Yoshua 8:1-35

  • Yoshua avamia Ai (1-13)

  • Jiji la Ai latekwa (14-29)

  • Sheria yasomwa kwenye Mlima Ebali (30-35)

8  Kisha Yehova akamwambia Yoshua: “Usiogope wala usihofu.+ Nenda na wanajeshi wote ulishambulie jiji la Ai. Naam, nimemtia mikononi mwako mfalme wa Ai, watu wake, jiji lake, na nchi yake.+  Mlitendee Ai na mfalme wake kama mlivyolitendea Yeriko na mfalme wake,+ lakini mnaweza kujichukulia nyara zake na mifugo yake. Wekeni watu watakaovizia nyuma ya jiji hilo.”  Basi Yoshua na wanajeshi wote wakaenda kulishambulia jiji la Ai. Yoshua akachagua mashujaa hodari 30,000 na kuwatuma wakati wa usiku.  Akawaamuru hivi: “Mtavizia nyuma ya jiji. Msiende mbali sana na jiji, na nyote kaeni tayari.  Mimi na watu walio pamoja nami tutalikaribia jiji, na watakapotoka ili kutushambulia kama walivyofanya mwanzoni,+ tutawakimbia.  Watakapotukimbiza, tutawavuta mbali na jiji lao, kwa kuwa watasema, ‘Wanatukimbia kama walivyofanya mwanzoni.’+ Nasi tutaendelea kuwakimbia.  Kisha mtatoka mahali mnapovizia na kuliteka jiji; Yehova Mungu wenu atalitia mikononi mwenu.  Na mara tu baada ya kuliteka jiji, mnapaswa kuliteketeza kwa moto.+ Mtafanya kama Yehova alivyoagiza. Hayo ndiyo maagizo mtakayofuata.”  Kisha Yoshua akawatuma, nao wakaenda kuvizia; wakapiga kambi kati ya Betheli na Ai, upande wa magharibi wa Ai, lakini Yoshua alikaa pamoja na watu usiku huo. 10  Yoshua akaamka asubuhi na mapema, akakusanya wanajeshi, kisha yeye na wazee wa Israeli wakawaongoza hadi Ai. 11  Na wanajeshi wote+ waliokuwa pamoja naye wakapanda na kukaribia mbele ya jiji. Wakapiga kambi upande wa kaskazini wa Ai, na bonde lilikuwa kati yao na Ai. 12  Wakati huo, alikuwa ameweka wanajeshi wapatao 5,000 wavizie+ kati ya Betheli+ na Ai, upande wa magharibi wa jiji. 13  Basi kikosi kikubwa kilikuwa upande wa kaskazini wa jiji+ na wanajeshi waliokuwa wakivizia nyuma walikuwa upande wa magharibi wa jiji,+ na usiku huo Yoshua akaenda katikati ya bonde.* 14  Na mara tu mfalme wa Ai alipoona hilo, yeye pamoja na wanaume wa jiji wakaamka mapema na kwenda haraka kupigana na Waisraeli mahali fulani ng’ambo ya jangwa tambarare. Lakini hakujua kwamba kulikuwa na wanajeshi waliokuwa wakivizia nyuma ya jiji. 15  Watu wa Ai walipowashambulia, Yoshua na wanajeshi wote Waisraeli wakakimbia barabarani kuelekea nyikani.+ 16  Ndipo watu wote waliokuwa ndani ya jiji wakaambiwa wawakimbize; na walipokuwa wakimkimbiza Yoshua, walienda mbali na jiji. 17  Hakuna mwanamume yeyote aliyebaki Ai na Betheli, wote waliwakimbiza Waisraeli. Waliacha jiji lao wazi na kuwakimbiza Waisraeli. 18  Sasa Yehova akamwambia Yoshua, “Nyoosha mkuki ulio mkononi mwako kuelekea Ai,+ kwa maana nitalitia jiji hilo mikononi mwako.”+ Basi Yoshua akanyoosha mkuki uliokuwa mkononi mwake kuelekea jiji hilo. 19  Na mara tu aliponyoosha mkono wake, wanajeshi waliokuwa wakivizia wakatoka haraka mahali walipokuwa, wakakimbia kuingia jijini, na kuliteka jiji hilo. Na mara moja wakaliteketeza.