Yoshua 9:1-27

  • Wagibeoni wajanja watafuta amani (1-15)

  • Hila ya Wagibeoni yagunduliwa (16-21)

  • Wagibeoni watakuwa watekaji wa maji na wakusanyaji wa kuni (22-27)

9  Waliposikia habari hizo, wafalme wote waliokuwa upande wa magharibi wa Yordani,+ katika eneo lenye milima, na Shefela, na eneo lote la pwani ya Bahari Kuu,*+ na mbele ya Lebanoni—Wahiti, Waamori, Wakanaani, Waperizi, Wahivi, na Wayebusi+  wakaungana ili kupigana na Yoshua na Waisraeli.+  Wakaaji wa Gibeoni+ walisikia pia mambo ambayo Yoshua alitenda katika jiji la Yeriko+ na Ai.+  Basi wakatenda kwa busara na kuweka vyakula katika magunia yaliyochakaa na kuyabeba kwa punda wao, pamoja na viriba vya divai vilivyochakaa na kutiwa viraka;  pia walivaa viatu vilivyochakaa vyenye viraka na nguo zilizochakaa. Na mikate waliyobeba ilikuwa imekauka na kuvunjika-vunjika.  Kisha wakaenda kwa Yoshua kambini kule Gilgali,+ wakamwambia yeye na wazee wa Waisraeli: “Tumetoka nchi ya mbali. Basi fanyeni agano pamoja nasi.”  Lakini wazee wa Waisraeli wakawaambia hao Wahivi:+ “Huenda mnakaa karibu nasi. Tunawezaje kufanya agano nanyi?”+  Wakamjibu Yoshua: “Sisi ni watumishi* wako.” Kisha Yoshua akawauliza: “Ninyi ni nani, na mnatoka wapi?”  Wakamjibu: “Sisi watumishi wako tumetoka nchi ya mbali sana+ kwa sababu ya heshima ya jina la Yehova Mungu wako, kwa kuwa tumesikia umaarufu wake na mambo yote aliyotenda Misri+ 10  na mambo yote aliyowatendea wale wafalme wawili wa Waamori waliokuwa ng’ambo ya* Yordani, yaani, Mfalme Sihoni+ wa Heshboni na Mfalme Ogu+ wa Bashani, aliyekuwa Ashtarothi. 11  Kwa hiyo wazee wetu na wakaaji wote wa nchi yetu wakatuambia, ‘Bebeni chakula kwa ajili ya safari mwende mkakutane nao. Waambieni hivi: “Tutakuwa watumishi wenu;+ basi fanyeni agano pamoja nasi.”’+ 12  Mikate hii ilikuwa moto tulipotoka nyumbani ili kuja hapa. Sasa angalieni jinsi ilivyokauka na inavyovunjika-vunjika.+ 13  Na viriba hivi vilikuwa vipya tulipovijaza divai, lakini sasa vimepasuka.+ Na nguo na viatu vyetu vimechakaa kwa sababu ya safari ndefu.” 14  Ndipo wazee wa Waisraeli wakachukua* vyakula vyao, lakini hawakutafuta mwongozo wa Yehova.+ 15  Basi Yoshua akafanya amani nao,+ pia akafanya agano pamoja nao ili kuwaacha waishi, na hivyo ndivyo wakuu wa Waisraeli walivyowaapia.+ 16  Siku tatu baada ya kufanya agano pamoja nao, wakasikia kwamba walikuwa majirani wao na waliishi karibu nao. 17  Ndipo Waisraeli wakaanza safari na kufika katika majiji ya watu hao siku ya tatu; na majiji yao yalikuwa Gibeoni,+ Kefira, Beerothi, na Kiriath-yearimu.+ 18  Lakini Waisraeli hawakuwashambulia, kwa sababu wakuu wa Waisraeli walikuwa wamewaapia kwa jina la Yehova+ Mungu wa Israeli. Kwa hiyo Waisraeli wote wakaanza kuwanung’unikia wakuu hao. 19  Basi wakuu wote wakawaambia hivi: “Kwa kuwa tuliwaapia kwa jina la Yehova Mungu wa Israeli haturuhusiwi kuwadhuru. 20  Hili ndilo jambo tutakalofanya: Tutawaacha waishi, ili hasira ya Mungu isiwake dhidi yetu kwa sababu ya kiapo tulichowaapia.”+ 21  Wakuu wakaendelea kuwaambia hivi: “Waacheni waishi, lakini watakuwa wakusanyaji wa kuni na watekaji wa maji kwa ajili ya Waisraeli wote.” Hivyo ndivyo wakuu walivyowaahidi. 22  Basi Yoshua akawaita na kuwauliza: “Kwa nini mlitudanganya mkisema, ‘Tumetoka mbali sana,’ na kumbe mnaishi karibu kabisa nasi?+ 23  Kuanzia sasa mmelaaniwa,+ na sikuzote mtakuwa watumwa wa kukusanya kuni na kuteka maji kwa ajili ya nyumba ya Mungu wangu.” 24  Ndipo wakamjibu Yoshua: “Tulifanya hivyo kwa sababu sisi watumishi wako tuliambiwa waziwazi kwamba Yehova Mungu wako alimwamuru Musa mtumishi wake awape ninyi nchi yote na kuwaangamiza wakaaji wote kutoka mbele yenu.+ Basi tulifanya hivyo kwa sababu tuliogopa mtatuua.+ 25  Sasa tuonyeshe rehema.* Tutendee upendavyo.” 26  Na hivyo ndivyo alivyofanya; aliwaokoa kutoka mikononi mwa Waisraeli, nao hawakuwaua. 27  Lakini tangu siku hiyo, Yoshua akawafanya kuwa wakusanyaji wa kuni na watekaji wa maji kwa ajili ya kusanyiko+ na kwa ajili ya madhabahu ya Yehova mahali ambapo Mungu angechagua.+

Maelezo ya Chini

Yaani, Mediterania.
Au “watumwa.”
Yaani, upande wa mashariki wa.
Au “wakakagua.”
Tnn., “tumo mikononi mwako.”