Yoshua 20:1-9

  • Majiji ya makimbilio (1-9)

20  Kisha Yehova akamwambia Yoshua:  “Waambie Waisraeli, ‘Jichagulieni majiji ya makimbilio+ kama nilivyowaambia kupitia Musa,  ili mtu atakayemuua mwenzake* bila kukusudia au bila kujua akimbilie humo. Atakimbilia humo ili kumkwepa mtu anayetaka kulipiza kisasi cha damu.+  Ni lazima akimbilie mojawapo ya majiji hayo+ na kusimama langoni,+ kisha atawaambia wazee wa jiji hilo kesi yake. Nao lazima wampokee jijini na kumpa makao, naye ataishi pamoja nao.  Na yule anayetaka kulipiza kisasi cha damu akimfuatia, wazee hawapaswi kumtia muuaji huyo mikononi mwake, kwa maana alimuua mwenzake bila kukusudia,* wala hakuwa akimchukia.+  Ni lazima akae ndani ya jiji hilo mpaka kesi yake itakaposikilizwa mbele ya kusanyiko,+ naye atabaki humo mpaka kuhani mkuu+ anayehudumu wakati huo atakapokufa. Kisha muuaji huyo anaweza kurudi nyumbani kwake katika jiji alilokimbia.’”+  Basi wakatenga majiji haya kuwa matakatifu: Kedeshi+ kule Galilaya katika eneo lenye milima la Naftali, Shekemu+ katika eneo lenye milima la Efraimu, na Kiriath-arba,+ yaani, Hebroni, katika eneo lenye milima la Yuda.  Na katika eneo la Yordani, upande wa mashariki wa Yeriko, wakachagua jiji la Beseri+ lililo nyikani kwenye uwanda wa juu katika eneo la kabila la Rubeni, Ramothi+ kule Gileadi katika eneo la kabila la Gadi, na Golani+ kule Bashani katika eneo la kabila la Manase.+  Hayo ndiyo majiji yaliyochaguliwa kwa ajili ya Waisraeli wote na wageni walioishi kati yao, ili mtu yeyote atakayemuua mwenzake bila kukusudia akimbilie humo,+ ili asiuawe na mtu anayetaka kulipiza kisasi cha damu mpaka kesi yake isikilizwe mbele ya kusanyiko.+

Maelezo ya Chini

Au “anayeua nafsi.”
Au “bila kujua.”