+ 20  Wanaume wa Ai walipogeuka na kuangalia nyuma, wakaona moshi ukipanda angani kutoka jijini, wakaishiwa na nguvu na hawakuweza kukimbia upande wowote. Kisha wanajeshi Waisraeli waliokuwa wakikimbia kuelekea nyikani wakageuka na kuanza kuwashambulia wale waliokuwa wakiwakimbiza. 21  Yoshua na Waisraeli wote walipoona kwamba wanajeshi waliovizia walikuwa wameliteka jiji na kuona moshi ukipanda kutoka jijini, wakageuka na kuwashambulia wanaume wa Ai. 22  Na wale walioliteka jiji wakaenda kuungana na wenzao, na wanaume wa Ai wakanaswa katikati, baadhi ya Waisraeli walikuwa upande huu na wengine upande wa pili, wakawaua na hakuna yeyote aliyeokoka wala kuponyoka.+ 23  Lakini walimkamata mfalme wa Ai+ akiwa hai na kumpeleka kwa Yoshua. 24  Baada ya Waisraeli kumaliza kuwaua wakaaji wote wa Ai nyikani, ambako waliwafuatia na kumuua kila mmoja wao kwa upanga, Waisraeli wote walirudi Ai na kuwaua kwa upanga watu waliobaki jijini. 25  Watu wote walioangamia siku hiyo, wanaume na wanawake, walikuwa 12,000, yaani, watu wote wa Ai. 26  Yoshua hakuushusha mkono wake uliokuwa umeshika mkuki+ mpaka alipowaangamiza wakaaji wote wa Ai.+ 27  Hata hivyo, Waisraeli walijichukulia mifugo na nyara za jiji kama Yehova alivyomwagiza Yoshua.+ 28  Kisha Yoshua akateketeza jiji la Ai, na tangu siku hiyo likabaki rundo la kudumu la magofu.+ 29  Akamtundika mtini mfalme wa Ai mpaka jioni, na jua lilipokaribia kutua, Yoshua akaagiza maiti yake iondolewe mtini.+ Kisha wakaitupa kwenye lango la jiji na kurundika mawe mengi juu ya maiti hiyo, na rundo hilo lipo mpaka leo. 30  Kisha Yoshua akamjengea Yehova Mungu wa Israeli madhabahu kwenye Mlima Ebali,+ 31  kama Musa mtumishi wa Yehova alivyowaamuru Waisraeli na kama ilivyoandikwa katika kitabu cha Sheria+ ya Musa: “Madhabahu ya mawe ambayo hayakuchongwa wala kuguswa na kifaa chochote cha chuma.”+ Na juu yake wakamtolea Yehova dhabihu za kuteketezwa na pia dhabihu za ushirika.+ 32  Kisha akiwa huko akaandika juu ya mawe hayo nakala ya Sheria+ ambayo Musa alikuwa ameandika mbele ya Waisraeli.+ 33  Waisraeli wote pamoja na wazee wao, viongozi wao, na waamuzi wao, walikuwa wamesimama pande mbili za hilo sanduku la agano la Yehova mbele ya makuhani Walawi waliokuwa wamelibeba. Wakaaji wageni na pia wenyeji walikuwepo.+ Nusu yao walisimama mbele ya Mlima Gerizimu, na nusu walisimama mbele ya Mlima Ebali+ (kama Musa mtumishi wa Yehova alivyokuwa ameagiza mwanzoni),+ ili kuwabariki Waisraeli. 34  Kisha Yoshua akasoma kwa sauti maneno yote ya Sheria,+ baraka+ na laana,+ kulingana na yote ambayo yameandikwa katika kitabu cha Sheria. 35  Hakuna neno lolote kati ya maneno yote ambayo Musa alikuwa ameamuru ambalo Yoshua hakusoma kwa sauti mbele ya kutaniko lote la Israeli,+ lililotia ndani wanawake, watoto, na wakaaji wageni+ walioishi* miongoni mwao.+

Maelezo ya Chini

Au “nchi tambarare ya chini.”
Tnn., “waliotembea.”