Yoshua 7:1-26

  • Waisraeli washindwa kule Ai (1-5)

  • Sala ya Yoshua (6-9)

  • Dhambi yasababisha Waisraeli washindwe (10-15)

  • Akani afichuliwa na kupigwa mawe (16-26)

7  Lakini Waisraeli walikosa uaminifu kuhusiana na vitu vilivyopaswa kuharibiwa, kwa kuwa Akani+ mwana wa Karmi, mwana wa Zabdi, mwana wa Zera, wa kabila la Yuda, alichukua baadhi ya vitu vilivyopaswa kuharibiwa.+ Ndipo hasira ya Yehova ikawaka dhidi ya Waisraeli.+  Basi Yoshua akatuma wanaume kutoka Yeriko waende Ai,+ karibu na Beth-aveni, upande wa mashariki wa Betheli,+ akawaambia: “Pandeni mkaipeleleze nchi.” Kwa hiyo wanaume hao wakapanda na kwenda kupeleleza jiji la Ai.  Waliporudi kwa Yoshua, wakamwambia: “Si lazima watu wote waende. Wanaume elfu mbili au elfu tatu hivi wanatosha kulishinda jiji la Ai. Usiwachoshe watu wote kwa kuwatuma huko, kwa sababu jiji hilo lina watu wachache tu.”  Basi wanaume wapatao 3,000 wakapanda huko, lakini wakakimbizwa na wanaume wa Ai.+  Na wanaume hao wa Ai wakawaua watu 36, wakawakimbiza kutoka nje ya lango la jiji mpaka Shebarimu,* wakaendelea kuwaua kwenye mteremko. Basi ujasiri wa watu ukayeyuka* na kuwa kama maji.  Ndipo Yoshua akararua mavazi yake na kuanguka chini kifudifudi mbele ya Sanduku la Yehova mpaka jioni, yeye pamoja na wazee wa Israeli, nao wakaendelea kujirushia mavumbi vichwani.  Yoshua akasema: “Ole wangu, Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, kwa nini umewaleta watu hawa njia yote hii na kuwavusha Yordani ili tu kututia mikononi mwa Waamori watuangamize? Ni afadhali tungeridhika kubaki ng’ambo ile nyingine ya* Yordani!  Nakusihi Ee Yehova, niseme nini baada ya Waisraeli kuwakimbia maadui wao?  Wakanaani na wakaaji wote wa nchi hii watakaposikia habari hii, watatuzingira na kufutilia mbali jina letu kutoka duniani, nawe utafanya nini kwa ajili ya jina lako kuu?”+ 10  Yehova akamwambia Yoshua: “Inuka! Kwa nini umelala chini kifudifudi? 11  Waisraeli wametenda dhambi. Wamevunja agano langu+ nililowaamuru washike. Wamechukua baadhi ya vitu vilivyopaswa kuharibiwa,+ wameviiba+ na kuvificha kati ya vitu vyao.+ 12  Kwa hiyo, Waisraeli hawawezi kusimama dhidi ya maadui wao. Watageuka na kuwakimbia maadui wao, kwa sababu wanapaswa kuangamizwa. Sitakuwa pamoja nanyi tena msipoharibu kitu mlicho nacho kinachopaswa kuharibiwa.+ 13  Inuka uwatakase watu!+ Waambie, ‘Jitakaseni kesho, kwa sababu Yehova Mungu wa Israeli anasema hivi: “Kuna kitu kinachopaswa kuharibiwa miongoni mwenu, Ee Israeli. Hamtaweza kusimama dhidi ya maadui wenu msipoondoa kitu kinachopaswa kuharibiwa. 14  Mtakusanyika asubuhi, kabila kwa kabila, na kabila ambalo Yehova atachagua+ litakaribia, ukoo kwa ukoo, na ukoo ambao Yehova atachagua utakaribia, nyumba kwa nyumba, na nyumba ambayo Yehova atachagua itakaribia, mwanamume kwa mwanamume. 15  Mtu atakayepatikana akiwa na kitu kinachopaswa kuharibiwa atateketezwa kwa moto,+ yeye pamoja na vitu vyake vyote, kwa sababu amevunja agano+ la Yehova na kwa sababu ametenda jambo la aibu katika Israeli.”’” 16  Kesho yake, Yoshua akaamka asubuhi na mapema akawakusanya Waisraeli, kabila kwa kabila, na kabila la Yuda likachaguliwa. 17  Kisha akaleta karibu koo za Yuda na ukoo wa Wazera+ ukachaguliwa, kisha akaleta karibu familia za ukoo wa Wazera, mwanamume kwa mwanamume, na Zabdi akachaguliwa. 18  Mwishowe akaleta karibu familia ya Zabdi, mwanamume kwa mwanamume, naye Akani mwana wa Karmi, mwana wa Zabdi, mwana wa Zera, wa kabila la Yuda, akachaguliwa.+ 19  Kisha Yoshua akamwambia Akani: “Tafadhali mwanangu, mheshimu Yehova Mungu wa Israeli na uungame kwake. Tafadhali niambie jambo ulilofanya. Usinifiche chochote.” 20  Akani akamwambia Yoshua: “Kwa kweli ni mimi niliyemtendea dhambi Yehova Mungu wa Israeli, na hili ndilo jambo nililofanya. 21  Nilipoona katika nyara vazi rasmi maridadi kutoka Shinari+ na shekeli 200 za fedha na kipande kimoja cha dhahabu chenye uzito wa shekeli 50,* nilivitamani, kwa hiyo nikavichukua. Nimevificha ardhini ndani ya hema langu, na fedha ziko chini yake.” 22  Mara moja Yoshua akatuma wajumbe, wakakimbia kwenda hemani, wakakuta lile vazi likiwa limefichwa ndani ya hema lake, na fedha zilikuwa chini yake. 23  Basi wakavichukua vitu hivyo kutoka hemani na kumletea Yoshua na Waisraeli wote na kuviweka mbele za Yehova. 24  Yoshua na Waisraeli wote wakamchukua Akani+ mwana wa Zera, zile fedha, lile vazi rasmi maridadi, na kile kipande cha dhahabu,+ pamoja na wanawe, binti zake, ng’ombe dume wake, punda wake, kondoo na mbuzi wake, hema lake, na vitu vyake vyote, wakavileta katika Bonde la* Akori.+ 25  Yoshua akasema: “Kwa nini umetuletea msiba?*+ Leo Yehova atakuletea msiba.” Ndipo Waisraeli wote wakawapiga mawe,+ kisha wakawateketeza kwa moto.+ Naam, waliwapiga mawe wote. 26  Nao wakarundika mawe mengi juu yake ambayo yapo hadi leo. Ndipo hasira ya Yehova ikapoa.+ Ndiyo sababu tangu siku hiyo mahali hapo panaitwa Bonde la Akori.*

Maelezo ya Chini

Maana yake “Machimbo.”
Tnn., “mioyo ya watu ikayeyuka.”
Yaani, upande wa mashariki wa.
Shekeli moja ilikuwa na uzito wa gramu 11.4. Angalia Nyongeza B14.
Au “Nchi Tambarare ya Chini ya.”
Au “shida; laana.”
Maana yake “Msiba; Laana.”