila la Manase walipewa pia maeneo mengine kumi zaidi ya nchi ya Gileadi na Bashani, ng’ambo ya* Yordani,+  kwa kuwa binti za Manase walipokea pia urithi pamoja na wanawe, na nchi ya Gileadi ikawa mali ya wazao waliobaki wa Manase.  Na mpaka wa Manase ulianzia Asheri hadi Mikmethathi,+ mbele ya Shekemu,+ na kuendelea hadi upande wa kusini* wa nchi ya wakaaji wa En-Tapua.  Nchi ya Tapua+ ikawa ya Manase lakini mji wa Tapua uliokuwa kwenye mpaka wa nchi ya Manase ulikuwa wa wazao wa Efraimu.  Na mpaka huo ulishuka hadi kwenye Bonde la Kana, upande wa kusini. Watu wa kabila la Efraimu walikuwa na majiji miongoni mwa majiji ya kabila la Manase,+ na mpaka wa Manase ulikuwa upande wa kaskazini wa bonde la mto, nao ulifika kwenye bahari.+ 10  Upande wa kusini ulikuwa wa kabila la Efraimu, na upande wa kaskazini ulikuwa wa Manase, na mpaka wake ulikuwa bahari,+ na mpaka wa kaskazini* ulifika kwenye eneo la Asheri na mpaka wa mashariki ulifika kwenye eneo la Isakari. 11  Katika maeneo ya Isakari na Asheri, watu wa kabila la Manase walipewa Beth-sheani na miji yake, Ibleamu+ na miji yake, Dori+ na miji yake, En-dori+ na miji yake, Taanaki+ na miji yake, Megido na miji yake, maeneo matatu yenye milima. 12  Lakini wazao wa Manase hawakumiliki majiji hayo; Wakanaani waliendelea kukaa katika nchi hiyo.+ 13  Waisraeli walipopata nguvu, waliwatumikisha Wakanaani,+ lakini hawakuwafukuza* wote.+ 14  Wazao wa Yosefu wakamuuliza Yoshua: “Kwa nini umetupatia eneo moja tu kwa kura+ na sehemu moja kuwa urithi wetu? Tuko wengi sana kwa sababu Yehova ametubariki mpaka sasa.”+ 15  Yoshua akawajibu: “Ikiwa ninyi ni wengi sana na eneo lenye milima la Efraimu+ haliwatoshi, pandeni msituni katika nchi ya Waperizi+ na Warefaimu,+ mkaufyeke msitu ili mpate makao huko.” 16  Kisha wazao wa Yosefu wakasema: “Eneo lenye milima halitutoshi, na Wakanaani wote wanaokaa bondeni,* yaani, wale wanaokaa Beth-sheani+ na miji yake na wale wanaokaa katika Bonde la* Yezreeli,+ wana magari ya vita+ yenye miundu ya chuma.”* 17  Basi Yoshua akaiambia hivi nyumba ya Yosefu, yaani, kabila la Efraimu na Manase: “Ninyi ni wengi sana, nanyi mna nguvu nyingi. Hamtapata eneo moja tu,+ 18  eneo lenye milima litakuwa lenu pia.+ Ingawa ni msitu, ufyekeni, utakuwa mwisho wa eneo lenu. Mtawafukuza Wakanaani, hata kama wana nguvu na wana magari ya vita yenye miundu ya chuma.”*+

Maelezo ya Chini

Yaani, upande wa mashariki wa.
Tnn., “upande wa kulia.”
Yaani, mpaka wa watu wa kabila la Manase au eneo la Manase.
Au “hawakuchukua nchi yao.”
Au “nchi tambarare ya chini.”
Au “Nchi Tambarare ya Chini ya.”
Tnn., “magari ya chuma.”
Tnn., “magari ya chuma.”