Yoshua 22:1-34

  • Makabila ya mashariki yarudi nyumbani (1-8)

  • Madhabahu yajengwa karibu na Yordani (9-12)

  • Kusudi la madhabahu laelezwa (13-29)

  • Mgogoro wasuluhishwa (30-34)

22  Kisha Yoshua akawaita watu wa kabila la Rubeni, Gadi, na nusu ya kabila la Manase  na kuwaambia: “Mmefanya mambo yote ambayo Musa mtumishi wa Yehova aliwaamuru mfanye,+ nanyi mmetii sauti yangu kwa kufanya mambo yote niliyowaamuru.+  Hamjawaacha ndugu zenu kwa muda wote huo, mpaka leo hii;+ nanyi mmetimiza wajibu wa kushika amri ya Yehova Mungu wenu.+  Na Yehova Mungu wenu amewapumzisha ndugu zenu kama alivyowaahidi.+ Basi sasa rudini kwenye mahema yenu katika nchi ambayo Musa mtumishi wa Yehova aliwapa ng’ambo ya* Yordani.+  Lakini muwe waangalifu sana kutekeleza amri na Sheria ambayo Musa mtumishi wa Yehova aliwapa,+ kwa kumpenda Yehova Mungu wenu,+ kutembea katika njia zake zote,+ kushika amri zake,+ kushikamana naye,+ na kumtumikia+ kwa moyo wenu wote na nafsi* yenu yote.”+  Basi Yoshua akawabariki na kuwaambia waende zao, nao wakarudi katika mahema yao.  Musa alikuwa ameipa nusu ya kabila la Manase urithi kule Bashani,+ na Yoshua akaipa nusu iliyobaki ya kabila hilo nchi upande wa magharibi wa Yordani,+ pamoja na ndugu zao. Zaidi ya hilo, Yoshua alipowaambia warudi katika mahema yao, aliwabariki  na kuwaambia: “Rudini katika mahema yenu mkiwa na utajiri mwingi, mifugo mingi sana, fedha na dhahabu, shaba na chuma, na mavazi mengi sana.+ Gawaneni na ndugu zenu nyara mlizochukua+ kutoka kwa maadui wenu.”  Kisha watu wa kabila la Rubeni, Gadi, na nusu ya kabila la Manase wakawaacha Waisraeli wengine huko Shilo katika nchi ya Kanaani, wakarudi Gileadi,+ nchi yao ya urithi waliyokuwa wakiimiliki kama Yehova alivyowaagiza kupitia Musa.+ 10  Watu wa kabila la Rubeni, Gadi, na nusu ya kabila la Manase walipofika maeneo ya Yordani katika nchi ya Kanaani, walijenga madhabahu karibu na Mto Yordani, madhabahu kubwa inayovutia. 11  Baadaye Waisraeli wengine wakasikia habari hizo+ na kusema, “Watu wa kabila la Rubeni, Gadi, na nusu ya kabila la Manase wamejenga madhabahu kwenye mpaka wa nchi ya Kanaani katika maeneo ya Yordani ambayo ni ya Waisraeli.” 12  Waisraeli waliposikia habari hizo, wakakusanyika wote Shilo+ ili waende kupigana nao. 13  Kisha Waisraeli wakamtuma Finehasi+ mwana wa kuhani Eleazari kwa watu wa kabila la Rubeni, Gadi, na nusu ya kabila la Manase katika nchi ya Gileadi, 14  na wakuu kumi walikuwa pamoja naye, mkuu mmoja kwa ajili ya kila ukoo* katika makabila yote ya Israeli, kila mmoja wao alikuwa kiongozi wa ukoo wake* miongoni mwa maelfu ya* Israeli.+ 15  Walipofika kwa watu wa kabila la Rubeni, Gadi, na nusu ya kabila la Manase katika nchi ya Gileadi, wakawaambia: 16  “Kusanyiko lote la Yehova linasema hivi: ‘Mnawezaje kukosa uaminifu kwa Mungu wa Israeli kwa kufanya jambo kama hili?+ Leo, mmeacha kumfuata Yehova kwa kujijengea madhabahu na kumwasi Yehova.+ 17  Je, dhambi tuliyotenda kule Peori haikutosha? Mpaka leo hatujajitakasa kutokana nayo hata ingawa kusanyiko la Yehova lilipata pigo.+ 18  Na sasa mnaacha kumfuata Yehova! Mkimwasi Yehova leo, kesho atawakasirikia Waisraeli wote.