Yoshua 18:1-28

  • Maeneo yaliyobaki yagawanywa huko Shilo (1-10)

  • Urithi wa kabila la Benjamini (11-28)

18  Baada ya kuitiisha nchi,+ Waisraeli wote wakakusanyika Shilo+ na kupiga hema la mkutano+ huko.  Lakini makabila saba ya Waisraeli bado hayakuwa yamegawiwa urithi wao.  Ndipo Yoshua akawaambia Waisraeli: “Mtakawia mpaka lini kumiliki nchi ambayo Yehova Mungu wa mababu zenu amewapa?+  Chagueni wanaume watatu kutoka kila kabila ili niwatume; watazunguka katika nchi yote na kuchora ramani kulingana na urithi wao. Kisha wataniletea habari.  Wataigawanya nchi hiyo katika maeneo saba.+ Kabila la Yuda litabaki katika eneo lake upande wa kusini,+ na nyumba ya Yosefu itabaki katika eneo lake upande wa kaskazini.+  Igawanyeni nchi katika maeneo saba na kuniletea ramani yake, nami nitawapa urithi kwa kupiga kura+ mbele za Yehova Mungu wetu.  Lakini Walawi hawana urithi kati yenu,+ kwa sababu ukuhani wa Yehova ndio urithi wao;+ na tayari Gadi, Rubeni, na nusu ya kabila la Manase+ wamechukua urithi wao upande wa mashariki wa Yordani, ambao Musa mtumishi wa Yehova aliwapa.”  Wanaume hao wakajitayarisha kwenda kuchora ramani ya nchi, naye Yoshua akawaambia hivi: “Nendeni mkazunguke katika nchi yote, mchore ramani yake na kuniletea habari, nami nitawapa urithi kwa kupiga kura mbele za Yehova hapa Shilo.”+  Basi wanaume hao wakaenda, wakazunguka nchini na kuchora ramani yenye maeneo saba kulingana na majiji, wakaandika habari hizo katika kitabu. Kisha wakarudi kwa Yoshua kambini huko Shilo. 10  Ndipo Yoshua akapiga kura kwa ajili ya maeneo hayo mbele za Yehova.+ Kisha Yoshua akawagawia Waisraeli nchi kulingana na makabila yao.+ 11  Kabila la Benjamini liligawiwa urithi wao kwa kura kulingana na koo zao, walipewa urithi kati ya kabila la Yuda+ na wazao wa Yosefu.+ 12  Mpaka wao wa kaskazini ulianzia Yordani, na kwenda kaskazini kwenye mteremko wa Yeriko+ na kupanda mlimani upande wa magharibi, hadi katika nyika ya Beth-aveni.+ 13  Kisha ukaendelea mpaka Luzi kwenye mteremko wa kusini wa Luzi, yaani, Betheli;+ nao ukashuka hadi Ataroth-adari+ kwenye mlima ulio upande wa kusini wa Beth-horoni ya Chini.+ 14  Na mpaka huo uligeuka upande wa magharibi kuelekea kusini kutoka kwenye mlima unaotazamana na Beth-horoni upande wa kusini; nao ukafika Kiriath-baali, yaani, Kiriath-yearimu,+ jiji la Yuda. Huo ndio mpaka wa magharibi. 15  Mpaka wa kusini ulianzia mwisho wa jiji la Kiriath-yearimu, na kuelekea upande wa magharibi; kisha ukafika kwenye chemchemi ya Neftoa.+ 16  Nao ulishuka hadi mwisho wa mlima unaotazamana na Bonde la Mwana wa Hinomu,+ upande wa kaskazini katika Bonde* la Refaimu,+ nao ukashuka upande wa kusini katika Bonde la Hinomu, kwenye mteremko wa Myebusi,+ na kufika En-rogeli.+ 17  Kisha ulielekea kaskazini hadi En-shemeshi na kufika Gelilothi, mbele ya njia inayopanda kuelekea Adumimu,+ na kushuka kwenye jiwe+ la Bohani+ mwana wa Rubeni. 18  Ukaendelea hadi kwenye mteremko wa kaskazini mbele ya Araba na kushuka hadi Araba. 19  Kisha ukaendelea hadi kwenye mteremko wa kaskazini wa Beth-hogla,+ na kufika katika ghuba ya kaskazini ya Bahari ya Chumvi+ upande wa kusini wa Yordani. Huo ndio uliokuwa mpaka wa kusini. 20  Na Mto Yordani ulikuwa mpaka wa mashariki. Huo ndio uliokuwa urithi wa wazao wa Benjamini kulingana na koo zao, na hiyo ndiyo mipaka yao yote. 21  Na majiji ya kabila la Benjamini kulingana na koo zao yalikuwa: Yeriko, Beth-hogla, Emek-kesisi, 22  Beth-araba,+ Semaraimu, Betheli,+ 23  Avimu, Para, Ofra, 24  Kefar-amoni, Ofni, na Geba+—majiji 12 na vijiji vyake. 25  Gibeoni,+ Rama, Beerothi, 26  Mispe, Kefira, Mosa, 27  Rekemu, Irpeeli, Tarala, 28  Zela,+ Ha-elefu, Yebusi, yaani, Yerusalemu,+ Gibea,+ na Kiriathi—majiji 14 na vijiji vyake. Huo ndio uliokuwa urithi wa wazao wa Benjamini kulingana na koo zao.

Maelezo ya Chini

Au “Nchi Tambarare ya Chini.”