Zekaria 1:1-21

  • Mwito wa kumrudia Yehova (1-6)

    • ‘Nirudieni nami nitawarudia’ (3)

  • Maono ya 1: Wapanda farasi katikati ya mihadasi (7-17)

    • “Yehova atalifariji tena Sayuni” (17)

  • Maono ya 2: Pembe nne na mafundi wanne (18-21)

1  Katika mwezi wa nane, mwaka wa pili wa utawala wa Dario,+ neno la Yehova lilimjia nabii Zekaria*+ mwana wa Berekia mwana wa Ido, likisema:  “Yehova aliwakasirikia vikali baba zenu.+  “Waambie, ‘Yehova wa majeshi anasema hivi: “‘Nirudieni,’ asema Yehova wa majeshi, ‘nami nitawarudia ninyi,’+ asema Yehova wa majeshi.”’  “‘Msiwe kama baba zenu walioambiwa hivi na manabii wa kale: “Yehova wa majeshi anasema, ‘Tafadhali, geukeni* kutoka katika njia zenu ovu na matendo yenu maovu.’”’+ “‘Lakini hawakusikiliza, wala hawakunikazia uangalifu,’+ asema Yehova.  “‘Baba zenu wako wapi sasa? Na je, manabii wanaishi milele?  Hata hivyo, je, maneno yangu na maagizo yangu niliyowaamuru watumishi wangu, manabii, hayakutimia kwa baba zenu?’+ Basi wakanirudia na kusema: ‘Yehova wa majeshi ametutendea kulingana na njia zetu na matendo yetu, kama alivyokusudia kututendea.’”+  Katika siku ya 24 ya mwezi wa 11, yaani, mwezi wa Shebati,* katika mwaka wa pili wa utawala wa Dario,+ neno la Yehova lilimjia nabii Zekaria mwana wa Berekia mwana wa Ido, likisema:  “Niliona maono wakati wa usiku. Nilimwona mtu akiendesha farasi mwekundu, akasimama tuli bondeni katikati ya miti ya mihadasi; na nyuma yake kulikuwa na farasi wekundu, wa kahawia, na weupe.”  Basi nikauliza: “Hawa ni nani, bwana wangu?” Malaika aliyekuwa akizungumza nami akanijibu: “Nitakuonyesha hawa ni nani.” 10  Kisha mtu huyo aliyesimama tuli katikati ya mihadasi akasema: “Hawa ndio wale ambao Yehova amewatuma watembee huku na huku duniani.” 11  Nao wakamwambia malaika huyo wa Yehova aliyekuwa amesimama katikati ya mihadasi: “Tumetembea huku na huku duniani, na tazama! dunia yote imetulia na haina vurugu.”+ 12  Basi malaika wa Yehova akauliza: “Ee Yehova wa majeshi, utaendelea hadi lini kukataa kuwaonyesha rehema wakaaji wa Yerusalemu na wa majiji ya Yuda,+ ambao umewakasirikia kwa miaka hii 70?”+ 13  Yehova akamjibu kwa maneno ya fadhili na yenye kufariji malaika huyo aliyekuwa akizungumza nami. 14  Kisha malaika huyo aliyekuwa akizungumza nami akaniambia: “Tangaza hivi kwa sauti, ‘Yehova wa majeshi anasema hivi: “Nina bidii kwa ajili ya Yerusalemu na Sayuni, bidii nyingi.+ 15  Kwa hasira kali nimeyakasirikia mataifa yanayostarehe,+ kwa sababu niliwakasirikia kidogo watu wangu,+ lakini yalizidisha msiba wao.”’+ 16  “Basi Yehova anasema hivi: ‘“Nitarudi Yerusalemu kwa rehema,+ na nyumba yangu mwenyewe itajengwa humo,”+ asema Yehova wa majeshi, “na kamba ya kupimia itanyooshwa juu ya Yerusalemu.”’+ 17  “Tangaza tena hivi kwa sauti: ‘Yehova wa majeshi anasema, “Majiji yangu yatafurika wema tena; na Yehova atalifariji tena Sayuni+ na kulichagua tena Yerusalemu.”’”+ 18  Kisha nikatazama juu na kuona pembe nne.+ 19  Kwa hiyo nikamuuliza malaika aliyekuwa akizungumza nami: “Pembe hizi zinamaanisha nini?” Akanijibu: “Pembe hizi ndizo zilizowatawanya watu wa Yuda,+ Israeli,+ na Yerusalemu.”+ 20  Kisha Yehova akanionyesha mafundi wanne. 21  Nikauliza: “Hawa wanakuja kufanya nini?” Akajibu: “Hizi ndizo pembe zilizowatawanya watu wa Yuda hivi kwamba hakuna yeyote aliyeweza kuinua kichwa chake. Mafundi hawa watakuja kuzitisha, kuziangusha chini pembe za mataifa yaliyoinua pembe zao dhidi ya nchi ya Yuda, ili kuwatawanya wakaaji wake.”

Maelezo ya Chini

Maana yake “Yehova Amekumbuka.”
Au “rudini.”