Yoshua 5:1-15

  • Waisraeli watahiriwa kule Gilgali (1-9)

  • Sherehe ya Pasaka; mwisho wa mana (10-12)

  • Mkuu wa jeshi la Yehova (13-15)

5  Mara tu wafalme wote wa Waamori+ waliokuwa upande wa magharibi* wa Yordani na wafalme wote wa Wakanaani+ waliokuwa karibu na bahari waliposikia kwamba Yehova alikausha maji ya Yordani mpaka Waisraeli walipovuka, wakafa moyo*+ na hawakuwa na ujasiri wowote kwa sababu ya Waisraeli.+  Wakati huo Yehova akamwambia hivi Yoshua: “Tengeneza visu vya jiwe gumu na uwatahiri+ wanaume Waisraeli tena, mara ya pili.”  Basi Yoshua akatengeneza visu vya jiwe gumu na kuwatahiri wanaume Waisraeli kule Gibeath-haaralothi.*+  Yoshua aliwatahiri kwa sababu wanaume wote waliotoka Misri, yaani, wanaume wote wa kwenda vitani,* walikufa nyikani walipotoka Misri.+  Kwa maana watu wote waliotoka Misri walikuwa wametahiriwa, lakini watu wote waliozaliwa nyikani wakiwa safarini kutoka Misri hawakuwa wametahiriwa.  Waisraeli walitembea miaka 40+ nyikani mpaka taifa lote lilipokufa, yaani, wanaume wote wa kwenda vitani waliotoka Misri ambao hawakutii sauti ya Yehova.+ Yehova aliwaapia kwamba hatawaruhusu kamwe waione nchi+ ambayo Yehova alikuwa amewaapia mababu zao kwamba atatupatia,+ nchi inayotiririka maziwa na asali.+  Kwa hiyo, akawainua wana wao badala yao.+ Yoshua akawatahiri wana hao kwa sababu hawakuwa wametahiriwa safarini.  Walipomaliza kutahiri taifa lote, wakaendelea kukaa kambini mpaka walipopona.  Kisha Yehova akamwambia Yoshua: “Leo nimewaondolea aibu ya Misri.” Basi tangu wakati huo mahali hapo panaitwa Gilgali.*+ 10  Waisraeli wakaendelea kupiga kambi Gilgali, nao wakaadhimisha Pasaka siku ya 14 ya mwezi huo,+ wakati wa jioni, katika jangwa tambarare la Yeriko. 11  Kesho yake, baada ya Pasaka, siku hiyohiyo wakaanza kula mazao ya nchi, yaani, mikate isiyo na chachu+ na nafaka zilizokaangwa. 12  Mana ilikoma siku iliyofuata, baada ya Waisraeli kula baadhi ya mazao ya nchi; Waisraeli hawakupata mana tena,+ wakaanza kula mazao ya nchi ya Kanaani mwaka huo.+ 13  Yoshua alipokuwa karibu na Yeriko, aliinua macho na kumwona mwanamume+ fulani amesimama mbele yake akiwa ameshika upanga uliochomolewa.+ Yoshua akamkaribia na kumuuliza: “Uko upande wetu au wa maadui wetu?” 14  Akamjibu: “Hapana, mimi ni mkuu* wa jeshi la Yehova.”+ Basi Yoshua akaanguka chini kifudifudi, akasujudu, na kumwambia: “Bwana wangu una ujumbe gani kwangu mimi mtumishi wako?” 15  Mkuu wa jeshi la Yehova akamjibu hivi Yoshua: “Vua viatu vyako, kwa sababu mahali unaposimama ni patakatifu.” Yoshua akavua mara moja.+

Maelezo ya Chini

Tnn., “upande unaoelekea baharini.”
Tnn., “mioyo yao ikayeyuka.”
Maana yake “Kilima cha Magovi.”
Au “wanaume wote wenye umri wa kwenda vitani.”
Maana yake “Kuondoa; Kuondolea Mbali.”
Au “kiongozi.”