+ 19  Basi ikiwa mnaona nchi mliyorithi si safi, vukeni na kuingia katika nchi ya Yehova+ ambayo ina hema la ibada+ ya Yehova mkae kati yetu, lakini msimwasi Yehova, wala msitufanye tuwe waasi kwa kujijengea madhabahu nyingine zaidi ya madhabahu ya Yehova Mungu wetu.+ 20  Akani+ mwana wa Zera alipokosa uaminifu na kuchukua kitu kilichopaswa kuharibiwa, je, Mungu hakuwakasirikia Waisraeli wote?+ Akani hakufa peke yake kwa sababu ya dhambi yake.’”+ 21  Ndipo watu wa kabila la Rubeni, Gadi, na nusu ya kabila la Manase wakawajibu hivi viongozi wa maelfu* katika Israeli:+ 22  “Mungu wa miungu, Yehova!* Mungu wa miungu, Yehova!+ Anajua, na Waisraeli pia watajua. Ikiwa tuliasi na kukosa uaminifu kwa Yehova, msituache hai leo. 23  Ikiwa tulijijengea madhabahu ili tuache kumfuata Yehova na kutoa juu yake dhabihu za kuteketezwa, matoleo ya nafaka, na dhabihu za ushirika, Yehova atatuadhibu.+ 24  Lakini hatukuijenga kwa sababu hiyo, tuliijenga kwa sababu tulisema, ‘Wakati ujao wana wenu watawauliza wana wetu: “Mna haki gani ya kumwabudu* Yehova Mungu wa Israeli? 25  Yehova ameweka Mto Yordani kuwa mpaka kati yetu na ninyi, watu wa kabila la Rubeni na Gadi. Hamna ushirika wowote na Yehova.” Na wana wenu watawazuia wana wetu kumwabudu* Yehova.’ 26  “Basi tukasema, ‘Kwa vyovyote vile, tujenge madhabahu, lakini si kwa ajili ya matoleo au dhabihu za kuteketezwa, 27  bali iwe ushahidi kati yetu na ninyi+ na wazao wetu* kwamba tutamtumikia Yehova kwa dhabihu zetu za kuteketezwa, na matoleo yetu, na dhabihu zetu za ushirika,+ ili wana wenu wasiwaambie hivi wana wetu wakati ujao: “Hamna ushirika wowote na Yehova.”’ 28  Basi tukasema, ‘Wakituambia hivyo sisi na wazao wetu* wakati ujao, tutawajibu: “Angalieni mfano wa madhabahu ya Yehova ambayo mababu zetu walijenga, si kwa ajili ya matoleo au dhabihu za kuteketezwa, bali iwe ushahidi kati yetu na ninyi.”’ 29  Hatuwezi kamwe kuwazia kumwasi Yehova na kuacha kumfuata+ Yehova kwa kujenga madhabahu nyingine kwa ajili ya dhabihu za kuteketezwa, matoleo ya nafaka, na matoleo mengine, zaidi ya madhabahu ya Yehova Mungu wetu ambayo iko mbele ya hema lake la ibada!”+ 30  Basi kuhani Finehasi, wakuu wa Waisraeli, na viongozi wa maelfu* katika Israeli waliokuwa pamoja naye waliposikia maneno yaliyosemwa na wazao wa Rubeni, Gadi, na Manase, wakaridhika.+ 31  Ndipo Finehasi mwana wa kuhani Eleazari akawaambia wazao wa Rubeni, Gadi, na Manase: “Leo tunajua kwamba Yehova yuko kati yetu kwa sababu hamjakosa uaminifu kwa Yehova katika jambo hili. Sasa mmewaokoa Waisraeli kutoka mikononi mwa Yehova.” 32  Baada ya Finehasi mwana wa kuhani Eleazari na wale wakuu kukutana na watu wa kabila la Rubeni na Gadi katika nchi ya Gileadi wakarudi katika nchi ya Kanaani na kuwaambia Waisraeli wengine habari hizo. 33  Na Waisraeli wakaridhika na habari hizo. Wakamsifu Mungu na kuacha mipango ya kupigana na watu wa kabila la Rubeni na Gadi na kuiharibu nchi yao. 34  Watu wa kabila la Rubeni na Gadi wakaipa jina madhabahu* hiyo, kwa sababu walisema “ni ushahidi kati yetu kwamba Yehova ndiye Mungu wa kweli.”

Maelezo ya Chini

Yaani, upande wa mashariki wa.
Angalia Kamusi.
Au “koo za.”
Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Au “koo.”
Au “Mungu Mkuu, Yehova.”
Tnn., “Mna nini na.”
Tnn., “kumwogopa.”
Tnn., “vizazi vyetu.”
Tnn., “vizazi vyetu.”
Au “koo.”
Maelezo haya yanaonyesha kwamba huenda madhabahu hiyo iliitwa Ushahidi au Ushuhuda.