Zekaria 14:1-21

  • Ibada ya kweli yashinda kabisa (1-21)

    • Mlima wa Mizeituni utagawanyika katikati (4)

    • Yehova atakuwa Mungu pekee, na jina lake litakuwa ndilo jina pekee (9)

    • Ugonjwa utakaowapata wanaopigana na Yerusalemu (12-15)

    • Sherehe ya Vibanda (16-19)

    • Kila chungu kitakuwa kitakatifu kwa Yehova (20, 21)

14  “Tazama! Siku inakuja, siku ya Yehova, wakati ambapo nyara yenu* itagawanywa miongoni mwenu.  Nitayakusanya mataifa yote ili yapigane vita na Yerusalemu; na jiji hilo litatekwa na nyumba zitaporwa na wanawake watabakwa. Na nusu ya wakaaji wa jiji hilo watapelekwa uhamishoni, lakini watakaobaki jijini hawataangamizwa.  “Yehova atatoka na kupigana vita na mataifa hayo+ kama anavyopigana katika siku ya vita.+  Siku hiyo miguu yake itasimama kwenye Mlima wa Mizeituni,+ unaotazamana na jiji la Yerusalemu upande wa mashariki; na Mlima wa Mizeituni utagawanyika katikati, kuanzia mashariki* mpaka magharibi,* na bonde kubwa sana litatokea; na nusu ya mlima huo itaelekea kaskazini, na nusu nyingine kusini.  Mtakimbilia kwenye bonde la milima yangu, kwa maana bonde la milima hiyo litafika mpaka Aseli. Mtalazimika kukimbia kama mlivyokimbia kwa sababu ya tetemeko la ardhi katika siku za utawala wa Mfalme Uzia wa Yuda.+ Na Yehova Mungu wangu atakuja, na watakatifu wote watakuwa pamoja naye.+  “Siku hiyo hakutakuwa na nuru yenye thamani+—vitu vitagandishwa.*  Nayo itakuwa siku inayojulikana kuwa siku ya Yehova.+ Haitakuwa mchana, wala haitakuwa usiku; na jioni kutakuwa na nuru.  Siku hiyo maji yaliyo hai+ yatatiririka kutoka Yerusalemu,+ nusu yataelekea kwenye bahari ya mashariki*+ na nusu yataelekea kwenye bahari ya magharibi.*+ Hilo litatukia wakati wa kiangazi na wa baridi kali.  Na Yehova atakuwa Mfalme juu ya dunia yote.+ Siku hiyo Yehova atakuwa Mungu pekee,+ na jina lake litakuwa ndilo jina pekee.+ 10  “Nchi yote itakuwa kama Araba,+ kuanzia Geba+ mpaka Rimoni+ upande wa kusini wa Yerusalemu; na jiji la Yerusalemu litainuka na kukaliwa na watu,+ kuanzia Lango la Benjamini+ mpaka kwenye Lango la Kwanza, mpaka kwenye Lango la Pembeni, na kuanzia Mnara wa Hananeli+ mpaka kwenye mashinikizo ya divai* ya mfalme. 11  Na watu watakaa jijini humo; hakutakuwa tena na laana ya uharibifu,+ na watu watakaa Yerusalemu kwa usalama.+ 12  “Na huu ndio ugonjwa hatari ambao Yehova atawaletea watu wote wanaopigana vita na Yerusalemu:+ Miili yao itaoza wakiwa wamesimama, macho yao yataoza yakiwa kwenye matundu yake, na ndimi zao zitaoza vinywani mwao. 13  “Siku hiyo msukosuko kutoka kwa Yehova utaenea sana miongoni mwao; na kila mtu ataukamata mkono wa mwenzake, na mkono wake utaushambulia mkono wa mwenzake.*+ 14  Watu wa Yuda pia watashiriki katika vita huko Yerusalemu; na utajiri wa mataifa yote jirani utakusanywa, dhahabu na fedha na mavazi kwa wingi sana.+ 15  “Na ugonjwa hatari wa aina hiyo utawashambulia pia farasi, nyumbu, ngamia, punda, na mifugo yote iliyo katika kambi hizo. 16  “Kila mtu atakayebaki kutoka katika mataifa yote yatakayoshambulia Yerusalemu atapanda mwaka baada ya mwaka+ kwenda Yerusalemu kumwinamia* Mfalme, Yehova wa majeshi,+ na kusherehekea Sherehe ya Vibanda.*+ 17  Lakini ikiwa taifa lolote miongoni mwa mataifa yaliyo duniani halitapanda kwenda Yerusalemu kumwinamia Mfalme, Yehova wa majeshi, mvua haitanyesha katika taifa hilo.+ 18  Na ikiwa taifa la Misri halitapanda kwenda Yerusalemu na kuingia humo, halitapata mvua. Badala yake, litashambuliwa na ugonjwa hatari ambao Yehova anauleta kwa mataifa ambayo hayapandi kwenda kusherehekea Sherehe ya Vibanda. 19  Hiyo ndiyo itakayokuwa adhabu kwa sababu ya dhambi ya Misri na dhambi ya mataifa yote ambayo hayatapanda kwenda kusherehekea Sherehe ya Vibanda. 20  “Siku hiyo maneno ‘Utakatifu ni wa Yehova!’+ yataandikwa kwenye kengele za farasi. Na vyungu vya kupikia*+ vilivyo katika nyumba ya Yehova vitakuwa kama mabakuli+ yaliyo mbele ya madhabahu. 21  Na kila chungu cha kupikia* kilicho Yerusalemu na Yuda kitakuwa kitakatifu na kitakuwa cha Yehova wa majeshi, na wale wote wanaotoa dhabihu wataingia na kutumia baadhi ya vyungu hivyo kuchemshia. Siku hiyo hakutakuwa tena na Mkanaani* katika nyumba ya Yehova wa majeshi.”+

Maelezo ya Chini

Yaani, jiji linalotajwa katika mstari wa 2.
Au “mawio ya jua.”
Tnn., “kwenye ile bahari.”
Au “vitakakamazwa,” kana kwamba vimekakamazwa na baridi.
Yaani, Bahari ya Mediterania.
Yaani, Bahari ya Chumvi.
Au “mitungi ya kushinikizia divai.”
Au “mtu atamshambulia mwenzake.”
Au “Vibanda vya Muda.”
Au “kumwabudu.”
Au “vyungu vya kupikia vyenye mdomo mpana.”
Au “chungu cha kupikia chenye mdomo mpana.”
Au labda, “mfanyabiashara.”